24. Makokotezo ya Sutrah kwa mswaliji

Swali 24: Ndugu wengi wanatilia mkazo jambo la Sutrah kiasi cha kwamba wanasubiri kupatikana kwa Sutrah pale ambapo kumekosekana nguzo tupu. Sambamba na hilo wanamkemea ambaye hakuswali kwa kuelekea Sutrah. Baadhi yao wanaichukulia wepesi. Ni yepi ya haki katika hilo? Je, kupiga msitari kunasimama mahali pa Sutrah wakati wa kukosekana kwake? Je, kumepokelewa yanayofahamisha juu ya hayo?

Jibu: Kuswali kwa kuelekea Sutrah ni Sunnah iliyokokotezwa na sio lazima. Asipopata kitu kilichosimikwa basi kutasihi kupiga msitari. Hoja juu ya yale tuliyoyataja ni maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Atakaposwali mmoja wenu basi aswali kwa kuelekea Sutrah na awe karibu nayo.”

Ameipokea Abu Daawuud kwa mlolongo wa wapokezi Swahiyh.

Amesema tena (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Swalah ya mtu muislamu inakatika kusipokuwa mbele yake mfano wa bakora ya anayepanda kipando: mwanamke, punda na mbwa mweusi.”

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake.

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Pindi anaposwali mmoja wenu basi aweke mbele ya uso wake kitu, asipopata basi asimike bakora na asipopata basi apige msitari kisha hatomdhuru ambaye anapita mbele yake.”

Ameipokea Imaam Ahmad na Ibn Maajah kwa cheni ya wapokezi nzuri.

Haafidhw Ibn Hajar (Rahimahu Allaah) amesema katika “Buluugh-ul-Maraam”:

“Imethibiti kutoka kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuwa baadhi ya nyakati ameswali kwa kutoelekea Sutrah. Kwa hivyo imefahamisha kuwa sio lazima.”

Kunavuliwa katika hayo kuswali katika msikiti Mtakatifu. Mswaliji hahitajii Sutrah. Imethibiti kutoka kwa Ibn-uz-Zubayr (Radhiya Allaahu ´anhumaa):

“Ya kwamba alikuwa akiswali katika msikiti Mtakatifu kwa kutoelekea Sutrah na kunafanywa Twawaaf mbele yake.”

Vilevile kumepokelewa kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yanayofahamisha hayo. Lakini cheni ya wapokezi wake ni dhaifu.

Jengine ni kwamba mara nyingi msikiti Mtakatifu ni maeneo pa msongamano na haiwezekani mswaliji asipite mbele ya wanaoswali. Kwa hivyo ikadondoka Shari´ah ya jambo hilo kutokana na yaliyotangulia.

Kunaambatana na hilo msikiti wake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wakati wa msongamano. Vivyo hivyo maeneo mengine ambayo kuna msongamano. Yote hayo kwa ajili ya kutendea kazi maneno Yake (´Azza wa Jall):

فَاتَّقُوا اللَّـهَ مَا اسْتَطَعْتُمْ

”Mcheni Allaah muwezavyo.”[1]

Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Nikikuamrisheni jambo basi lifanyeni muwezavyo.”

Kuna maafikiano juu ya usahihi wake.

[1] 64:16

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fataawaa Muhimmah, uk. 26-27
  • Imechapishwa: 18/08/2022