05. Je, inafaa kutamba kwa maji ya zamzam?

Swali 05: Je, inafaa kutamba kwa maji ya zamzam[1]?

Jibu: Hadiyth ambazo ni Swahiyh zimefahamisha kuwa maji ya zamzam ni matukufu na yaliyobarikiwa. Katika “as-Swahiyh” ya Muslim imethibiti ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema kuhusu zamzam:

“Ni yenye kubarikiwa. Ni chakula chenye kushibisha.”[2]

Amezidisha katika upokezi mwingine uliopokea Abu Daawuud kwa cheni nzuri:

“Ni yenye kubarikiwa. Ni chakula chenye kushibisha na ponyo ya maradhi.”

Hadiyth hii Swahiyh inajulisha juu ya ubora wa maji ya zamzam na kuwa ni chakula chenye kushibisha, ponyo ya maradhi na kwamba yamebarikiwa.

Sunnah ni kuyanywa kama alivoyanywa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Inafaa kuyatawadha na kujitamba nayo. Vivyo hivyo inafaa kuoga nayo josho la janaba haja ikipelekea kufanya hivo.

Imethibiti kutoka kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba maji yaliota kutoka kati ya vidole vyake kisha watu wakachukua mahitaji yao kutoka katika maji hayo ili wanywe, watawadhe, kufua nguo zao na wajitambe. Yote haya yalitokea.

Maji ya zamzam hayawezi kuwa yanatofautiana na maji yaliyoota kati ya vidole vya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).  Yote ni maji matukufu. Ikiwa imefaa kutawadha, kuoga, kutamba na kuosha nguo kwa maji yaliyoota kati ya vidole vyake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), basi vivyo hivyo itafaa kufanya hayo kwa maji ya zamzam.

Kwa hali yoyote ni maji masafi, mazuri na ambayo inapendeza kuyanywa. Hapana vibaya kuyatawadha, kuyafulia nguo, kutamba ikiwa haja imepelekea kufanya hivo na mengineyo kama tulivotangulia kutaja. Inasemekana kuwa imepokelewa kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuwa amesema:

“Maji ya zamzam ni kwa kile alichonuia mtu.”[3]

Kuna unyonge katika cheni ya wapokezi wake. Lakini inatiwa nguvu na Hadiyth nyenginezo Swahiyh zilizotangulia na himdi zote njema anastahiki Allaah.

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (10/27-28).

[2] Muslim (6309).

[3] Ibn Maajah (3062).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Musaafir, uk. 15-17
  • Imechapishwa: 21/02/2022