14. Kuamini uola wa Allaah hakukingi damu na mali ya mtu

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Ukishahakikisha ya kwamba walikuwa wanakubali hili, na hili halikuwaingiza katika Tawhiyd ambayo aliwalingania kwayo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), na ukajua ya kwamba Tawhiyd waliyoipinga ni Tawhiyd al-´Ibaadah ambayo washirikina katika zama zetu wanaiita “al-I´tiqaad”.

Na walikuwa wakimuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) usiku na mchana. Halafu katika wao kulikuwa wanaowaomba Malaika kwa ajili ya wema wao na ukaribu wao kwa Allaah (Ta´ala) ili [Malaika hao] wawaombee, au wanaomba mtu mwema; kama mfano wa al-Laat, Mtume kama mfano wa ´Iysaa. Na umejua ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kapigana nao vita kwa shirki hii na akawalingania kumtakasia ´ibaadah Allaah peke Yake. Kama Alivyosema Allaah (Ta´ala):

لَهُ دَعْوَةُ الْحَقِّ ۖ وَالَّذِينَ يَدْعُونَ مِن دُونِهِ لَا يَسْتَجِيبُونَ لَهُم بِشَيْءٍ

“Kwake ndiko kunaelekezwa maombi yote ya haki. Na wale wanaoomba pasi Naye hawawaitikii kwa chochote.” (13:14)

Na umehakikisha ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kawapiga vita ili maombi yote atekelezewe Allaah, kuchinja kote kuwe kwa Allaah, uwekaji wa nadhiri wote uwe kwa Allaah, kuchinja kote kuwe kwa Allaah, kuomba uokozi [al-Istighaathah] yote afanyiwe Allaah na jumla ya ´Ibaadah zote afanyiwe Allaah. Na umejua kuwa kukubali kwao Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah hakukuwaingiza katika Uislamu. Na kwamba kuwakusudia kwao Malaika, au Mitume, au mawalii walikuwa wanataka maombezi yao na kujikurubisha kwa Allaah kwa hilo, Yeye ndiye Ambaye kahalalisha damu yao na dini na mali yao. Hivyo utakuwa umejua Tawhiyd waliyoilingania kwayo Mitume na washirikina wakakataa kuikubali.

MAELEZO

Kunakusudiwa washirikina ambao Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alitumwa kwao. Walikuwa wakikubali Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah, ambayo ni kuitakidi kuwa Allaah peke Yake ndiye Muumbaji, Mmiliki na Mwendeshaji wa mambo yote.

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“… na hili halikuwaingiza katika Tawhiyd ambayo aliwalingania kwayo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).”

Imani yao ya kuamini kuwa Allaah peke Yake ndiye Muumbaji, Mmiliki na Mwendeshaji wa mambo yote haikuwafanya kuingia katika Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah ambayo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiwalingania kwayo. Wala hakuifanya damu na mali yao isichukuliwe.

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“… na ukajua ya kwamba Tawhiyd waliyoipinga ni Tawhiyd-ul-´Ibaadah ambayo washirikina katika zama zetu wanaiita “al-I´tiqaad.”

Ukitambua kuwa walichokuwa wanapinga ilikuwa ni Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah, ambayo washirikna wa zama hizi wanaita kuwa ni “al-I´tiqaad”, itakubainikia kuwa kile walichokuwa wakikithibitisha hakitoshelezi kuihakikisha Tawhiyd. Bali uhakika wa mambo ni kuwa haitoshelezi kumfanya mtu akawa ni muislamu. Yule asiyethibitisha Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah sio muislamu, hata kama atathibitisha Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah. Ndio maana Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwapiga vita washirikina, pamoja na kuwa wanathibitisha Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah.

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“… na walikuwa wakimuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) usiku na mchana…”

Washirikina hawa walikuwa wakimuomba Allaah (Ta´ala) wanapokumbwa na majanga. Wengine wakiwaomba Malaika kutokamana na ukaribu wao mbele ya Allaah (´Azza wa Jall). Walikuwa wakidai kuwa ambaye yuko karibu na Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) yuko na haki ya kuabudiwa. Hili linathibitisha ujinga wao. Hakika ´ibaadah ni haki ya Allaah pekee na hashirikiani na yeyote yule. Kuna ambao walikuwa wakimuomba al-Laat. al-Laat alikuwa ni bwana ambaye anawatengenezea uji mahujaji. Alipofariki, wakawa wanabaki kwenye kaburi lake kwa muda mrefu na baadaye wakamwabudu. Wengine walikuwa wakimuabudu ´Iysaa (´alayhis-Salaam) kwa sababu alikuwa ni alama ya Allaah. Wako ambao walikuwa wakiwaabudu mawalii kwa sababu wako karibu na Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala). Yote haya yanatokamana na kwamba shaytwaan aliwapambia matendo yao ambayo wakapotea kwayo kutoka katika Njia iliyonyooka. Allaah (Ta´ala) amesema:

