43. Mpwekeshaji ambaye si msomi anawashinda wanachuoni elfu wa washirikina

Mtu ambaye si msomi katika wapwekeshaji anashinda watu elfu katika wanachuoni wa washirikina hawa. Kama alivyosema (Ta´ala):

وَإِنَّ جُندَنَا لَهُمُ الْغَالِبُونَ

”Hakika jeshi Letu ndilo litakaloshinda.” (asw-Swaaffaat 37 : 173)

MAELEZO

Haya ni katika maajabu kuona mpwekeshaji ambaye si msomi anawashinda wanachuoni elfu wa washirikina. Hili ni kwa sababu yule ambaye si msomi bado maumbile yake ni salama ambayo hayajachafuka na mashaka, dhana, kanuni za mantiki na elimu ya falsafa. Kuhusu mwanachuoni mshirikina hana maumbile yaliyosalimika wala elimu sahihi. Ambaye ana maumbile yaliyosalimika anamshinda ambaye hana maumbile wala elimu. Kwa kuwa elimu yake ni ujinga. Kwa hiyo watu wamegawanyika sampuli tatu:

Ya kwanza: Ambaye ana elimu sahihi na maumbile yaliyosalimika. Hii ndio ngazi ya juu kabisa. Huyu ni yule amemkimbilia Mola Wake na akasikiliza hoja Zake na ubainisho Wake. Kwa ajili hiyo akawa na elimu sahihi na maumbile yaliyosalimika.

Ya pili: Ambaye hana elimu lakini hata hivyo akawa na maumbile yaliyosalimika. Huyu ni yule mpwekeshaji ambaye si msomi.

Ya tatu: Ambaye hana maumbile yaliyosalimika wala elimu sahihi. Alichonacho ni udanganyifu tu. Huyu ataanguka mbele ya ambaye si msomi. Vipi kuhusu mbele ya mwanachuoni ambaye ana elimu yake sahihi na maumbile yaliyosalimika? Haya ni miongoni mwa mambo yanayofahamisha ya kwamba kujifunza elimu yenye manufaa inakuwa ni silaha ya yule muumini mbele ya maadui wa Allaah na wa Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 60
  • Imechapishwa: 15/12/2016