176- Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Lau angelijua yule anayekunywa ilihali amesimama kile kilichomo tumboni mwame basi angekitapika.”

Ameipokea ´Abdur-Razzaaq katika ”al-Muswannaf” (10/427) Ahmad (7795) kupitia kwake na Ibn Hibbaan (5300) kupitia kwa az-Zuhriy, kutoka kwa mtu, kutoka kwa al-A´mash, kutoka kwa Abu Swaalih, wote wawili wamepokea kutoka kwa Abu Hurayrah ambaye amesimulia kile kilichosemwa na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Katika Hadiyth kuna kiashirio kizuri chenye kuonyesha makatazo ya kunywa hali ya kusimama. Ni jambo limetajwa kwa uwazi katika Hadiyth ya Anas (Radhiya Allaahu ´anh):

“Amekataza (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) – katika upokezi mwingine imekuja “amekemea” – kunywa hali ya kuwa mtu amesimama.”

Ameipokea Muslim (6/110), Abu Daawuud (3717), at-Tirmidhiy (3/111), ad-Daarimiy (2/120), Ibn Maajah (2/338)…

Udhahiri wa makatazo katika Hadiyth hizi unaonyesha kuwa ni haramu kunywa kwa kusimama pasi na udhuru. Kumepokelewa vilevile Hadiyth nyingi ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikunywa hali ya kusimama. Matokeo yake wanachuoni wakatofautiana juu ya kitendo hicho. Wanachuoni wengi wanasema kwamba imechukizwa na kwamba imependekezwa kukitapika kile kilichonywiwa. Ibn Hazm ametofautiana nao na amesema kwamba kitendo hicho ni haramu. Huenda maoni haya ndio sahihi zaidi. Kwani kitu kilichochukizwa au kilichopendekezwa tu hakifuatiwi kwa tamko “amekemea”. Kutapika ni jambo lina uzito na tabu kubwa kwa mtu. Sitambui kuwa Shari´ah inamuwajibisha mtu kutapika ikiwa ni kama malipo ya kitu kilichopendekezwa tu! Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Shaytwaan amekunywa pamoja nawe.”

Katika Hadiyth hii kuna matahadharisho makubwa juu ya kunywa hali ya kusimama. Kitu kama hicho haisemwi kuwa mtu ameacha tu jambo lililopendekezwa.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Silsilat-ul-Ahaadiyth as-Swahiyhah (1/1/338-340)
  • Imechapishwa: 18/05/2019