30 – Mansuur bin ´Ammaar, mtoa mawaidha wa zama zake.

169 – Hakimu wa Hijr Sulmuuyah bin ´Aaswim amesema:

”Bishr al-Mariysiy aliniandikia barua kwenda kwa Mansuur bin ´Ammaar akiulizwa kuhusu maneno Yake Allaah (Ta´ala):

الرَّحْمَـٰنُ عَلَى الْعَرْشِ اسْتَوَىٰ

”Mwingi wa rehema amelingana juu ya ´Arshi.”

Akamwandikia akimjibu: ”Kulingana Kwake hakuna kikomo na jawabu ya swali hilo ni kujikakama. Kuuliza kwako jambo hilo ni Bid´ah na kuyaamini yote hayo ni wajibu. Amesema (Ta´ala):

فَأَمَّا الَّذِينَ فِي قُلُوبِهِمْ زَيْغٌ فَيَتَّبِعُونَ مَا تَشَابَهَ مِنْهُ ابْتِغَاءَ الْفِتْنَةِ وَابْتِغَاءَ تَأْوِيلِهِ

”Basi wale ambao katika nyoyo zao mna upotevu hufuata zile zisizokuwa wazi ili kutafuta fitina na kutafuta kuzipotosha.”[1]

Mansuur bin ´Ammaar alikuwa ni kielelezo inapokuja katika mawaidha na kuzitikisa nyoyo. Siku moja aliongoza swalah ya kuomba Mvua wakateremshiwa mvua. Matokeo yake Layth akampa kijakazi na dinari elfu moja.

[1] 03:07 Ameipokea al-Khatwiyb katika wasifu wa Mansuur kwenye “Taariykh Baghdaad” (13/75-76) kupitia kwa Abu ´Aliy al-Husayn bin al-Qaasim al-Kawkabiy: Jariyr bin Ahmad bin Abiy Du-aad Abu Maalik ametuhadithia: Hakimu wa Hijr Sulmuuyah bin ´Aaswim, ambaye alifanya kazi katika bara arabu na Shaam, amenihadithia.

Cheni ya wapokezi ni dhaifu. Haafidhw Ibn Hajar amesema kuhusu al-Kawkabiy:

”Msimulizi wa khabari zinazojulikana. Nimeona akisimulia masimulizi mengi dhaifu na yenye kugongana yakiwa na cheni za wapokezi nzuri.” (Lisaan-ul-Miyzaan)

Halafu akaeleza khabari za mabwana wawili, ambapo mmoja wao ni Ibn Jurayj, ambaye alikuwa ameketi katika msikiti wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), ambapo mmoja akamkemea mwenzie. Ndipo Ibn Jurayj akamwambia: ”Sisi tuko katika moja ya mabustani ya Peponi. Ndani ya Pepo kuna yale ambayo yanatamaniwa na nafsi.”

Haafidhw amesema:

”Akataja kisa cha ajabu ambacho usahihi wake uko mbali kabisa. Kinachotilia nguvu ubatilifu wake ni… ”

Sikuwajua hao mabwana wawili wengine kabla yake. Rejea “Taariykh Dimashq” ya Ibn ´Asaakir juu ya wasifu wa Salmuuyah bin ´Aaswim.

Ameipokea ´Abdullaah katika ”as-Sunnah”, uk. 24: ”´Uthmaan bin Abiy Shaybah amenihadithia:

”Mimi, Abu Bakr na Abu Muhammad (bi maana nduguze ´Abdullaah na al-Qaasim) tulikuwa kwa Sufyaan bin ´Uyaynah wakati Mansuur bin ´Ammaar alipouliza: ”Je, Qur-aan ni kiumbe?” Sufyaan akakaripia swali lake, akakasirika sana na kusema: ”Mimi naona kuwa wewe ni shaytwaan. Mimi naona kuwa wewe ni shaytwaan. Bali wewe ni shaytwaan.” Kukasemwa: ”Ee Abu Muhammad! Ni mtu wa Sunnah.” Akakataa kusikiliza na kukaripia swali lake.”

Pengine al-´Uqayliy kumtuhumu Mansuur kuwa na ´Aqiydah ya Jahmiyyah kunatokana na kisa hiki. Hata hivyo ni jambo liko wazi ya kwamba kile kitendo chake cha yeye kuuliza kama Qur-aan ni kiumbe hakifahamishi kuwa anayo ´Aqiydah ya Jahmiyyah, kwa sababu kuna uwezekano anaonelea kuwa Qur-aan sio kiumbe na kwamba aliuliza tu swali hilo ili kutaka kupata zaidi kutoka katika elimu ya yule muulizwaji – na Allaah ndiye mjuzi zaidi.

  • Mhusika: Imaam Shams-ud-Diyn Muhammad bin Ahmad adh-Dhahabiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Uluww lil-´Aliy al-Ghaffaar, uk. 154
  • Imechapishwa: 22/07/2024
  • taaliki: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy