01. Mirathi mikubwa aloacha Mtume kabla ya kufa

Himdi zote anastahiki Allaah, tunamhimidi Yeye, tunamuomba msaada na msamaha. Tunajilinda Kwake kutokamana na shari ya nafsi zetu na uovu wa matendo yetu. Yule mwenye kuongozwa na Allaah hakuna wa kumpoteza, na yule mwenye kupotezwa na Allaah hakuna wa kumwongoza. Ninashuhudia ya kwamba hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah, hali ya kuwa ni mmoja hana mshirika, na ninashuhudia ya kwamba Muhammad ni mja na Mtume Wake:

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّـهَ حَقَّ تُقَاتِهِ وَلَا تَمُوتُنَّ إِلَّا وَأَنتُم مُّسْلِمُونَ

“Enyi mlioamini! Mcheni Allaah kama apasavyo kuogopwa na wala msife isipokuwa nyinyi ni waislamu.”[1]

يَا أَيُّهَا النَّاسُ اتَّقُوا رَبَّكُمُ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن نَّفْسٍ وَاحِدَةٍ وَخَلَقَ مِنْهَا زَوْجَهَا وَبَثَّ مِنْهُمَا رِجَالًا كَثِيرًا وَنِسَاءً ۚ وَاتَّقُوا اللَّـهَ الَّذِي تَسَاءَلُونَ بِهِ وَالْأَرْحَامَ ۚ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلَيْكُمْ رَقِيبًا

“Enyi watu! Mcheni Mola wenu ambaye amekuumbeni kutokana na nafsi moja na akaumba kutoka humo mke wake na akaeneza kutoka hao wawili wanaume wengi na wanawake. Na mcheni Allaah ambaye Kwake mnaombana na jamaa. Hakika Allaah amekuwa juu yenu ni Mwenye kuchunga.”[2]

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّـهَ وَقُولُوا قَوْلًا سَدِيدًا يُصْلِحْ لَكُمْ أَعْمَالَكُمْ وَيَغْفِرْ لَكُمْ ذُنُوبَكُمْ ۗ وَمَن يُطِعِ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ فَقَدْ فَازَ فَوْزًا عَظِيمًا

“Enyi mlaomini! Mcheni Allaah na semeni neni la sawasawa. Atakutengenezeeni ‘amali zenu na kukusameheni madhambi yenu na anayemtii Allaah na Mtume Wake, basi hakika amefanikiwa mafaniko adhimu.”[3]

Amma ba´d:

Hakika maneno ya kweli kabisa ni Kitabu cha Allaah, uongofu bora ni wa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), mambo maovu kabisa ni ya kuzuliwa. Hakika kila kitakachozushwa ni Bid´ah. Kila Bid´ah ni upotevu. Kila upotevu ni Motoni.

Hakika Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amekufa hali ya kuwa ameuacha Ummah wake katika weupe ambao usiku wake ni kama mchana wake – hatopotea nao isipokuwa mwenye kustahiki kuangamia. Alipofariki (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ameacha mirathi mikubwa. Hakuacha pesa wala nguo itayoisha. Bali aliacha mirathi mikubwa itayobaki. Ameacha mirathi anayoweza kuipata kila ambaye atajibidisha kufanya sababu zake. Ameacha elimu na akarithisha elimu.

Dini ya Kiislamu ni dini, yakini na matendo. Hakika sio dini ya ´ibaadah pasi na elimu – kwani hiyo ni njia ya wapotevu. Kadhalika sio dini ya elimu pasi na matendo – kwani hiyo ni njia ya wale walioghadhibikiwa. Njia ya Uislamu ni njia iliyonyooka. Ni njia ya elimu, yakini na kuitendea kazi elimu hiyo.

[1] 03:102

[2] 04:01

[3] 33:70-71

  • Mhusika: Shaykh Sulaymaan bin Saliymillaah ar-Ruhayliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Ilm wa Wasaaailuh wa Thimaaruh
  • Imechapishwa: 22/10/2016