Swali: Tunaona katika baadhi ya nchi za Kiislamu watu wanaotufu katika makaburi kutokana na ujinga. Ni ipi hukumu ya watu hawa? Je, mmoja wao anaweza kuitwa mshirikina?

Jibu: Hukumu ya mwenye kuyaomba masanamu, akayataka uokozi na mfano wake iko wazi; ni ukafiri mkubwa. Isipokuwa akidai kuwa ametufu makaburi kwa lengo la kumwabudu Allaah kama anavotufu kwenye Ka´bah na hivyo akafikiri kuwa inafaa kutufu kwenye makaburi na asikusudie kwa kufanya hivo kujikurubisha kwa wenye nayo na kwamba eti amekusudia kujikurubisha kwa Allaah pekee. Huyu anazingatiwa kuwa ni mzushi na sio kafiri. Kwa sababu kutufu kwenye makaburi ni Bid´ah na maovu kama vile kuswali makaburi. Yote hayo ni miongoni mwa njia zinazopelekea katika ukafiri.

Lakini mara nyingi kwa watu wanaoyaabudia makaburi ni kujikurubisha kwa wenye nayo kwa kuyazunguka, kama wanavyojikurubisha kwayo kwa kuyachinjia na kuyawekea nadhiri. Yote hayo ni shirki kubwa. Yeyote anayekufa katika hali hiyo amekufa akiwa ni kafiri; haoshwi, haswaliwi, hazikwi kwenye makaburi ya waislamu na huko Aakhirah jambo lake liko kwa Allaah. Akiwa si miongoni mwa wale waliofikiwa na ujumbe basi atakuwa miongoni mwa Ahl-ul-Fatrah. Dalili ya hilo ni yale yaliyompitikia mama yake na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hakufikiwa na ujumbe na alikuwa katika dini ya watu wake. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimwomba idhini Mola Wake ya kumuombea msamaha lakini hakumpa idhini ya kufanya hivo. Kwa sababu alikuwa katika dini ya watu kabla ya kuja Uislamu. Vivyo hivyo baba yake amesema juu yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wakati muulizaji alipomuuliza kuhusu baba yake ambapo akamjibu kwa kusema:

“Baba yangu na baba yako wako Motoni.”[1]

Baba yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikufa katika kipindi kabla ya kuja Uislamu juu ya dini ya watu wake. Hivyo hukumu yake ikawa hukumu ya makafiri. Lakini yule ambaye hakufikiwa na ujumbe hapa duniani na akafa bila kuijua haki basi atapewa mtihani siku ya Qiyaamah kwa mujibu wa maoni sahihi zaidi ya wanazuoni. Akifaulu ataingia Peponi na akiasi ataingia Motoni. Hali kadhalika wengineo katika Ahl-ul-Fatrah ambao hawakufikiwa na ulinganizi. Amesema (Ta´ala):

وَمَا كُنَّا مُعَذِّبِينَ حَتَّىٰ نَبْعَثَ رَسُولًا

”Hatukuwa Wenye kuadhibu mpaka tumtume Mtume.”[2]

Ama wale waliofikiwa na Qur-aan na kutumilizwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wasiitikie, basi hoja imekwishawasimamia. Amesema (´Azza wa Jall):

وَأُوحِيَ إِلَيَّ هَـٰذَا الْقُرْآنُ لِأُنذِرَكُم بِهِ وَمَن بَلَغَ

“Nimefunuliwa Wahy hii Qur-aan ili nikuonyeni kwayo na kila itakayomfikia.”[3]

Bi maana aliyefikiwa na Qur-aan basi amekwishaonywa.

Vilevile amesema (Ta´ala):

هَـٰذَا بَلَاغٌ لِّلنَّاسِ وَلِيُنذَرُوا بِهِ

“Hii ni ufikishwaji wa ujumbe kwa watu na ili wawaonye kwayo.”[4]

Yule ambaye amefikiwa na Qur-aan na akafikiwa na Uislamu na asiingie ndani yake, basi ana hukumu moja kama ya makafiri. Imesihi kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Naapa kwa Yule ambaye nafsi yangu iko mikononi Mwake. Hakuna yeyote atakayesikia kuhusu mimi, si myahudi wala mkristo, kisha akafa na asiamini yale nilivyotumilizwa nayo isipokuwa atakuwa miongoni mwa watu wa Motoni.”[5]

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake.

Amefanya kule kusikia kutumilizwa kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni hoja dhidi yake.

Kwa kumalizia ni kwamba ambaye atadhihirisha ukafiri katika mji wa Kiislamu basi hukumu yake ni hukumu ya makafiri. Kuhusu siku ya Qiyaamah kama atakuwa ni mwenye kusalimika au si mwenye kusalimika hili anaachiwa Allaah (Sunhaanahu wa Ta´ala). Kama alikuwa miongoni mwa wale ambao hawakufikiwa na ulinganizi na hawakusikia kutumilizwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), basi watapewa mtihani siku ya Qiyaamah. Watatumiwa kipande cha Moto aina ya shingo ndefu, kama ilivyopokelewa katika Hadiyth ya al-Aswad Sariy´, na kumwambia aingie ndani. Akiingia ndani utakuwa kwake ni baridi tena yenye salama, na akikataa shingo hiyo itageuzwa na kuingizwa Motoni[6]. Tunamuomba Allaah usalama.

Kwa kumalizia ni kwamba wale ambao hawakufikiwa na ulinganizi, kama vile wale walioko pembezoni mwa dunia, katika nyakati ambazo kumesimamishwa kutumilizwa Mitume, ujumbe umemfikia lakini ni mwendawazimu asiyekuwa na akili au mtumzima sana asiyekuwa na akili, watu aina hii na mfano wao kama vile watoto wa washirikina ambao wamekufa bado wachanga, watoto wa washirikina ambao wamekufa bado hawajafikia labeghe, wote hawa jambo lao liko kwa Allaah. Allaah ndiye anayejua nini atakachowafanya. Hivo ndivo alivojibu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambaye alimuuliza juu yao. Allaah atadhihirisha ujuzi Wake kwao kwa kuwapa mtihani; ambaye atafaulu katika wao, ataingia Peponi, na yule atakayefeli, ataingia Motoni.

[1] Muslim (203).

[2] 17:15

[3] 06:19

[4] 14:52

[5] Muslim (153).

[6] Ahmad (15866).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr min Fitnat-il-Qubuur, uk. 79-72
  • Imechapishwa: 07/07/2022