Suufiyyah wamepetuka mipaka kwa kuwatakasa Mashaykh zao kaisi cha kwamba mpaka wakaona kuwa kila kinachofanywa na Shaykh ni haki na sahihi bali dalili ya fadhilah na karama zake. Wameandika “karama” za Mashaykh zao katika vitabu vyao, nayo ni aina mbalimbali na inafikia daraja zote, kwa mfano daraja ya kuwahuisha wafu. Zengine hazina maana yoyote, kiasi cha kwamba mpaka mtu anaona haya kuyataja.

Kuhuisha wafu

Sikiliza makarama mbalimbali yaliyopokelewa na ´Abdur-Rahmaan al-Manaawiy:

“Aina ya kwanza: kumuhuisha wafu, aina ambayo ndio ya juu kabisa. Miongoni mwayo ni kwamba Abu ´Ubayd al-Yusriy alipigana vita na alikuwa pamoja na kipando cha mnyama ambaye alikufa. Akamuomba Allaah Amhuishe na akasimama na kutikisa masikio. Mufarrij ad-Damaamiyniy aliletewa ndege wa kuchomwa. Akasema: “Ruka kwa idhini ya Allaah (Ta´ala) na yule ndege akaruka. al-Kaylaaniy aliweka mkono wake juu ya mfupa wa kuku aliyokula na akauambia: “Simama kwa idhini ya Allaah” ambapo akasimama. Mtoto wa mwanafunzi wa Abu Yuusuf ad-Dahmaaniy alikufa ambapo akamhuzunikia. Kisha Shaykh akamwambia: “Simama kwa idhini ya Allaah” ambapo akasimama na kuishi maisha marefu.”[1]

Karama hizi, bali tuseme miujiza hii, haiwezi kulinganishwa na miujiza ambayo Mtume wa Allaah ´Iysaa (´alayhis-Salaam) alifanya, miujiza ambayo ni maalum kwake.

Mijibwa wa kiwalii ya Suufiyyah

ash-Sha´raaniy ameeleza kuhusu makarama ya al-´Ajmiy:

“Jicho lake lilimwangukia jibwa mmoja basi mijibwa yote ikajisalimisha kwake. Baadaye watu wakawa wanaijia ili iwatatulie matatizo yao. Jibwa yule akawa mgonjwa na mijibwa mingine ikakusanyika pambizoni mwake wakilia. Alipokufa wakadhihirisha kulia kwao na kuomboleza kwa kujiadhibu. Hivyo Allaah (Ta´ala) Akawapa Ilhaam baadhi ya watu na wakamzika. Mbwa wengine wakawa wanalitembelea kaburi lake mpaka nao wakafa. Ikiwa haya ni matokeo ambayo yameweza kufanyika kwa jicho lililomnenga mbwa, jifikirie hali ingekuweje lau jicho hili lingemnenga mtu?”[2]

ash-Sha´raaniy amedai pia kwamba bwana wake Ahmad al-Badawiy anaendesha ulimwengu ilihali yuko ndani ya kaburi lake. Anasema:

“Shaykh wangu alichukua ahadi kutoka kwangu kwenye kaburi wakati nilipokuwa nimesimama mbele ya Ahmad al-Badawiy na akanisalimia kwa kunipa mkono. Akautoa nje ya kaburi mkono wake mtukufu na ukashika mkono wangu. Kiongozi wangu ash-Shanaawiy akasema: “Iweke akili yako kwake na mfanye awe chini ya macho yako.” Hivyo nikamsikia kiongozi wangu Ahmad al-Badawiy akisema kutoka ndani ya kaburi lake: “Ndio.” Kisha akasema: “Sikuweza kushiriki katika siku ya kuzaliwa. Kulikuwepo mmoja katika mawalii na akanieleza kwamba Ahmad al-Badawiy siku hiyo alikuwa ametoa nguo ya juu ndani ya kaburi lake na akasema: “´Abdul-Wahhaab amekuja.”[3]

Je, mtu hatosikia aibu yoyote kwa kusimulia “karama” na jarima za Suufiyyuun, ambazo zinahusiana waziwazi na kuwajamii wanyama barabarani na majanga mengine, pamoja na kudai ya kwamba ni moja katika “karama” zao? Wacha tuwatajie moja katika “karama” hizi za Shaykh Ibraahiym al-´Uryaan. ash-Sha´raaniy amesema:

“Miongoni mwao ni Shaykh Ibraahiym al-´Uryaan ambaye alikuwa akipanda juu ya minbari na akiwatolea Khutbah uchi… na watu walikuwa wakizingatia yale anayoyasema.”

