Hii ndio miujiza ya Mitume. Hii ndio tofauti kati ya miujiza na uchawi. Ni dalili ioneshayo ya kwamba uchawi kwa watu ulikuwepo tangu hapo kale wakati wa Fir´awn, kama alivyosema Allaah katika Qur-aan. Kama ambavyo kuna uwezekano vilevile ulikuwepo kabla vilevile. Uchawi ukabaki kwa wana wa israaiyl. Kwa ajili hii katika zama za Sulaymaan (´alayhis-Salaam), naye ni Nabii na mfalme, ni miongoni mwa Manabii na wafalme wa wana wa israaiyl. Allaah alifanya majini na mashaytwaan wakawa wanamtumikia kwa mujibu wa amri yake. Kwa sababu Allaah alimpa ufalme ambao hakumpa kiumbe yeyote yule:

قَالَ رَبِّ اغْفِرْ لِي وَهَبْ لِي مُلْكًا لَّا يَنبَغِي لِأَحَدٍ مِّن بَعْدِي

”Akasema: “Mola wangu! Nisamehe na nitunukie ufalme asiupate mtu yeyote baada yangu.” (Swaad  38:35)

Miongoni mwa hayo ni kwamba Allaah alimsahilishia majini kumtumikia:

وَالشَّيَاطِينَ كُلَّ بَنَّاءٍ وَغَوَّاصٍ وَآخَرِينَ مُقَرَّنِينَ فِي الْأَصْفَادِ

”na [pia Tukamtiishia] mashaytwaan kila ajengaye na mpiga mbizi na wengineo wafungwao minyororoni.” (Swaad 38:37-38)

Wote hawa (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiwatumia na kumfanyia kazi kubwakubwa, kama alivyotaja Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala). Wakati sulaymaan (´alayhis-Salaam) alipokufa ndipo mashaytwaan wakaja na kusema kwamba Sulaymaan asingeliweza kutawala majini isipokuwa kwa kutumia uchawi. Alikuwa akiwatumia majini na mashaytwaan kwa msaada wa uchawi. Namna hii ndivyo walivyomzulia Sulaymaan (´alayhis-Salaam). Allaah akamtakasa Sulaymaan na akasema kuwa uchawi ni kufuru na wala haimstahikii Sulaymaan, ambaye ni Mtume wa Allaah, kufanya kufuru. Allaah akawaraddi mayahudi:

وَاتَّبَعُوا مَا تَتْلُو الشَّيَاطِينُ عَلَىٰ مُلْكِ سُلَيْمَانَ ۖ وَمَا كَفَرَ سُلَيْمَانُ

”Wakafuata yale waliyoyasoma mashaytwaan kuhusu ufalme wa Sulaymaan. Sulaymaan hakukufuru… “

Bi maana hakufanya uchawi. Ameita uchawi kuwa ni kufuru. Akaendelea kusema:

وَلَـٰكِنَّ الشَّيَاطِينَ كَفَرُوا يُعَلِّمُونَ النَّاسَ السِّحْرَ وَمَا أُنزِلَ عَلَى الْمَلَكَيْنِ بِبَابِلَ هَارُوتَ وَمَارُوتَۚ وَمَا يُعَلِّمَانِ مِنْ أَحَدٍ حَتَّىٰ يَقُولَا إِنَّمَا نَحْنُ فِتْنَةٌ فَلَا تَكْفُرْ ۖ فَيَتَعَلَّمُونَ مِنْهُمَا مَا يُفَرِّقُونَ بِهِ بَيْنَ الْمَرْءِ وَزَوْجِهِ ۚ وَمَا هُم بِضَارِّينَ بِهِ مِنْ أَحَدٍ إِلَّا بِإِذْنِ اللَّـهِۚ وَيَتَعَلَّمُونَ مَا يَضُرُّهُمْ وَلَا يَنفَعُهُمْ ۚ وَلَقَدْ عَلِمُوا لَمَنِ اشْتَرَاهُ مَا لَهُ فِي الْآخِرَةِ مِنْ خَلَاقٍ ۚ وَلَبِئْسَ مَا شَرَوْا بِهِ أَنفُسَهُمْ ۚ لَوْ كَانُوا يَعْلَمُونَ وَلَوْ أَنَّهُمْ آمَنُوا وَاتَّقَوْا لَمَثُوبَةٌ مِّنْ عِندِ اللَّـهِ خَيْرٌ ۖ لَّوْ كَانُوا يَعْلَمُونَ

”… lakini mashaytwaan ndio waliokufuru; wanafundisha watu uchawi na yaliyoteremshwa kwa Malaika wawili [katika mji wa] Baabil Haaruut na Maaruut. Na [hao Malaika wawili] hawamfundishi yeyote mpaka wamwambie kwanza: “Hakika sisi ni mtihani, hivyo basi usikufuru [kwa kufanya uchawi].” Basi wakajifunza kutoka kwa hao [Malaika] wawili yenye kupelekea kutenganishaa kwayo baina ya mtu na mkewe – na wao si wenye uwezo wa kumdhuru yeyote kwayo isipokuwa kwa idhini ya Allaah – na wanajifunza yanayowadhuru na wala hayawanufaishi; na kwa hakika walielewa kwamba atakayenunua [huo uchawi] hatopata katika Aakhirah fungu lolote, na ni ubaya ulioje walichouzia kwayo  nafsi zao lau wangelikuwa wanaelewa. Lau wangeliamini na wakamcha Allaah, basi malipo kutoka kwa Allaah yangekuwa ni kheri lau wangekuwa wanajua.” (al-Baqarah 02:102-103)

Katika Aayah hizi kuna ubainisho ya kwamba uchawi ni katika matendo ya mashaytwaan na kwamba hailingani kwa Sulaymaan (´alayhis-Salaam), ambaye ni Mtume wa Allaah  na ni mtoto wa Mtume wa Allaah, kufanya uchawi. Lakini huu ni uzushi wa mayahudi ambao wamenong´onezwa kwao na mashaytwaan.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Nawaaqidh-il-Islaam, uk. 147-148
  • Imechapishwa: 30/01/2019