03. ´Aqiydah sahihi juu ya Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah

Miongoni mwa ´Aqiydah ya Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah ni pamoja na mtu kumpwekesha Allaah (Ta´ala) katika ´ibaadah. Hawaabudu mungu mwengine pamoja na Allaah. Badala yake wanamtekelezea Allaah pekee aina zote za ´ibaadah za wajibu na zilizopendekezwa.

Hawamsujudii yeyote isipokuwa Allaah. Hawamfanyii Twawaaf yeyote isipokuwa Allaah. Hawachinji kwa ajili ya yeyote isipokuwa Allaah. Hawamuwekei nadhiri isipokuwa Allaah. Hawaapi kwa yeyote isipokuwa kwa Allaah. Hawategemei isipokuwa kwa Allaah. Hawamuombi yeyote isipokuwa Allaah. Hii ndio Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah:

وَاعْبُدُوا اللَّـهَ وَلَا تُشْرِكُوا بِهِ شَيْئًا

“Na mwabuduni Allaah na wala msimshirikishe na chochote.” (04:36)

وَقَضَىٰ رَبُّكَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ

“Na Mola wako amehukumu kwamba msiabudu yeyote isipokuwa Yeye.” (17:23)

وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا إِلَـٰهًا وَاحِدًا

“Hawakuamrishwa jengine isipokuwa kumwabudu Mungu mmoja.” (09:31)

وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّـهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ

“Na hawakuamrishwa jengine isipokuwa wamwabudu Allaah hali ya kuwa ni wenye kumtakasia Yeye dini.” (98:05)

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ

“Na Sikuumba majini na watu isipokuwa waniabudu.” (51:56)

Waniabudu maana yake ni “wanipwekeshe mimi tu”.

Kinyume chake ni shirki – Allaah atukinge nayo. Shirki ndio dhambi kubwa ambayo Allaah ameasiwa kwayo. Amesema (Ta´ala):

إِنَّ اللَّـهَ لَا يَغْفِرُ أَن يُشْرَكَ بِهِ وَيَغْفِرُ مَا دُونَ ذَٰلِكَ لِمَن يَشَاءُ ۚ وَمَن يُشْرِكْ بِاللَّـهِ فَقَدِ افْتَرَىٰ إِثْمًا عَظِيمًا

“Hakika Allaah hasamehi kushirikishwa, lakini anasamehe yaliyo chini ya hayo kwa Amtakae. Na yeyote atakayemshirikisha Allaah basi kwa hakika amebuni dhambi kuu.” (04:48)

إِنَّ اللَّـهَ لَا يَغْفِرُ أَن يُشْرَكَ بِهِ وَيَغْفِرُ مَا دُونَ ذَٰلِكَ لِمَن يَشَاءُ ۚ وَمَن يُشْرِكْ بِاللَّـهِ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا بَعِيدًا

“Hakika Allaah hasamehi kushirikishwa, lakini anasamehe yaliyo chini ya hayo kwa Amtakae. Na yeyote atakayemshirikisha Allaah basi kwa hakika amepotoka upotofu wa mbali.” (04:116)

حُنَفَاءَ لِلَّـهِ غَيْرَ مُشْرِكِينَ بِهِ ۚ وَمَن يُشْرِكْ بِاللَّـهِ فَكَأَنَّمَا خَرَّ مِنَ السَّمَاءِ فَتَخْطَفُهُ الطَّيْرُ أَوْ تَهْوِي بِهِ الرِّيحُ فِي مَكَانٍ سَحِيقٍ

“Muelemee haki kwa Allaah pasi na kumshirikish; na yeyote anayemshirikisha Allaah basi ni kana kwamba ameporomoka kutoka mbinguni, wakamnyakua ndege au upepo ukamtupa mahali mbali mno.” (22:31)

وَإِذْ قَالَ لُقْمَانُ لِابْنِهِ وَهُوَ يَعِظُهُ يَا بُنَيَّ لَا تُشْرِكْ بِاللَّـهِ ۖ إِنَّ الشِّرْكَ لَظُلْمٌ عَظِيمٌ

“Na Luqmaan alipomwambia mwanawe huku akimuwaidhi: “Ee mwanangu! Usimshirikishe Allaah, kwani hakika shirki ni dhuluma kuu!”” (31:13)

Amebainisha (Ta´ala) ya kwamba shirki inabatilisha matendo yote na inamtoa mtu katika Uislamu. Amesema (Ta´ala):

