Imaam Ahmad amepokea katika “al-Musnad” yake kupitia kwa al-Hasan bin ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anhumaa) ambaye amesimulia: ”Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alinifunza maneno nitayoyasema katika Qunuut ya Witr:

اللهم اهدني فيمن هديت, وعافني فيمن عافيت, وتولني فيمن توليت, وبارك لي فيما أعطيت, وقني شر ما قضيت, فإنك تقضي ولا يقضى عليك, وإنه لا يذلّ من واليتَ تباركت ربنا وتعاليت

“Ee Allaah! Niongoze pamoja na wale Uliowaongoza, uniafu pamoja na wale Uliowaafu, Uniangalie pamoja na wale Unaowaangalia, Unibariki katika kile Ulichotoa na Unilinde kutokamana na shari kwa yale Uliyohukumu. Kwani hakika Wewe ndiye mwenye kuhukumu na wala Huhukumiwi. Hakika hatwezeki yule Uliyemlinda. Umebarikika na Umetukuka Mola wetu.”[1]

MAELEZO

Ee Allaah! Niongoze pamoja na wale Uliowaongoza – Nielekeze katika haki na unijaalie kuweza kuifanya kazi. Hilo ni kwa sababu uongofu uliokamilika na wenye manufaa ni ule ambao Allaah anamjaalia mja kukusanya baina ya elimu na matendo mema. Uongofu bila ya matendo haunufaishi kitu, bali ni madhara. Kwa sababu mtu asipoyafanyia kazi yale aliyoyajua basi elimu yake inakuwa ni majuto kwake. Mfano wa mwongozo wa kielimu pasi na matendo ni maneno Yake Allaah (Ta´ala):

وَأَمَّا ثَمُودُ فَهَدَيْنَاهُمْ فَاسْتَحَبُّوا الْعَمَىٰ عَلَى الْهُدَىٰ

“Na ama kina Thamuud, tuliwaongoza, lakini walipendelea upofu kuliko uongofu.”[2]

Kwa maana ya kwamba tuliwabainishia njia na kuwafikishia elimu. Hata hivyo wakapendelea upofu badala ya uongofu.

Vilevile Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) amesema:

وَإِنَّكَ لَتَهْدِي إِلَىٰ صِرَاطٍ مُّسْتَقِيمٍ

”Na hakika wewe bila shaka unaongoza kuelekea njia iliyonyooka.”[3]

Kwa maana ya kwamba unaelekeza, unabainisha na unawafunza watu njia ilionyooka.

[1] Ahmad (01/199) nr. (1425), at-Tirmidhiy (464), an-Nasaa´iy (1745) na Ibn Maajah (1178).

[2] 41:17

[3] 42:52

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Du´aa´ al-Qunuut-il-Witr, uk. 05-06
  • Imechapishwa: 04/03/2024