Namna ya kuoga josho la janaba II

Swali: Ni vipi mtu anakoga josho la janaba?

Jibu: Kuna sifa mbili za kuoga janaba:

1- Njia ambayo ni ya lazima. Mtu akaosha mwili wake mzima. Amesema (Ta´ala):

وَإِن كُنتُمْ جُنُبًا فَاطَّهَّرُوا

“Mkiwa na janaba basi jitwaharisheni.”[1]

Mtu akiosha mwili wake wote kwa namna yoyote ile baada ya kunuia kunamtosheleza. Ni jambo linalojulikana kwamba kusukutua na kupandisha maji puani ni mambo yanaingia katika hilo. Kwa sababu pua na mdomo ni katika hukumu ya uinje na si hukumu ya undani. Kwa ajili hii Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akisukutua na akipalizia wakati wa kutawadha. Haya ni tafsiri ya maneno Yake (Ta´ala):

فَاغْسِلُوا وُجُوهَكُمْ

“Hivyo basi osheni nyuso zenu… “[2]

Kwa hali yoyote hii ndio sifa ya wajibu katika kuoga. Mtu ayaeneze maji mwili wake mzima mara moja. Katika hayo kunaingia pia kusukutua na kupalizia.

2- Njia ambayo imependekezwa. Mtu aoshe tupu yake na zile [sehemu] zilizochafuliwa nayo. Kisha atawadhe wudhuu´ kamilifu kama wa swalah; aoshe uso wake baada ya kusukutua na kupalizia, aoshe mikono yake mpaka kwenye visugudi, apanguse kichwa chake na masikio yake, aoshe miguu yake. Baada ya hapo akiwa ni mtu mwenye nywele nyingi ajimwagie maji juu ya kichwa chake mpaka yaingie kwenye mizizi. Kisha ajimwagie juu ya kichwa mara tatu. Halafu aoshe mwili wake uliobaki. Hii ni sifa iliopokelewa na ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Kuhusu aliyopokea Maymuunah (Radhiya Allaahu ´anhaa) kuna baadhi ya mambo yanatofautiana kidogo. Kwanza aanze kuosha tupu yake na zile [sehemu] zilizochafuliwa nayo, apige mikono yake juu ya ardhi au ukuta mara mbili au tatu aisafishe baada ya muosho huu na aioshe. Kisha asukutue na apandishe maji puani na aoshe uso wake. Halafu mikono yake mpaka kwenye visugudi. Kisha aoshe kichwa chake kikamilifu na wala asioshe miguu yake. Baada ya hapo ajimwagie maji sehemu ya mwili wake uliobaki, kisha aoshe miguu yake sehemu nyingine. Namna hii ndivo alivyopokea mama wa waumini Maymuunah (Radhiya Allaahu ´anhaa).

Bora kwa mtu atendee kazi sifa zote mbili hizi. Kwa msemo mwingine mara aoge kwa mujibu wa namna alivyopokea ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) na mara nyingine aoge kwa mujibu wa namna alivyopokea Maymuunah (Radhiya Allaahu ´anhaa). Hivyo atakuwa ni mwenye kutendea kazi Sunnah zote mbili. Ikiwa mtu hajui isipokuwa sifa moja tu katika sifa hizi mbili basi hakuna neno kwa kulazimiana nayo.

Muulizaji: Je, ni lazima kurudi kutawadha mara nyingine baada ya kuoga janaba?

Ibn ´Uthaymiyn: Si lazima.

Muulizaji: Kwa kuwa mtu atagusa ima tupu ya mbele au ya nyuma.

Ibn ´Uthaymiyn: Si lazima. Kwa kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakuwa anatawadha baada ya kuoga. Lakini akigusa dhakari yake basi ni lazima kutawadha. Sio kwa sababu ya janaba iliotangulia, lakini ni kwa sababu ya Hadiyth iliojitokeza ambayo ni kugusa dhakari. Hapa ni pale tutaposema kuwa kugusa dhakari kunachengua wudhuu´. Kwa sababu wanachuoni wametofautiana juu ya masuala haya.

[1] 05:06

[2] 05:06

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Nuur ´alaad-Darb (10) http://binothaimeen.net/content/6734
  • Imechapishwa: 24/11/2020