Hata wizi unazingatiwa kuwa ni katika karama za Suufiyyuun. Msikilize ad-Dibaagh, ambaye ni mmoja katika viongozi wao, ambaye amesema:

“Walii aliye na mamlaka ya kuendesha ulimwengu anaweza kuunyoosha mkono wake ndani ya mfuko wa yeyote anayetaka na kuchukua pesa zozote anazotaka, pasi na mwenye mfuko huyo kuhisi kitu.”[4]

Huyu ni Suufiy anayedai ya kwamba kuona kwa Shaykh wake kuna manufaa zaidi kuliko kuona kwa Allaah. Siku moja Abu Twuraab alimwambia muridi wake:

“Lau ungelimuona Abu Yaziyd al-Bustwaamiy.” Hivyo akawa amesema: “Sina muda wa hilo, kwa kuwa nimemuona Allaah. Imenitosheleza kwangu kwa kuwa na haja ya Abu Yaziyd.” Abu Twuraab akasema: “Ole wako! Unajifakhari kwa kuwa umemuona Allaah (´Azza wa Jall), lau ungelimuona Abu Yaziyd mara moja, ingelikuwa ni bora kwako kuliko kumuona Allaah mara sabini.”[5]

al-Ghazzaaliy ameongeza:

“Mfano wa mafunuo kama haya haitakikani kwa muumini kuyakanusha.”

Ndugu wapendwa! Mapokezi haya yanatuonyesha ya kwamba viongozi wa Suufiyyah hawajatosheka kwa kuhalalisha vile Alivyoharamisha Allaah katika kuiba, machafu na mengineyo, bali wameyafanya hayo ni katika alama za uwalii na karama. Hayo yanapingana  waziwazi na mafunzo ya Uislamu. Isitoshe ni kufuru ya wazi kabisa kwa maandiko ya Qur-aan na Sunnah iliyotwaharishwa. Wanachuoni wa Uislamu wameafikiana juu ya kwamba yule anayehalalisha yale Aliyoharamisha Allaah ambayo yanajulikana fika kuwa ni haramu, ni kafiri. Vipi basi kwa yule anayeona ya kwamba kutenda madhambi makubwa ni katika alama ya uwalii na makarama?

Ishara kubwa na ya khatari kabisa kwa Suufiyyah ni kumuomba asiyekuwa Allaah. Wanawaomba wafu. Hii ndio shirki kubwa ambayo imetahadharishwa na Qur-aan Tukufu:

وَلَا تَدْعُ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُكَ وَلَا يَضُرُّكَ ۖ فَإِن فَعَلْتَ فَإِنَّكَ إِذًا مِّنَ الظَّالِمِينَ

“Wala usiombe badala ya Allaah asiyekufaa na wala asiyekudhur; na ukifanya hivyo, basi hakika utakuwa miongoni mwa madhalimu.” (Yuunus 10:106-107)

Kwa msemo mwingine utakuwa miongoni mwa washirikina.

al-Buuswayriy – mshairi wa Suufiyyah – amesema akimsemeza Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

Ee kiumbe mbora! Sina mwengine zaidi yako wa kumkimbilia wakati wa majanga

Usiponitukuza siku ya Qiyaamah na ukanishika mkono, nimeangamia.

Katika ukarimu wako ni pamoja na dunia hii na mali zake

na miongoni mwa elimu zako ni pamoja na elimu ya Ubao na Kalamu.

[1] Haadhihi hiyaa as-Suufiyyah, uk. 116, na “al-Kawaakib ad-Durriyyah”, uk. 11 cha ´Abdur-Rauuf al-Manaawiy.

[2] Haadhihi hiyaa asSuufiyyah, uk. 113, na at-Twabaqaat (2/61) katika wasifu wa al-´Ajmiy.

[3] Haadhihi hiyaa as-Suufiyyah, uk. 113.

[4] Haadhihi hiyaa as-Suufiyyah, uk. 124, na “al-Ibriyz” (2/12) ya ad-Dibaagh.

[5] Ufupisho kutoka kwenye “Ihyaa´ ´Uluum-id-Diyn” (4/356) ya al-Ghazzaaliy.

  • Mhusika: Shaykh Muhammad bin Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Haqiyqat-us-Suufiyyah
  • Imechapishwa: 25/12/2019