11. Allaah alimtuma Muhammad ili aifanye upya dini ya Ibraahiym (´alayhis-Salaam)

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Allaah (Ta´ala) akawatumia Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) awafanyie upya dini yao, ambayo ndio dini ya baba yao Ibraahiym (´alayhis-Salaam), na kuwaambia ya kwamba kujikurubisha huku na I´tiqaad hii ni haki ya Allaah peke Yake, kwamba si jambo la sawa kufanyiwa chochote katika hayo [´ibaadah] mwengine yeyote, si kwa Malaika aliyekaribu, wala Mtume aliyetumwa, tusiseme wasiokuwa hao.

Vinginevyo, watu hawa washirikina walikuwa wanashuhudia ya kwamba Allaah ndiye Muumbaji pekee asiyekuwa na mshirika, na kwamba hakuna anayeruzuku isipokuwa Yeye, na hakuna anayehuisha wala kufisha isipokuwa Yeye, na wala hakuna anayeendesha mambo isipokuwa Yeye na kwamba mbingu zote saba na vilivyomo ndani yake, na ardhi saba na vilivyomo ndani yake, vyote hivyo [walikuwa wanaamini kuwa] ni viumbe Vyake na viko chini ya uendeshaji na Uwezo Wake (Allaah).

MAELEZO

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema kuwa watu hawa walikuwa katika hali hii ya kikafiri ambayo ni kuabudia masanamu, ambayo kwa madai yao, yanawakurubisha kwa Allaah (Ta´ala). Walikuwa katika hali hii mpaka Allaah alipomtuma Mtume Wake na Nabii Wake wa mwisho Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Allaah (Ta´ala) alimtuma kwa Tawhiyd safi na takasifu. Akawaita watu kumuabudu Allaah peke Yake na wakati huohuo kuwatahadharisha na shirki. Allaah (Ta´ala) amesema:

إِنَّهُ مَن يُشْرِكْ بِاللَّـهِ فَقَدْ حَرَّمَ اللَّـهُ عَلَيْهِ الْجَنَّةَ وَمَأْوَاهُ النَّارُ ۖوَمَا لِلظَّالِمِينَ مِنْ أَنصَارٍ

“Hakika mwenye kumshirikisha Allaah bila shaka Allaah atamharamishia  Pepo na makazi yake yatakuwa ni Motoni – na madhalimu hawatopata yeyote mwenye kuwanusuru.” (05:72)

Amewabainishia kuwa ´ibaadah ni haki ya Allaah pekee. Kadhalika amewabainishia kuwa haijuzu kutekeleza aina yoyote ile ya ´ibaadah kumfanyia asiyekuwa Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala), pasi na kujali huyo mwabudiwa kama ni Malaika aliyekaribu wala Mtume aliyetumwa, seuze wasiokuwa hao. Amesema (Ta´ala):

أَلَمْ أَعْهَدْ إِلَيْكُمْ يَا بَنِي آدَمَ أَن لَّا تَعْبُدُوا الشَّيْطَانَ ۖ إِنَّهُ لَكُمْ عَدُوٌّ مُّبِينٌ وَأَنِ اعْبُدُونِي ۚ هَـٰذَا صِرَاطٌ مُّسْتَقِيمٌ

“Je, Sijakukuahidini enyi wana wa Aadam kwamba: “Msimwabudu shaytwaan, hakika yeye kwenu ni adui wa wazi na kwamba niabuduni Mimi pekee – hii ndio njia iliyonyooka.”” (36:60-61)

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“Awafanyie upya dini yao… ”

Kana kwamba anaashiria maneno Yake (Ta´ala):

ثُمَّ أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ أَنِ اتَّبِعْ مِلَّةَ إِبْرَاهِيمَ حَنِيفًا ۖ وَمَا كَانَ مِنَ الْمُشْرِكِينَ

“Kisha Tukakufunulia Wahy kwamba fuata dini ya Ibraahiym, aliyejiengua kutokana na shirki na kuielekea Tawhiyd, na hakuwa miongoni mwa washirikina.” (16:123)

´Ibaadah ni haki ya Allaah pekee.

Maneno yake mtunzi (Rahimahu Allaah):

“Vinginevyo, watu hawa washirikina walikuwa wanashuhudia ya kwamba Allaah ndiye Muumbaji pekee… “

Anasema (Rahimahu Allaah) ya kwamba washirikina hawa ambao Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alitumwa kwao, walikuwa wakikiri ya kwamba Allaah peke Yake ndiye Muumbaji na kwamba Yeye ndiye ambaye ameumba mbingu na ardhi. Walikuwa wakitambua kuwa Yeye ndiye Mwenye kuyaendesha mambo. Haya Allaah ameyataja kuhusu wao katika Aayah nyingi katika Qur-aan Tukufu. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَلَئِن سَأَلْتَهُم مَّنْ خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ لَيَقُولُنَّ خَلَقَهُنَّ الْعَزِيزُ الْعَلِيمُ

“Na ukiwauliza: “Ni nani yule aliyeumba mbingu na ardhi?” Bila shaka watasema: “Ameziumba Mwenye nguvu Aliyeshinda, Mjuzi wa yote.”” (43:09)

وَلَئِن سَأَلْتَهُم مَّنْ خَلَقَهُمْ لَيَقُولُنَّ اللَّـهُ

“Na ukiwauliza: “Ni nani kawaumba?” Bila shaka watasema: “Allaah.” (43:87)

Aayah zenye maana kama hii ni nyingi.

Lakini kukiri huku hakuwanufaishi kitu, kwa sababu kukubali uola peke yake hakunufaishi kitu kama mtu hakubali uungu na akamuabudu Allaah pekee. Kukubali uola wa Allaah kunapelekea vilevile kukubali kuabudiwa kwa Allaah pekee na kwamba kukubali kuabudiwa kwa Allaah pekee ndani yake kuna kukubali pia uola wa Allaah.

Ama sampuli ya kwanza, ni dalili yenye kulazimisha. Kwa maana nyingine kukiri huku ni dalili yenye kulazimisha kwa yule anayekiri kuabudiwa kwa Allaah pekee. Ikiwa Allaah peke Yake ndiye Muumbaji, Mwenye kuyaendesha mambo na ndiye Ambaye mikononi Mwake mna uwezo wa kila kitu, basi ni wajibu ´ibaadah afanyiwe Yeye pekee na si mwengine.

Ama sampuli ya pili, ndani yake kunaingia ile aina ya kwanza. Kwa msemo mwingine ni kwamba Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah ndani yake mnaingia Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah kwa sababu mtu anamuabudu Mola (´Azza wa Jall) ambaye mtu anaamini kuwa Yeye pekee ndiye Muumbaji (Subhaanahu wa Ta´ala) na ndiye Mwenye kuyaendesha mambo yote.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Utaymiyn
  • Mfasiri: Fitqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 21-23
  • Imechapishwa: 23/04/2022