Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“Jua, Allaah akurehemu… ”

Kuwa na utambuzi wa kitu kama jinsi kilivyo kikweli. Utambuzi huu una daraja sita:

Ya kwanza: Ujuzi, wa kukitambua kitu kama jinsi kilivyo kikweli kwa njia ya kihakika.

Ya pili: Ujinga mwepesi, wa kutokuwa na utambuzi kabisa.

Ya tatu: Ujinga uliopandiana, nao ni kule kukitambua kitu kwa njia inayoenda kinyume na uhakika wake.

Umeitwa ujinga uliopandiana kwa sababu ni ujinga aina mbili; mtu kutojua ukweli wa mambo na pia mtu kutoijua hali yake kwa sababu anafikiri kuwa ni mtambuzi ilihali ukweli wa mambo hayuko hivo.

Ya nne: Ufikiriaji, ambao ni wa kukitambua kitu wakati kinyume chake pengine ndio ikawa sahihi zaidi.

Ya tano: Mashaka, ambayo ni kule kukitambua kitu pamoja na uwezekano wa kuwepo kitu kingine kinachoweza kuwa kama kile.

Ya sita: Dhana, ambayo ni kule kukitambua kitu na wakati huohuo kuna uwezekano kikawa ni sahihi zaidi kuliko kile kinachoenda kinyume.

Ujuzi umegawanyika sehemu mbili; ya kidharurah na kinadhari.

Kuhusu ujuzi wa kilazima, ni ule ambao unahusiana na kuyatambua mambo kilazima kwa njia ya kwamba mtu hahitajii kufanya utafiti wala dalili. Mfano wa hilo ni mtu kujua kuwa moto unachoma.

Kuhusiana na ujuzi wa aina ya kinadhari, ni ule ambao unahitajia nadhariya na dalili. Mfano wa ujuzi huu ni kama mtu kujua kwamba ni wajibu kutia nia wakati wa kutawadha.

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“Allaah akurehemu.”

Allaah akumiminie rehema Zake ambazo unafikia malengo yako na kukuokoa na yawezayo kukudhuru. Maana ya hilo ni Allaah akusamehe yaliyopita katika madhambi yako na akuwafikishe na kukuhifadhi na yaliyo huko mbele. Maana hii ni pale endapo rehema inapotajwa peke yake. Lakini pale ambapo inapoambatanishwa pamoja na msamaha, msamaha unakuwa kwa yale madhambi yaliyopita, wakati rehema ni kule kuwafikishwa katika kheri na kusalimika na madhambi siku za mbele.

Kitendo cha mtunzi (Rahimahu Allaah) kinafahamisha namna anavyomjali na kumuonea huruma yule anayemzungumzisha.

Tawhiyd maana yake kilugha ni kukifanya kitu kuwa kimoja. Hili halihakikishwi isipokuwa kwa kupatikana ukanushaji na uthibitishaji vyote viwili kwa pamoja. Kukanusha peke yake hakutoshelezi, kwa sababu maana yake ni kitu kisichokuwepo. Kwa upande mwingine kuthibitisha peke yake hakutoshelezi, kwa sababu kuthibitisha peke yake hakukanushi ushirikiano.

Mfano wa hilo ni kuwa upwekeshaji wa mtu hautimii isipokuwa mpaka ashuhudie ya kwamba hakuna mungu wa haki isipokuwa Allaah. Katika hali hii akanushe kuabudiwa kwa asiyekuwa Allaah na wakati huohuo amthibitishie nao Allaah pekee.

Maana ya kiistilahi ya Tawhiyd mtunzi (Rahimahu Allaah) ameitambulisha kwa njia ifuatayo:

“Tawhiyd ni kumpwekesha Allaah (´Azza wa Jall) kwa ´ibaadah.”

Bi maana kumwabudu Allaah pekee na usimshirikishe na chochote. Bali umpwekeshe pekee kwa ´ibaadah hali ya kumpenda, kumuadhimisha, matarajio na khofu.

Makusudio ya Shaykh (Rahimahu Allaah) ni ile aina ya Tawhiyd ambayo Mitume walitumwa ili kuja kuihakikisha. Sampuli hii ndio ambayo ilikuwa sababu ya kutoke migogoro na tofauti kati ya Mitume na nyumati zao.

Vilevile kuna utambulisho wa Tawhiyd wenye kuenea, nao ni:

“Kumpwekesha Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) katika yale ambayo ni maalum Kwake.”

Kuna aina tatu za Tawhiyd:

1 – Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah. Hii maana yake ni kumpwekesha Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) kwa uumbaji, umiliki na uendeshaji wa mambo. Allaah (´Azza wa Jall) amesema:

اللَّـهُ خَالِقُ كُلِّ شَيْءٍ

“Allaah ndiye Muumbaji wa kila kitu.” (39:62)

هَلْ مِنْ خَالِقٍ غَيْرُ اللَّـهِ يَرْزُقُكُم مِّنَ السَّمَاءِ وَالْأَرْضِ ۚ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ

“Je, kuna muumbaji yeyote badala ya Allaah anayekuruzukuni kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Hakuna mungu wa haki isipokuwa Yeye.” (35:03)

تَبَارَكَ الَّذِي بِيَدِهِ الْمُلْكُ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ

“Amebarikika Ambaye mkononi Mwake umo ufalme, Naye juu ya kila kitu ni Muweza.” (67:01)

أَلَا لَهُ الْخَلْقُ وَالْأَمْرُ ۗ تَبَارَكَ اللَّـهُ رَبُّ الْعَالَمِينَ

“Tanabahi! Ni Vyake pekee uumbaji na amri. Amebarikika Allaah, Mola wa walimwengu.” (07:54)

2 – Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah. Kumpwekesha Allaah (Ta´ala) kwa kumuabudu kwa njia ya kwamba mtu asichukue mwengine yeyote pamoja na Allaah akawa anamuabudu au kujikurubisha kwake kama anavyomuabudu na kujikurubisha kwa Allaah.

3 – Tawhiyd-ul-Asmaa´ was-Swifaat. Hii ina maana ya kumpwekesha Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) kwa majina na sifa Zake zilizothibiti katika Kitabu Chake na Sunnah za Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hilo linapitika kwa kuthibitisha yale Aliyojithibitishia na kukanusha yale aliyojikanushia pasi na upotoshaji, ukanushaji, kuzifanyia namna wala kuzilinganisha.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Utaymiyn
  • Mfasiri: Fitqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 14-15
  • Imechapishwa: 23/04/2022