وَلَوْ أَشْرَكُوا لَحَبِطَ عَنْهُم مَّا كَانُوا يَعْمَلُونَ

“Na kama wangemshirikisha bila shaka yangebatilika yale waliyokuwa wakitenda.” (06:88)

وَلَقَدْ أُوحِيَ إِلَيْكَ وَإِلَى الَّذِينَ مِن قَبْلِكَ لَئِنْ أَشْرَكْتَ لَيَحْبَطَنَّ عَمَلُكَ وَلَتَكُونَنَّ مِنَ الْخَاسِرِينَ

“Kwa hakika umefunuliwa Wahy na kwa wale walio kabla yako: “Ukifanya shirki bila shaka yatabatilika matendo yako na bila shaka utakuwa miongoni mwa waliokhasirika.”” (39:65)

Katika “as-Swahiyh” ya Muslim kutoka kwa Jaabir bin ´Abdillaah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kukutana na Allaah pasi na kumshirikisha Yeye na chochote, basi ataingia Peponi, na mwenye kukutana Naye ilihali anamshirikisha Yeye na chochote, basi ataingia Motoni.”

Katika “as-Swahiyh” ya al-Bukhaariy kutoka kwa Ibn Mas´uud (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kufa ilihali ni mwenye kuomba mwenza pamoja na Allaah, basi ataingia Motoni.”

Yule mwenye kufanya aina yoyote ile ya ´ibaadah akamfanyia asiyekuwa Allaah, basi huyo ni mshirikina kafiri.

Kwa mfano du´aa ni moja miongoni mwa ´ibaadah ambazo Allaah ameamrisha. Hivyo basi, yule mwenye kumuomba Allaah peke yake, huyo ni mpwekeshaji. Upande mwingine, yule mwenye kumuomba asiyekuwa Allaah, ameshirikisha. Amesema (Ta´ala):

وَلَا تَدْعُ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُكَ وَلَا يَضُرُّكَ ۖ فَإِن فَعَلْتَ فَإِنَّكَ إِذًا مِّنَ الظَّالِمِينَ

“Wala usiombe badala ya Allaah asiyekufaa na wala asiyekudhuru. Endapo utafanya hivo, basi hakika utakuwa miongoni mwa madhalimu.” (10:106)

وَمَن يَدْعُ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ لَا بُرْهَانَ لَهُ بِهِ فَإِنَّمَا حِسَابُهُ عِندَ رَبِّهِ ۚ إِنَّهُ لَا يُفْلِحُ الْكَافِرُونَ

“Na yeyote yule anayeomba pamoja na Allaah mungu mwengine – hana ushahidi wa wazi wa hilo – basi hakika hesabu yake iko kwa Mola wake. Hakika hawafaulu makafiri.” (23:117)

وَأَنَّ الْمَسَاجِدَ لِلَّـهِ فَلَا تَدْعُوا مَعَ اللَّـهِ أَحَدًا وَأَنَّهُ لَمَّا قَامَ عَبْدُ اللَّـهِ يَدْعُوهُ كَادُوا يَكُونُونَ عَلَيْهِ لِبَدًا قُلْ إِنَّمَا أَدْعُو رَبِّي وَلَا أُشْرِكُ بِهِ أَحَدً

“Na kwamba mahala pote pa kuswalia ni kwa ajili ya Allaah pekee, basi msiombe yeyote pamoja na Allaah. Na kwamba mja wa Allaah aliposimama kumwomba, walikaribia kumzonga. Sema: “Hakika mimi namuomba Mola wangu pekee na wala simshirikishi na yeyote.”” (72:18-20)

لَهُ دَعْوَةُ الْحَقِّ ۖ وَالَّذِينَ يَدْعُونَ مِن دُونِهِ لَا يَسْتَجِيبُونَ لَهُم بِشَيْءٍ إِلَّا كَبَاسِطِ كَفَّيْهِ إِلَى الْمَاءِ لِيَبْلُغَ فَاهُ وَمَا هُوَ بِبَالِغِهِ ۚ وَمَا دُعَاءُ الْكَافِرِينَ إِلَّا فِي ضَلَالٍ

“Kwake ndiko kuna maombi yote ya haki. Na wale wenye kuomba badala Yake hawawaitikii kwa chochote isipokuwa kama anayenyosha viganja vyake viwili vya mikono kwenye maji ili yafikie kinywani mwake, wala hayafikii – na du’aa za makafiri hazipo isipokuwa katika upotevu.” (13:14)

