140. Miongoni mwa dalili kwamba Allaah atawafufua viumbe baada ya kufa

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema

Kauli Yake (Ta´ala):

وَاللَّـهُ أَنبَتَكُم مِّنَ الْأَرْضِ نَبَاتًا ثُمَّ يُعِيدُكُمْ فِيهَا وَيُخْرِجُكُمْ إِخْرَاجًا

”Na Allaah amekuotesheni kutoka katika ardhi mimea; kisha atakurudisheni humo [ardhini] na atakutoeni [tena upya] mtoke.”[1]

MAELEZO

وَاللَّـهُ أَنبَتَكُم مِّنَ الْأَرْضِ

”Na Allaah amekuotesheni kutoka katika ardhi mimea.”

Pindi alipoumbwa Aadam (´alayhis-Salaam):

ثُمَّ يُعِيدُكُمْ فِيهَا

“Kisha atakurudisheni humo [ardhini]… “

Bi maana kwa kufa na kuingizwa makaburini:

وَيُخْرِجُكُمْ إِخْرَاجًا

“… na atakutoeni [tena upya] mtoke.”

Huku ndio kufufuliwa. Watatolewa ndani ya makaburi na kupelekwa katika uwanja. Amesema (Ta´ala):

فِيهَا تَحْيَوْنَ وَفِيهَا تَمُوتُونَ وَمِنْهَا تُخْرَجُونَ

”Humo mtaishi, na humo mtakufa na kutoka humo mtatolewa.”[2]

Bi maana mtapewa uhai juu ya mgongo wake. Humo mtafishwa na humo mtatolewa kwa ajili ya kufufuliwa siku ya Qiyaamah. Hizi ni dalili kutoka katika Qur-aan juu ya kufufuliwa.

Pia kuna dalili ya kiakili kutoka katika Qur-aan yenyewe. Nayo ni kwamba yule ambaye ameweza kuanzisha basi ana haki zaidi ya kuweza kukirudisha kitu hicho. Amesema (Ta´ala):

وَهُوَ الَّذِي يَبْدَأُ الْخَلْقَ ثُمَّ يُعِيدُهُ وَهُوَ أَهْوَنُ عَلَيْهِ ۚ وَلَهُ الْمَثَلُ الْأَعْلَىٰ فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۚ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ

”Naye ndiye aliyeanzisha uumbaji, kisha anaurudisha, nayo ni mepesi mno Kwake. Naye ana wasifu wa juu kabisa katika mbingu na ardhi. Naye ni Mwenye nguvu kabisa aliyeshinda, Mwenye hekima ya kila jambo.”[3]

Ambaye ameweza kuwaumba watu kutoka katika kisichokuwa kitu ana haki zaidi ya kuwarudisha baada ya wao kufa. Hii ni dalili ya kiandiko na ya kiakili.

[1] 71:17-18

[2] 07:25

[3] 30:27

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 278
  • Imechapishwa: 16/02/2021