قُلْ هَلْ نُنَبِّئُكُم بِالْأَخْسَرِينَ أَعْمَالًا الَّذِينَ ضَلَّ سَعْيُهُمْ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَهُمْ يَحْسَبُونَ أَنَّهُمْ يُحْسِنُونَ صُنْعًا أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ كَفَرُوا بِآيَاتِ رَبِّهِمْ وَلِقَائِهِ فَحَبِطَتْ أَعْمَالُهُمْ فَلَا نُقِيمُ لَهُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَزْنًا

“Sema: “Je, Tukujulisheni wale waliokhasirika matendo yao? Ni wale ambao wamepoteza juhudi zao katika uhai wa dunia nao huku wakidhani kwamba wanatenda vizuri katika kutenda – hao ni wale waliozikanusha Aayah za Mola wao na [pia wakakanusha] kukutana Naye; basi yameporomoka matendo yao. Hivyo Hatutowasimamishia Siku ya Qiyaamah mizani.” (18:103-105)

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“… na umejua ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kapigana nao vita kwa shirki hii… “

Aliposema “kwa shirki hii” kunamaanishwa ya kwamba walikuwa wakiwaabudu wengine badala ya Allaah. Makusudio sio shirki katika Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah. Washirikina ambao Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alitumilizwa kwao, walikuwa wakiamini kuwa Allaah peke Yake ndiye Mola. Walikuwa wakikubali kuwa Yeye ndiye anajibu du´aa ya mwenye kudhikika, kwamba anaondosha majanga na mengineyo ambayo Allaah ameyataja juu yao, jambo lenye kufahamisha kuwa walikuwa wakithibitisha uola wa Allaah (´Azza wa Jall).

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akawapiga vita washirikina hawa ambao walikuwa hawathibitishi Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah. Bali uhakika wa mambo ni kuwa alihalalisha damu na mali yao, hata kama walikuwa wakikubali kwamba Allaah peke Yake ndiye Muumbaji, kwa sababu hawakumuabudu na hawakumtakasia ´ibaadah.

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“… na akawalingania kumtakasia ´ibaadah Allaah peke Yake… “

Kumtakasia ´ibaadah Allaah maana yake ni mtu akusudie kwa ´ibaadah yake kujikurubisha kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) na kufikia Pepo Yake. Masanamu haya ambayo wanayaomba badala ya Allaah hayawezi kuwajibu kwa chochote. Amesema (Ta´ala):

وَمَنْ أَضَلُّ مِمَّن يَدْعُو مِن دُونِ اللَّـهِ مَن لَّا يَسْتَجِيبُ لَهُ إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ وَهُمْ عَن دُعَائِهِمْ غَافِلُونَ وَإِذَا حُشِرَ النَّاسُ كَانُوا لَهُمْ أَعْدَاءً وَكَانُوا بِعِبَادَتِهِمْ كَافِرِينَ

“Na nani aliyepotoka zaidi kuliko ambaye anayeomba asiyekuwa Allaah ambaye hamuitikii mpaka Siku ya Qiyaamah; nao kuhusu du’aa zao ni wenye kughafilika. Na [Qiyaamah] watakapokusanywa watu [miungu ya uongo] watakuwa maadui wao na watakuwa kwa ‘ibaadah zao ni wenye kuzikanusha.” (46:05-06)

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“Na umehakikisha ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kawapiga vita ili du´aa [maombi] yote atekelezewe Allaah… “

Kuna sampuli mbili za du´aa:

1 – Du´aa ambayo ni ´ibaadah. Aina hii ni yule mwenye kuombwa anaabudiwa na wakati huohuo mtu anataka thawabu kutoka kwake na anachelea adhabu yake. Hili halisihi kwa mwengine asiyekuwa Allaah. Kumtekelezea aina hii asiyekuwa Allaah ni shirki kubwa inayomtoa mwenye nayo katika Uislamu. Mtu kama huyo anatumbukia katika makemeo ya maneno Yake (Ta´ala):

إِنَّ الَّذِينَ يَسْتَكْبِرُونَ عَنْ عِبَادَتِي سَيَدْخُلُونَ جَهَنَّمَ دَاخِرِينَ

“Hakika wale wanaotakabari na ‘ibaadah Yangu wataingika [Moto wa] Jahannam hali ya kudhalilika.” (40:60)

2 – Du´aa ya kuomba. Du´aa hii inahusiana na kuomba mahitaji mbalimbali na imegawanyika sehemu tatu:

1 – Kumuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) kitu asichokiweza yeyote asiyekuwa Yeye. Hii inazingatiwa kuwa ni ´ibaadah anayotekelezewa Allaah (Ta´ala) peke Yake, kwa kuwa ina maana ya kumnyenyekea Allaah (Ta´ala), kumwelekea na kuitakidi kuwa Yeye ndiye Muweza na Mkarimu mwenye fadhilah na rehema kunjufu. Kwa hivyo, yule mwenye kumuomba mwengine asiyekuwa Allaah kwa kitu kisichoweza yeyote zaidi ya Allaah, ni mshirikina na kafiri. Ni mamoja ikiwa yule mwenye kuombwa yuko hai au ameshakufa.

