27. Maneno ya ´Abdullaah bin Salaam kuhusu mikono ya Allaah

28- Imesihi kupokelewa kutoka kwa ´Abdullaah bin Salaam ambaye amesema:

“Allaah amemuumba Aadam katika saa ya mwisho ya ijumaa. Kisha akamwacha kwa muda wa siku arubaini akimtazama na kusema: “Amebarikika Allaah, Muumbaji bora kabisa!” Kisha Akampulizia kutoka katika roho Yake. Wakati alipopata sehemu ya roho akaenda kuketi chini ambapo Allaah akasema: “Mtu ameumbwa kuwa na pupa.” Pindi roho nzima ilipoingia ndani mwake akachemua. Allaah akamwambia: “Sema: “Himdi zote anastahiki Allaah.” Akasema: “Himdi zote anastahiki Allaah.” Akamwambia: “Mola wako akurehemu. Nenda kwa Malaika wale kule uwasalimie.” Akafanya hivo ambapo akaambiwa: “Haya ni mamkuzi yako na ya kizazi chako.” Kisha akashika mgongoni mwake kwa mikono Yake ambapo akatoa kizazi chake Atachoumba hadi siku ya Qiyaamah. Kisha akakamata kwa mikono Yake na akasema: “Chagua, ee Aadam!” Akasema: “Nachagua mkono Wako wa kuume – na mikono Yako yote miwili ya kuume.” Akaukunjua na ndani yake kulikuwemo kizazi chake kitachoingia Peponi. Akasema: “Ni kina nani hawa, ee Mola?” Akasema: “Ni kizazi chako hadi siku ya Qiyaamah Nilichokwishapanga kuingia Peponi.” Akaona watu wenye kung´ara ambapo akasema: “Ni kina nani hawa, ee Mola?” Akasema: “Ni Mitume.” Akasema: “Ni nani huyu ambaye ang´ara zaidi?” Akasema: “Ni mwana wako Daawuud.” Akasema: “Umepanga ataishi umri kiasi gani?” Akasema: “Miaka sitini.” Akasema: “Umri wangu ni kiasi gani?” Akasema: “Elfumoja.” Akasema: “Ee Mola! Mzidishie miaka arubaini kutoka kwenye umri wangu.” Akasema: “Ukitaka.” Akasema: “Nataka.” Akasema: “Yataandikwa na kupigwa muhuri na hayatobadilishwa.” Halafu akaona mwishoni mwa kiganja cha mkono cha Mwingi wa huruma mtu ambaye anang´ara zaidi akasema: “Ni nani huyu, ee Mola?” Akasema: “Ni Muhammad. Yeye ni wa mwisho wao na ndiye wa kwanza kuingia Peponi.”

Wakati Malaika wa mauti alipokuja kutoa roho yake akasema: “Nimebaki na miaka arubaini.” Malaika wa mauti akasema: “Wewe sulimpa mwana wako Daawuud?” Aadam amesahau na kizazi chake kimesahau. Amesahau na kizazi chake kimesahau. Amekanusha na kizazi chake kimekanusha. Hiyo ndio siku ya kwanza ambapo ushahidi uliwekwa katika Shari´ah.”[1]

Ibn Battwah ameipokea kwa cheni za wapokezi nyingi kukiwemo: Muhammad bin al-Husayn al-Aajurriy amenikhabarisha: al-Firyaaby amenihadithia: Qutaybah ametuhadithia: Layth ametuhadithia, kutoka kwa Ibn ´Ajlaan, kutoka kwa al-Maqbariy, kutoka kwa baba yake, kutoka kwa ´Abdullaah bin Salaam.

[1] al-Aajurriy katika ”ash-Shariy´ah”, uk. 206, na Ibn Battah katika ”al-Ibaanah” (1591).

  • Mhusika: Imaam Shams-ud-Diyn Muhammad bin Ahmad adh-Dhahabiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ithbaat-ul-Yad li-Laah Swifatan min Swifwaatih, uk. 25-26