Baya zaidi kuliko hivo ni shirki na kuyaabudia makaburi. Watu wengi leo wanaojidai kuwa ni waislamu wanayaabudia makaburi na wanasema kuwa kitendo hicho ndio Tawhiyd na kuwaadhimisha waja wema na kutambua nafasi yao. Hiyo ni shirki na kumwabudu mwingine asiyekuwa Allaah. Turejee wapi katika mzozo wetu huu? Tunaurudisha katika Qur-aan na Sunnah. Qur-aan na Sunnah vyote viwili vinashuhudia ya kwamba anayemwabudu mwengine asiyekuwa Allaah ni mshirikina, pasi na kujali anachokiabudu kiko hai, kimeshakufa, mti, jiwe, Malaika, Mtume au mja mwema:

وَأَنَّ الْمَسَاجِدَ لِلَّـهِ فَلَا تَدْعُوا مَعَ اللَّـهِ أَحَدًا

“Sehemu zote za kuswalia ni kwa ajili ya Allaah, hivyo basi msiombe yeyote pamoja na Allaah.”[1]

Haijalishi kitu ni nani au ni kitu gani. ´Ibaadah ni haki ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) pekee na ndio lengo la viumbe kuubwa:

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ

“Na Sikuumba majini na wanadamu isipokuwa waniabudu.”[2]

Ukichukia haki ya Allaah na ukampa nayo mwengine na ukamwabudu mwengine, unakuwa mshirikina na kafiri. Ni wajibu kuzindukana juu ya jambo hili. Mizozo, magomvi na tofauti zetu zote tunatakiwa kuzirudisha katika Qur-aan na Sunnah. Muhimu zaidi katika mambo hayo ni suala la ´Aqiydah. Hatutakiwi kurejea katika maoni na fikira ya fulani. Hakuna njia nyingine ya kutatua mzozo isipokuwa hii. Yule anayetulingania katika kitu kingine kisichokuwa hicho anatulingania katika upotofu na anatutoa kutoka katika nuru na kutuingiza katika viza:

اللَّـهُ وَلِيُّ الَّذِينَ آمَنُوا يُخْرِجُهُم مِّنَ الظُّلُمَاتِ إِلَى النُّورِ ۖ وَالَّذِينَ كَفَرُوا أَوْلِيَاؤُهُمُ الطَّاغُوتُ يُخْرِجُونَهُم مِّنَ النُّورِ إِلَى الظُّلُمَاتِ

“Allaah ni mlinzi wa wale ambao wameamini; Anawatoa kutoka katika viza na  kuwaingiza katika nuru.  Na wale ambao wamekufuru walinzi  wao ni Twaaghuut; huwatoa kutoka katika nuru na kuwaingiza katika viza.”[3]

Wanawatoa katika kufuata Qur-aan na Sunnah na badala yake kufuata vyenginevyo, kwa maana nyingine viza.

[1] 72:18

[2] 51:56

[3] 2:257

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaaa al-Hamawiyyah, uk. 50-51
  • Imechapishwa: 30/07/2024