2 – Kumuomba mtu aliye hai kwa kitu anachoweza kukifanya. Mfano wa hilo ni kama kumuomba mtu maji. Kitendo hichi kinajuzu.

3 – Kumuomba maiti au mtu asiyekuwepo kwa kitu mfano wa hicho. Kitendo hicho ni shirki kwa kuwa maiti wala mtu asiyekuwepo hawezi kufanya kitu hicho. Kwa hivyo kile kitendo chake cha yeye kumuomba kinafahamisha kwamba anaamini kuwa mtu huyo ana nguvu fulani ya uendeshaji ulimwengu. Hili linamfanya mtu huyo kuwa mshirikina.

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“… kuchinja kote kuwe kwa Allaah… “

Kuchinja ni kutoa uhai kwa kumwaga damu kwa njia maalum. Sampuli zake ni zifuatazo:

1 – Mtu akusudie kumuadhimisha yule anayemchinjia, kujidhalilisha na kujikurubisha kwake. Hii ni ´ibaadah ambayo hafanyiwi yeyote isipokuwa Allaah (Ta´ala) pekee kwa njia ile alioiweka katika Shari´ah. Kumtekelezea aina hii mwengine asiyekuwa Allaah ni shirki kubwa. Amesema (Ta´ala):

قُلْ إِنَّ صَلَاتِي وَنُسُكِي وَمَحْيَايَ وَمَمَاتِي لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ لَا شَرِيكَ لَهُ ۖ وَبِذَٰلِكَ أُمِرْتُ وَأَنَا أَوَّلُ الْمُسْلِمِينَ

“Sema: “Hakika swalah yangu na kichinjwa changu na uhai wangu na kufa kwangu ni kwa ajili ya Allaah pekee, Mola wa walimwengu. Hana mshirika, na kwa hayo ndio nimeamrishwa, nami ni muislamu wa kwanza.”” (37:162-163)

2 – Mtu akusudie kumkirimu mgeni, chakula cha harusi na mfano wa hayo. Haya yameamrishwa ima ni wajibu au ni jambo linapendeza. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Yule anayemwamini Allaah na siku ya Mwisho, basi amkirimu mgeni wake.”[1]

Vilevile alimwambia ´Abdur-Rahmaan bin ´Awf pindi alipooa:

“Fanya karamu ya ndoa, ijapokuwa kondoo mmoja.”[2]

3 – Mtu akusudie kujiburudisha kwa chakula, kufanya biashara kwayo na mfano wa hayo. Kitendo hichi kimeruhusiwa. Msingi ni kuwa kinaruhusiwa. Amesema (Ta´ala):

أَوَلَمْ يَرَوْا أَنَّا خَلَقْنَا لَهُم مِّمَّا عَمِلَتْ أَيْدِينَا أَنْعَامًا فَهُمْ لَهَا مَالِكُونَ وَذَلَّلْنَاهَا لَهُمْ فَمِنْهَا رَكُوبُهُمْ وَمِنْهَا يَأْكُلُونَ

“Je, hawaoni kwamba Sisi tumewaumbia kutokana na yale iliyofanya mikono Yetu; wanyama wa mifugo – basi wao wanawamiliki? Na Tumewadhalilisha kwao, basi baadhi yao humo ni vipando vyao na wengine humo wanawala?” (36:71-72)

Kitendo hichi pia kinaweza kuwa chenye kutakikana au chenye kukatazwa. Itategemea na itatumiwa kwa ajili ya kitu gani.

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“… uwekaji wa nadhiri wote uwe kwa Allaah… “

´Ibaadah zote zilizofaradhishwa mtu anaweza kuita kuwa ni “nadhiri”. Lakini hata hivyo maana yake maalum ni mtu kujilazimishia mwenyewe kufanya kitu kwa ajili ya Allaah (´Azza wa Jall). Lakini makusudio hapa ni ile maana ya kwanza. ´Ibaadah zote anatekelezewa Allaah (Ta´ala) pekee. Amesema:

وَقَضَىٰ رَبُّكَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ

“Na Mola wako amehukumu kwamba: “Msiabudu yeyote isipokuwa Yeye pekee.” (17:23)

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“… kuomba uokozi [al-Istighaathah] yote afanyiwe Allaah… ”

Maana yake ni kuomba msaada na uokozi wakati wa matatizo na maangamivu. Jambo hili limegawanyika sehemu mbalimbali:

