30. Mitihani inamfanya mtu kunyenyekea na kutubia

Miongoni mwa manufaa yake ni kwamba inafanya kuomba du´aa kwa kumtakasia Allaah nia, ukweli wa kurejea kwa Allaah (Ta´ala), kuelekea na kumnyenyekea kwelikweli yule ambaye hakifichikani Kwake chochote ardhini wala mbinguni:

وَإِن يَمْسَسْكَ اللَّـهُ بِضُرٍّ فَلَا كَاشِفَ لَهُ إِلَّا هُوَ ۖ وَإِن يَمْسَسْكَ بِخَيْرٍ فَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ

“Allaah Akikugusisha dhara, basi hakuna wa kuiondosha isipokuwa Yeye, na akikugusisha kheri, basi Yeye juu ya kila kitu ni Muweza.”[1]

Baadhi ya Salaf wamesema:

“Mwenendo wa Allaah amewafanya waja Wake kumwabudu ili awakunjulie riziki na kuwahifadhia uzima, ili wapate kurejea Kwake (Subhaanah) kwa neema Zake. Wasipofanya hivo, basi anawajaribu kwa maafa na madhara, pengine wakarejea Kwake.”

Miongoni mwa faida za mitihani ni kuyafuta madhambi na makosa na kumpelekea mtu katika ngazi za juu zaidi Peponi. Bora kuliko yote hayo ni kupata radhi za Allaah, Aliyetukuka, ambayo ndio bora kuliko Pepo na neema zake zenye kudumu.

[1] 6:17

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin ´Abdillaah bin Naaswir-id-Diyn ad-Dimashqiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bard-ul-Akbaad ´inda Faqd-il-Awlaad, uk. 113-114
  • Imechapishwa: 27/08/2023