وَالَّذِينَ يَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ لَا يَخْلُقُونَ شَيْئًا وَهُمْ يُخْلَقُونَ أَمْوَاتٌ غَيْرُ أَحْيَاءٍ ۖ وَمَا يَشْعُرُونَ أَيَّانَ يُبْعَثُونَ

“Na wale wanaowaomba badala ya Allaah hawaumbi kitu chochote – bali wao wanaumbwa. Ni wafu si wahai na hawatambui lini watafufuliwa.” (16:20-21)

فَلَا تَدْعُ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ فَتَكُونَ مِنَ الْمُعَذَّبِينَ

“Basi usiombe pamoja na Allaah mungu mwengine; ukaja kuwa miongoni mwa watakaoadhibiwa.” (26:213)

يُولِجُ اللَّيْلَ فِي النَّهَارِ وَيُولِجُ النَّهَارَ فِي اللَّيْلِ وَسَخَّرَ الشَّمْسَ وَالْقَمَرَ كُلٌّ يَجْرِي لِأَجَلٍ مُّسَمًّى ۚ ذَٰلِكُمُ اللَّـهُ رَبُّكُمْ لَهُ الْمُلْكُ ۚ وَالَّذِينَ تَدْعُونَ مِن دُونِهِ مَا يَمْلِكُونَ مِن قِطْمِيرٍ إِن تَدْعُوهُمْ لَا يَسْمَعُوا دُعَاءَكُمْ وَلَوْ سَمِعُوا مَا اسْتَجَابُوا لَكُمْ ۖ وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ يَكْفُرُونَ بِشِرْكِكُمْ ۚ وَلَا يُنَبِّئُكَ مِثْلُ خَبِيرٍ

“Anauingiza usiku ndani ya mchana na anauingiza mchana ndani ya usiku na anaitisha jua na mwezi; kila kimoja kinakwenda hadi muda maalum uliokadiriwa. Huyo ndiye Allaah, Mola wenu, ufalme ni Wake pekee.  Wale mnaowaomba badala Yake hawamiliki hata kijiwavu cha kokwa ya tende. Mkiwaomba, hawasikii maombi yenu, na hata wakisikia, hawatakuitikieni na siku ya Qiyaamah watakanusha ushirikina wenu na wala hakuna atakayekujulisha vyyema kama Mwenye khabari zote.” (35:13-14)

وَلَئِن سَأَلْتَهُم مَّنْ خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ لَيَقُولُنَّ اللَّـهُ ۚ قُلْ أَفَرَأَيْتُم مَّا تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ إِنْ أَرَادَنِيَ اللَّـهُ بِضُرٍّ هَلْ هُنَّ كَاشِفَاتُ ضُرِّهِ أَوْ أَرَادَنِي بِرَحْمَةٍ هَلْ هُنَّ مُمْسِكَاتُ رَحْمَتِهِ ۚقُلْ حَسْبِيَ اللَّـهُ ۖ عَلَيْهِ يَتَوَكَّلُ الْمُتَوَكِّلُونَ

“Na ukiwauliza: “Ni nani aliyeumba mbingu na ardhi?” Bila shaka watasema: “Allaah.” Sema: “Je, mnaonaje wale mnaowaomba badala ya Allaah ikiwa Allaah atanikusudia dhara, je, wao wataweza kuondosha dhara Yake? Au akinikusudia  rehema, je, wao wataweza kuizuia rehema Zake?” Sema: “Ananitosheleza Allaah. Kwake wanategemea wenye kutegemea.” (39:38)

قُلْ أَرَأَيْتُم مَّا تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ أَرُونِي مَاذَا خَلَقُوا مِنَ الْأَرْضِ أَمْ لَهُمْ شِرْكٌ فِي السَّمَاوَاتِ ۖ ائْتُونِي بِكِتَابٍ مِّن قَبْلِ هَـٰذَا أَوْ أَثَارَةٍ مِّنْ عِلْمٍ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ وَمَنْ أَضَلُّ مِمَّن يَدْعُو مِن دُونِ اللَّـهِ مَن لَّا يَسْتَجِيبُ لَهُ إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ وَهُمْ عَن دُعَائِهِمْ غَافِلُونَ وَإِذَا حُشِرَ النَّاسُ كَانُوا لَهُمْ أَعْدَاءً وَكَانُوا بِعِبَادَتِهِمْ كَافِرِينَ