1 – Kumuomba uokozi Allaah (´Azza wa Jall). Haya ni katika matendo bora na kamilifu zaidi. Jambo hilo ni miongoni mwa matendo ya Mitume (Swalla Allaahu ´alayim wa sallam) na wafuasi wao. Dalili ya hilo ni maneno Yake (Ta´ala):

إِذْ تَسْتَغِيثُونَ رَبَّكُمْ فَاسْتَجَابَ لَكُمْ أَنِّي مُمِدُّكُم بِأَلْفٍ مِّنَ الْمَلَائِكَةِ مُرْدِفِينَ

“Na pale mlipomuomba uokozi Mola wenu Naye akakujibuni kuwa: “Hakika Mimi nitakusaidieni kwa Malaika elfu wafuatanao mfululizo.”” (08:09)

2 – Kuwaomba uokozi maiti au watu wasiokuwepo mbele yako na watu wasiokuwa na uwezo. Kitendo hichi ni shirki, kwa sababu hakuna anayefanya hivo isipokuwa tu yule anayeamini kuwa watu hawa wana nguvu fulani za kuendesha ulimwengu. Hivyo amewajaalia sehemu katika uola. Allaah (Ta´ala) amesema:

أَمَّن يُجِيبُ الْمُضْطَرَّ إِذَا دَعَاهُ وَيَكْشِفُ السُّوءَ وَيَجْعَلُكُمْ خُلَفَاءَ الْأَرْضِ ۗ أَإِلَـٰهٌ مَّعَ اللَّـهِ ۚ قَلِيلًا مَّا تَذَكَّرُونَ

“Au nani anayemuitika aliyedhikika anapomwomba na akamuondoshea dhiki na akakufanyeni makhalifa wa ardhi? Je, yuko mungu wa haki mwengine pamoja na Allaah? Ni machache mno mnayokumbuka.” (27:62)

3 – Kuwaomba uokozi walio hai, watendaji na watu wenye uwezo. Kitendo hichi kinajuzu ni kama mfano wa kuwataka msaada. Allaah (Ta´ala) amesema kuhusu Muusa (´alayhis-Salaam):

فَاسْتَغَاثَهُ الَّذِي مِن شِيعَتِهِ عَلَى الَّذِي مِنْ عَدُوِّهِ فَوَكَزَهُ مُوسَىٰ فَقَضَىٰ عَلَيْهِ

“Akamsaidia yule ambaye ni katika kundi lake dhidi ya yule ambaye ni katika adui wake, Muusa akampiga ngumi akamuua.” (28:15)

4 – Kumuomba uokozi mtu aliye hai lakini asiyekuwa na uwezo pasi na mtu huyo kuamini kuwa ana nguvu fulani zilizojificha. Mfano wa hilo ni kama kumuomba uokozi mtu ambaye amepoza mwili dhidi ya adui mwenye kushambulia. Hili si jengine isipokuwa ni upumbavu na ni kumfanyia maskhara yule mpozaji. Kwa ajili hiyo kitendo hichi hakijuzu kutokana na hii sababu. Sababu nyingine ni kuwa wengine wanaweza kufikiria kuwa mtu huyu ambaye si muweza pengine yuko na nguvu fulani zilizojificha ambazo anaweza kwazo kuokoa wakati wa matatizo.

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“Na umehakikisha ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kawapiga vita ili du´aa na maombi yote atekelezewe Allaah… “

Mtunzi (Rahimahu Allaah) anazidi kukariri ya kuwa Tawhiyd ambayo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuja nayo kutoka kwa Allaah ni Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah. Washirikina ambao Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alitumwa kwao, walikuwa wakithibitisha Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah. Pamoja na hayo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alihalalisha damu na mali zao. Sababu ilikuwa wanaabudu Malaika, mawalii na watu wema. Kwa kufanya hivo walikuwa wanakusudia wawakurubishe mbele ya Allaah. Ni kama alivyosema Allaah (Ta´ala):

وَالَّذِينَ اتَّخَذُوا مِن دُونِهِ أَوْلِيَاءَ مَا نَعْبُدُهُمْ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَا إِلَى اللَّـهِ زُلْفَىٰ

“Na wale wanaowafanya wengine badala Yake kuwa walinzi [wakisema]: “Hatuwaabudu isipokuwa kwa lengo la kutukurubisha kwa Allaah ukaribu.” (39:03)

Walikuwa wakikubali ya kwamba Allaah ndiye mkusudiwa, lakini kadhalika wanawatumia Malaika na wengineo ili wawakurubish mbele ya Allaah. Pamoja na hivyo hawakuingia katika Tawhiyd.

[1] al-Bukhaariy (6018) na Muslim (74).

[2] al-Bukhaariy (5167) na Muslim (1427).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 24-26
  • Imechapishwa: 23/04/2022