Huenda mtu akauliza ni vipi nimeshikamana na maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mwenye kuweka katika Uislamu njia nzuri basi atapewa ujira kwayo na ujira wa yule mwenye kuifanya mpaka siku ya Qiyaamah.”[1]

Jibu langu ni kuwa aliyesema:

“Mwenye kuweka katika Uislamu njia nzuri basi atapewa ujira kwayo na ujira wa yule mwenye kuifanya mpaka siku ya Qiyaamah.”

ndiye huyohuyo aliyesema:

“Ninakutahadharisheni na mambo ya kuzua, kwani hakika kila kitakachozushwa ni Bid´ah na kila Bid´ah ni upotevu na kila upotevu ni Motoni.”

Ni jambo lisilowezekana kwa mkweli na mwenye kusadikishwa akazungumza maneno yanayojigonga. Mwenye kudhania kuwa maneno ya Allaah (Ta´ala) au Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni yenye kujigonga anatakiwa kufanya utafiti tena. Dhana hii inatokamana ima na mapungufu ya uelewa wake au mapungufu ya uoni wake. Ni jambo lisilowezekana kabisa maneno ya Allaah (Ta´ala) au Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yakawa ni yenye kujigonga. Kwa hiyo hakuna mgongano kati ya Hadiyth hizo mbili. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kuweka njia nzuri katika Uislamu… “

Bid´ah sio katika Uislamu. Wala sio kitu kizuri. Tofauti kati ya Sunnah na Bid´ah iko wazi kabisa.

Inaweza pia kusemwa sentesi “Mwenye kuweka njia nzuri katika Uislamu… “ kunamaanishwa kuhuisha kitu ambacho kilikuwepo hapo kitambo na baadaye kikawa kimepotea. Katika hali hii Sunnah ni nisba kama jinsi Bid´ah ni nisba pindi mtu ataihuisha Sunnah hiyo baada ya kuwa imesahauliwa.

Inaweza pia kusemwa ya kwamba sababu ya Hadiyth ni kundi kubwa la watu lililokuja kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Wakati Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipoona hali zao taabani ndipo akaamrisha wasaidiwe. Mtu mmoja katika Answaar akaja na mfuko wa fedha uliokuwa mzito kiasi cha kwamba ulikuwa unakaribia kumshinda kubeba na akauweka mbele ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Ndipo uso wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ukaingiwa na furaha akasema:

“Mwenye kuweka katika Uislamu njia nzuri basi atapewa ujira kwayo na ujira wa yule mwenye kuifanya mpaka siku ya Qiyaamah.”

Hapa maana inakuwa “mwenye kufanya kitendo kizuri” na sio “mwenye kuweka kitendo kizuri” kwa sababu uwekaji [Tashriy´a] ni jambo limekatazwa. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Ninakutahadharisheni na mambo ya kuzua, kwani hakika kila kitakachozushwa ni Bid´ah na kila Bid´ah ni upotevu na kila upotevu ni Motoni.”

[1] Muslim (1017).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Ibdaa´ fiy Kamaal-ish-Shar´ wa Khatwar-il-Ibtidaa´, uk. 13-14
  • Imechapishwa: 23/10/2016