“Sema: “Je, mnaonaje wale mnaowaomba badala ya Allaah! Nionyesheni nini wameumba katika ardhi au wana ushirika katika mbingu? Nileteeni Kitabu kabla ya hiki au alama yeyote iliobakia ya elimu mkiwa wakweli!” Na nani aliyepotoka zaidi kuliko ambaye anayeomba asiyekuwa Allaah ambaye hamuitikii mpaka siku ya Qiyaamah nao kuhusu du’aa zao ni wenye kughafilika? Na [siku ya Qiyaamah] watakapokusanywa watu [miungu ya uongo] watakuwa maadui wao na watakuwa kwa ‘ibaadah zao ni wenye kuzikanusha.” (46:04-06)

Imethibiti katika “as-Sunan” kutoka kwa an-Nu´maan bin Bashiyr (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye ameeleza kwamba amemsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akisema:

“Du´aa ndio ´ibaadah.”

Tawhiyd hii – Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah – ndio ambayo kulitokea magomvi kati ya Mitume na watu wao. Tawhiyd hii ndio sababu ya Allaah kuwatuma Mitume kwa ajili ya kuibainisha na kulingania kwayo. Hali kadhalika akateremsha Vitabu kwa ajili ya kuithibitisha, kuiweka wazi na kutumia hoja kwayo. Amesema (Ta´ala):

وَلَقَدْ بَعَثْنَا فِي كُلِّ أُمَّةٍ رَّسُولًا أَنِ اعْبُدُوا اللَّـهَ وَاجْتَنِبُوا الطَّاغُوتَ

“Na kwa hakika Tulituma katika kila ummah Mtume [awaamrishe watu wake] kwamba: “Mwabuduni Allaah na jiepusheni na Twaaghuut.” (16:36)

وَمَا أَرْسَلْنَا مِن قَبْلِكَ مِن رَّسُولٍ إِلَّا نُوحِي إِلَيْهِ أَنَّهُ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا أَنَا فَاعْبُدُونِ

“Na Hatukutuma kabla yako Mtume yeyote isipokuwa Tulimfunulia Wahy ya kwamba: “Hakika hapana mungu wa haki isipokuwa Mimi – hivyo basi niabuduni!” (21:25)

يُنَزِّلُ الْمَلَائِكَةَ بِالرُّوحِ مِنْ أَمْرِهِ عَلَىٰ مَن يَشَاءُ مِنْ عِبَادِهِ أَنْ أَنذِرُوا أَنَّهُ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا أَنَا فَاتَّقُونِ

“Anateremsha Malaika na Roho kwa amri Yake juu ya amtakaye miongoni mwa waja Wake kwamba: “Onyeni: “Hakika hapana mungu wa haki isipokuwa Mimi; basi nicheni!” (16:02)

Hii ndio ambayo Mitume walikuwa wakianza kuwaamrisha watu wao pindi walipokuwa wakiwalingania katika dini ya Allaah. Kila Mtume alikuwa akiwaamrisha watu wake:

يَا قَوْمِ اعْبُدُوا اللَّـهَ مَا لَكُم مِّنْ إِلَـٰهٍ غَيْرُهُ

“Enyi watu wangu! Mwabuduni Allaah, hakika hamna mungu mwengine wa haki asiyekuwa Yeye.” (07:59,65,73,85)

Nuuh alisema hivyo na hali kadhalika Huud, Swaalih, Shu´ayb na Mitume wengine wote – swalah na salamu ziwashukie wote.

Amesema (Ta´ala):

وَإِبْرَاهِيمَ إِذْ قَالَ لِقَوْمِهِ اعْبُدُوا اللَّـهَ وَاتَّقُوهُ ۖ ذَٰلِكُمْ خَيْرٌ لَّكُمْ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ إِنَّمَا تَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ أَوْثَانًا وَتَخْلُقُونَ إِفْكًا ۚ إِنَّ الَّذِينَ تَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ لَا يَمْلِكُونَ لَكُمْ رِزْقًا فَابْتَغُوا عِندَ اللَّـهِ الرِّزْقَ وَاعْبُدُوهُ وَاشْكُرُوا لَهُ ۖ إِلَيْهِ تُرْجَعُونَ

“Ibraahiym alipowaambia watu wake: “Mwabuduni Allaah na mcheni! Hivyo ni kheri kwenu mkiwa mnajua. Hakika si vyenginevyo vile mnaabudu badala ya Allaah ni masanamu na mnazua uzushi. Hakika wale mnaowaabudu badala ya Allaah hawakumilikiini riziki, basi tafuteni riziki kwa Allaah na mwabuduni Yeye na mshukuruni; Kwake mtarejeshwa.” (29:16-17)

