27- Kifo cha mtu kikikutana na kupatwa kwa jua au mwezi basi jambo hilo halifahamishi kitu chochote. Kuamini kwamba ni dalili inayofahamisha juu ya utukufu wa yule aliyekufa ni miongoni mwa ukhurafi wa kipindi cha kikafiri ambao umebatilishwa na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) siku aliyokufa mtoto wake Ibraahiym (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Jua lilipatwa na akawakhutubia watu, akamuhimidi Allaah na kumsifu. Kisha akasema:

“Amma ba´d:

Enyi watu! Watu wa kipindi cha kikafiri walikuwa wakisema kwamba jua na mwezi havipatwi isipokuwa kwa kufariki kwa mtu mtukufu. Viwili hivyo ni alama mbili miongoni mwa alama za Allaah. Havipatwi kwa kufariki au kupata uhai kwa yeyote. Allaah kwavyo anawatia khofu waja Wake. Mkiona kitu katika hayo basi kimbilieni kumtaja, kumuomba, kumtaka msamaha, kutoa swadaqah, kuwaachia watumwa huru na kuswali misikitini mpaka iondoke hali hiyo.”

Mtiririko huu umeokotwa kutoka katika jumla ya Hadiyth kadhaa ambazo nimezitaja katika kitabu changu “Swalaat-ul-Kusuuf”. Ndani yake nimezungumzia njia na matamshi yake. Halafu mwisho wake nikakusanya ufupisho wake katika mtririko mmoja. Kiasi kidogo hichi ni kutoka huko. Nyingi zake ziko katika kwa al-Bukhaariy na Muslim na katika tungo za “as-Sunan”.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Janaa-iz wa Bid´ahaa, uk. 63
  • Imechapishwa: 13/02/2020