69. ´Aqiydah ya Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah juu ya kuamini siku ya Mwisho

Imaam Ibn Abiy Daawuud (Rahimahu Allaah) amesema:

ولا تُنكِرَنْ جهلاً نكيراً ومُنكراً

29 – Usimpinge kwa ujinga Nakiyr na Munkar

ولا الحوْضَ والِميزانَ إنك تُنصحُ

     wala [usipinge] Hodhi na Mizani – hakika wewe unanasihiwa

MAELEZO

Shairi hili na yanayokuja baada yake ni kuhusu kuamini juu ya siku ya Mwisho. Nayo ni siku inayokuwa baada ya dunia. Ndio siku ya malipo na hesabu. Kuiamini ni moja katika nguzo za imani sita ambayo ilitajwa katika Hadiyth ya ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) katika kisa pindi Jibriyl (´alayhis-Salaam) alipomjia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akiwa pamoja na Maswahabah zake akimuuliza kuhusu Uislamu, imani, Ihsaan na Qiyaamah. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akajibu kwamba:

“Imani ni kumuamini Allaah, Malaika Wake, Vitabu Vyake, Mitume Yake, siku ya Mwisho na kuamini Qadar kheri na shari yake.”

Nguzo hizi sita wakati fulani zinatajwa zote kwa pamoja katika Qur-aan na wakati mwingine zinatajwa baadhi yake. Mara nyingi kumuamini Allaah na siku ya Mwisho hutajwa pamoja. Amesema (Ta´ala):

مَنْ آمَنَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ

“Mwenye kumuamini Allaah na siku ya Mwisho.” (02:62)

يُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ

“Waliomwamini Allaah na siku ya Mwisho.” (09:44)

Wakati mwingine yanatajwa yote kwa pamoja. Amesema (Ta´ala):

لَّيْسَ الْبِرَّ أَن تُوَلُّوا وُجُوهَكُمْ قِبَلَ الْمَشْرِقِ وَالْمَغْرِبِ وَلَـٰكِنَّ الْبِرَّ مَنْ آمَنَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ وَالْمَلَائِكَةِ وَالْكِتَابِ وَالنَّبِيِّينَ

“Si wema pekee kuwa mnaelekeza nyuso zenu upande wa mashariki na magharibi, lakini wema khasa ni ambaye anamuamini Allaah na siku ya Mwisho na Malaika na Kitabu na Manabii.” (02:177)

آمَنَ الرَّسُولُ بِمَا أُنزِلَ إِلَيْهِ مِن رَّبِّهِ وَالْمُؤْمِنُونَ ۚ كُلٌّ آمَنَ بِاللَّـهِ وَمَلَائِكَتِهِ وَكُتُبِهِ وَرُسُلِهِ

 “Mtume ameamini yaliyoteremshwa kwake kutoka kwa Mola wake na waumini – wote wamemwamini Allaah na Malaika Wake na Vitabu Vyake na Mitume Wake.” (02:285)

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh al-Mandhuumat-ul-Haaiyyah fiy ´Aqiydati Ahl-is-Sunnah wal-Jamaa´ah, uk. 157-158
  • Imechapishwa: 12/01/2024