Vilevile amesema (Ta´ala) kuhusu Mtume Wake Yuusuf (´alayhis-Salaam):

يَا صَاحِبَيِ السِّجْنِ أَأَرْبَابٌ مُّتَفَرِّقُونَ خَيْرٌ أَمِ اللَّـهُ الْوَاحِدُ الْقَهَّارُ مَا تَعْبُدُونَ مِن دُونِهِ إِلَّا أَسْمَاءً سَمَّيْتُمُوهَا أَنتُمْ وَآبَاؤُكُم مَّا أَنزَلَ اللَّـهُ بِهَا مِن سُلْطَانٍ ۚ إِنِ الْحُكْمُ إِلَّا لِلَّـهِ ۚ أَمَرَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ ۚ ذَٰلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ

“Enyi masahibu wangu wawili wa jela! Je, waungu wengi wanaofarakana ni bora au Allaah ambaye ni Mmoja pekee, Mwenye nguvu juu kabisa? Hamwabudu badala Yake isipokuwa majina [ya masanamu] mmeyaita nyinyi na baba zenu – hakuyateremshia Allaah kwayo ushahidi wowote. Hakuna hukumu isipokuwa ya Allaah. Ameamrisha kwamba msimwabudu yeyote isipokuwa Yeye pekee – hiyo ndio dini iliyonyooka, lakini watu wengi hawajui.” (12:39-40)

Washirikina hawana mategemezi yoyote kwa ushirikina wao. Hawawezi kupata mategemezi yoyote kutoka katika akili sahihi wala andiko kutoka kwa Mitume. Amesema (Ta´ala):

وَاسْأَلْ مَنْ أَرْسَلْنَا مِن قَبْلِكَ مِن رُّسُلِنَا أَجَعَلْنَا مِن دُونِ الرَّحْمَـٰنِ آلِهَةً يُعْبَدُونَ

“Na waulize wale Tuliowatuma kabla yako miongoni mwa Mitume Wetu, je, tulifanya badala ya Mwingi wa rehema miungu mingine iabudiwe?” (43:45)

Maana yake ni kwamba hakuna Mtume yeyote ambaye alimwita mtu kuabudu chochote pamoja na Allaah. Bali wote, kuanzia wa mwanzo wao hadi wa mwisho wao, walikuwa ni wenye kuita katika kumwabudu Allaah Mmoja wa pekee, hali ya kuwa hana mshirika. Amesema (Ta´ala):

قُلْ أَرَأَيْتُم مَّا تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ أَرُونِي مَاذَا خَلَقُوا مِنَ الْأَرْضِ أَمْ لَهُمْ شِرْكٌ فِي السَّمَاوَاتِ ۖ ائْتُونِي بِكِتَابٍ مِّن قَبْلِ هَـٰذَا أَوْ أَثَارَةٍ مِّنْ عِلْمٍ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ

“Sema: “Je, mnaonaje wale mnaowaomba badala ya Allaah! Nionyesheni nini wameumba katika ardhi au wana ushirika katika mbingu? Nileteeni Kitabu kabla ya hiki au alama yeyote iliobakia ya elimu mkiwa wakweli!” (46:04)

Hii ni dalili ya kiakili ya kukata kabisa inayoonesha kuwa kila ambaye si Allaah basi kumwabudu kwake ni kwa batili. Kwani hakuumba chochote na wala hakuwa ni msaidizi katika kuumba kitu. Allaah pekee ndiye aliyepwekeka kwa hayo. Kwa nini basi waabudiwe? Halafu Allaah akawakanushia washirikina kuwa na dalili ya kinakili kutoka katika vitabu vilivyoteremshwa au Mtume aliyetumilizwa katika ile shirki waliyoenda ndani yake. Kwa hayo imepata kubainika kuwa washirikina hawana hoja yoyote kabisa. Matokeo yake wakawa ni wenye kudumishwa Motoni milele – na ni uovu uliyoje wa sehemu ya kufikia!

Kutokana na yaliyotangulia, inapata kufahamika kuwa Tawhiyd hii ndio wajibu wa mwanzo na jambo muhimu kabisa. Aidha ndio dini pekee ambayo Allaah anaikubali.

  • Mhusika: Shaykh ´Abdus-Salaam bin Barjas
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Mu´taqad as-Swahiyh, uk. 21-29
  • Imechapishwa: 20/06/2020