Masimulizi hizi sahihi na zinazofanana nazo kutoka kwa maimamu wa Salaf zinahusiana na kujiepusha kwao kuzungumzia tafsiri ya Qur-aan kwa yale wasiyokuwa nayo elimu. Ama yule anayezungumza kuhusu yale anayoyajua kwa misingi ya lugha na Shari´ah, basi hapana vibaya kwake. Hii ni kwa sababu imepokelewa kutoka kwa mabwana hawa na wengineo maoni mbalimbali kuhusu tafsiri. Hakuna mgongano. Walizungumza kuhusu yale waliyoyajua na wakanyamaza kuhusu yale wasiyoyajua. Hivi ndivyo inavyompasa kila mtu. Kama ilivyo wajibu kunyamaza kuhusu jambo ambalo mtu hana elimu nalo, ndivyo pia inavyopaswa kusema kuhusu yale anayoulizwa anayoyajua. Amesema (Ta´ala):

وَإِذْ أَخَذَ اللَّـهُ مِيثَاقَ الَّذِينَ أُوتُوا الْكِتَابَ لَتُبَيِّنُنَّهُ لِلنَّاسِ وَلَا تَكْتُمُونَهُ

“Wakati alipochukua Allaah fungamano la wale waliopewa Kitabu [akawaambia:] “Bila shaka mtakibainisha kwa watu na wala hamtokificha!”[1]

Vilevile kutokana na Hadiyth, iliyopokelewa kwa njia mbalimbali, inayosema:

“Yeyote atakayeulizwa kuhusu elimu akaiyaficha, basi atafungwa mdomo wake siku ya Qiyaamah kwa lijamu ya Moto.”[2]

Ibn Jariyr amesema: Muhammad bin Bashshaar ametuhadithia: Mu-ammal ametuhadithia: Sufyaan ametuhadithia, kutoka kwa Abuz-Zinaad, ambaye amesimulia kwamba Ibn ´Abbaas amesema:

”Qur-aan inatafsiri kwa njia nne: ya kwanza  ambayo waarabu wanaifahamu kutokana na lugha yao, tafsiri ambayo hakuna mtu anayesamehewa kutoijua, tafsiri inayojulikana na wanazuoni na na tafsiri ambayo hakuna anayeijua isipokuwa na Allaah.”[3]

Na Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) ndiye mjuzi zaidi.

[1] 3:187

[2] Abu Daawuud (3658), at-Tirmidhiy (2649) na Ibn Maajah (261). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika “Swahiyh-ut-Targhiyb wat-Tarhiyb” (120).

[3] Jaamiy´-ul-Bayaan (1/57).

  • Muhusika: Shaykh-ul-Islaam Ahmad bin Taymiyyah
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Muqaddimah fiy Usuwl-it-Tafsiyr, uk. 108-109
  • Imechapishwa: 14/04/2025