119. Ambaye ameshawishiwa na mashaytwaan akiwa ni mwenye kukanganyika

91 – ´Abdul-´Aziyz bin Abiy Salamah al-Maajaashuun (afk. 164), mtoa fatwa na mwanachuoni wa Madiynah pamoja na Maalik.

91 – Imesihi kwamba Ibn-ul-Maajaashuun amesema wakati alipoulizwa kuhusu yale yaliyokanushwa na Jahmiyyah:

“Nimefahamu kuwa unauliza kuhusu yale ambayo Jahmiyyah na wale wapinzani wao wanaonelea kuhusu sifa za Mola Mtukufu ambaye utukufu Wake unapita maelezo na makadirio. Ndimi zinashindwa kufasiri sifa Zake na akili zinashindwa kuelewa uwezo Wake. Ukuu Wake umekataliwa na akili na haikupata njia isipokuwa kurudi hali ya kuwa imehizika, imenyong’onyea. Hakuna kingine walichoamrishwa isipokuwa kutazama na kutafakari katika yale Aliyoumba kwa ukamilifu wake. Swali “Vipi?” huulizwa kwa kitu ambacho hakikuwepo kisha baadaye kikawepo. Kuhusu Yule ambaye habadiliki wala hapotei na wala hakuna mfano Wake hakuna anayejua namna alivyo isipokuwa Yeye tu. Ni vipi atajulikana kiwango Chake Yule ambaye hakuzaliwa, hafi na wala hateketei? Ni vipi sifa Zake zitaambatanishwa na mpaka na mwisho? Mtambuzi ndiye anamjua na msifiaji ndiye anathibitisha kiwango Chake juu ya kwamba Yeye ni wa Haki ilio wazi – hakuna haki ambayo ni haki zaidi kuliko Yeye, hakuna chochote ambacho kiko wazi zaidi kuliko Yeye. Dalili ya kwamba akili haiwezi kuelewa sifa Zake ni kwamba haiwezi hata kuzielewa sifa za viumbe vilivyo vidogo zaidi; ni ndogo sana kiasi cha kwamba zinakaribia kutoziona. Zinabadilika na kupotea wala hakuonekani masikizi wala maono yao. Kwa sababu yale wanayoyafanya na kuyadhania yamejificha zaidi kwako kuliko yale yanayodhihiri katika masikizi na maono yao. Amebarikika Allaah, mbora wa waumbaji, Muumbaji wao, Bwana wa mabwana wao na Mola wao:

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖوَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia yote, Mwenye kuona yote.”[1]

Allaah akulinde kutokana na kupekua sifa ambayo Allaah hakujisifu nayo Mwenyewe, kwa sababu huwezi kumkadiria yale aliyojisifu Mwenyewe. Ikiwa huwezi kumkadiria yale aliyojisifu Mwenyewe, ni vipi basi unaweza kupekua yale ambayo hakujisifu? Utafanya hayo kwa ajili ya kumtii au utaepuka kitu katika yale aliyoyakataza? Yule anayejikakama na kupinga kitu katika yale ambayo Mola amejisifu Mwenyewe basi ameshawishiwa na mashaytwaan akikanganyika katika ardhi. Matokeo yake akawa anajengea dalili kwa kukanusha kwake sifa za Mola kwa dhana ambayo kwayo amepofushwa kuyaona yaliyo wazi kwa kupendelea yaliyojificha. Akakanusha yale aliyojiita Mwenyewe kwa kupendelea ambayo hakujiita Mwenyewe. Shaytwaan akaendelea kumshawishi mpaka akakanusha maneno Yake (´Azza wa Jall):

وُجُوهٌ يَوْمَئِذٍ نَّاضِرَةٌ إِلَىٰ رَبِّهَا نَاظِرَةٌ

“Kuna nyuso siku hiyo zitanawiri. Zikimtazama Mola wake.”[2]

Matokeo yake akasema kuwa hakuna yeyote atakayemuona siku ya Qiyaamah. Naapa kwa Allaah! Neema tukufu zaidi ambayo Allaah atawatunuku mawalii Wake siku ya Qiyaamah ni wao kutazama uso Wake na Yeye kuwatazama:

فِي مَقْعَدِ صِدْقٍ عِندَ مَلِيكٍ مُّقْتَدِرٍ

“… katika makao ya haki kwa Mfalme Mwenye nguvu zote, Mwenye uwezo wa juu kabisa.”[3]

Amehukumu kuwa hawatokufa na nyuso zao zitang´ara kwa furaha kwa kule kumwangalia.”

Kisha akasema:

“Amekanusha kuonekana kwa Allaah siku ya Qiyaamah kwa ajili ya kusimamisha hoja potofu na yenye kupotosha. Kwa sababu anajua kuwa ikiwa Atajionyesha siku ya Qiyaamah, wataona kile ambacho kabla ya hapo walikuwa wakikiamini na yeye mtu huyo alikuwa akikikanusha. Waislamu wamesema:

“Ee Mtume wa Allaah! Je, sisi tutamuona Mola wetu siku ya Qiyaamah?” Mtume wa Allaah akasema: “Je, kwani nyinyi mnasongamana katika kutazama jua mchana kweupee pasipo mawingu?” Wakasema: “Hapana, ee Mtume wa Allaah.” Ndipo akasema: “Basi vivyo hivyo ndivo mtamuona Mola wenu siku ya Qiyaamah.”[4]

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Moto hautojaa mpaka pale ambapo al-Jabbaar atapoweka ndani mguu Wake ambapo useme: “Tosha, tosha.” Ndipo uungane.”[5]

Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kumwambia Thaabit bin Qays (Radhiya Allaahu ´anh):

“Allaah amecheka kutokana na kile ulichomfanyia mgeni wako jana usiku.”[6]

Akataja mlango mrefu juu ya mada hiyo. Ameyapokea Abu Bakr al-Athram.

´Abdul-´Aziyz alikuwa ni mmoja katika bahari za elimu Hijaaz. Siku moja kulitolewa wito Madiynah kwa amri ya Mansuur:

“Hakuna yeyote anayo haki ya kuwatolea watu fatwa zaidi ya Maalik na ´Abdul-´Aziyz al-Maajaashuun!”

Ibn-ul-Maajaashuun alifariki mwaka wa 164. Mwanae ´Abdul-Malik alikuwa ni katika wanafunzi wakubwa wa Maalik.

[1] 42:11

[2] 75:22-23

[3] 54:55

[4] al-Bukhaariy (4581) na Muslim (183).

[5] al-Bukhaariy (4848) na Muslim (2848).

[6] al-Bukhaariy (3797), Muslim (2054), at-Tirmidhiy (3304), an-Nasaa’iy (11582) na al-Bayhaqiy (4/185) na katika ”al-Asmaa’ was-Swifaat”, uk. 469, kupitia kwa Fudhwayl bin Ghazwaan, kutoka kwa Abu Haazim, kutoka kwa Abu Hurayrah.

  • Mhusika: Imaam Shams-ud-Diyn Muhammad bin Ahmad adh-Dhahabiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Uluww lil-´Aliy al-Ghaffaar, uk. 141-142
  • Imechapishwa: 21/07/2024
  • taaliki: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy