Abu Ja´far at-Twahaawiy (Rahimahu Allaah) amesema:
12 – Mwenye kufisha bila ya khofu yoyote, Mwenye kufufua bila ya uzito wowote.
13 – Ni Mwenye kusifika milele juu ya sifa Zake kabla ya kuumba Kwake.
14 – Sifa Zake hazikuongezeka kutokana nao.
15 – Kama ambavyo siku zote alikuwa ni mwenye kusifiwa kwa sifa Zake, vivyo hivyo ndivo atavoendelea kuwa milele.
16 – Hakuwa ni Muumbaji baada ya kuumba wala Mwanzilishi viumbe baada ya kuanzisha viumbe.
17 – Alikuwa na sifa ya uungu wakati hapakuwa yeyote wa kuabudu, alikuwa ni Muumbaji wakati hapakuwa kiumbe yeyote.
18 – Kama ambavyo anazingatiwa ni Mwenye kuwahuisha wafu na amestahiki jina hili kabla ya kuwapa uhai, kadhalika amestahiki jina la Muumbaji kabla ya kuwaumba.
19 – Kwa sababu Yeye juu ya kila jambo ni muweza. Kila kitu ni chenye kumuhitajia Yeye. Kila jambo Kwake ni jepesi:
لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖوَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ
“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”[1]
MAELEZO
Baadhi wanasema kuwa Allaah ni muweza kwa yale anayoyataka. Hayo si sahihi. Sahihi ni yale yaliyotajwa katika Qur-aan na Sunnah; kwamba Yeye juu ya kila kitu ni muweza kwa sababu matakwa na uwezo Wake ni vyenye kuenea.
Mu´tazilah wanasema kuwa Allaah (Ta´ala) hakutaka mja aingie ndani ya madhambi; bali mja mwenyewe ndiye kataka hivo, na si Allaah. Kwa ajili hiyo amesema mmoja katika wapotofu wao:
Amedai mjinga na yule mwenye kuonelea kama yeye
ya kwamba Muumba ndiye kahukumu maasi
ikiwa hayo anayoyasema ni kweli
ni kwa nini basi aadhibiwe mzinzi na mwizi akatwe mkono?
Abul-Khattwaab (Rahimahu Allaah) amesema pindi alipokuwa akibainisha haki na usawa:
Wamesema: “Vipi basi matendo ya waja?”
Nikasema hakuna Muumba isipokuwa Mungu mtukufu
Wakasema: “Je, anataka kutokee kwa mambo mabaya?”
Nikasema matakwa yote yanayotokana na Mola
Ni upungufu ikiwa yatatokea pasi na kutaka Kwake
Ametakasika kushindwa na kitu duni
Matakwa anayozungumzia Abul-Khattwaab ni ya kilimwengu, na si ya kidini. Hayo yatakuja kubainishwa huko mbele.”[2]
[1] 42:11
[2] Haashiyah ´alaa al-´Aqiydah at-Twahaawiyyah, uk. 23-24
- Muhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
- Tarjama: Firqatunnajia.com
- Marejeo: al-´Aqiydah at-Twahaawiyyah – Sharh wa Ta´liyq, uk. 14-15
- Imechapishwa: 12/09/2024
Mshirikishe mwenzako:
- Click to share on Telegram (Opens in new window)
- Click to share on WhatsApp (Opens in new window)
- Click to print (Opens in new window)
- Click to email a link to a friend (Opens in new window)
- Click to share on Facebook (Opens in new window)
- Click to share on Twitter (Opens in new window)
- Click to share on Pocket (Opens in new window)