Ulinganisho huu unafahamisha kuonesha ni ujinga kiasi gani alonao. Vipi Haafidhw Ibn Hajar na an-Nawawiy watalinganishwa na watu kama at-Turaabiy, al-Ghazaaliy na al-Qaradhwaawiy. Vipi udongo utalinganishwa na nyota? Vipi kinyesi kitalinganishwa na ngamia?

Hao waliotajwa mwanzoni wanapenda Sunnah. Wanaifasiri. Wanaibainisha. Makosa waliyotumbukia ndani yake ni madogo ukilinganisha na yale waliyobainisha katika mambo ya Uislamu. Wanachuoni siku zote wamenufaika kwa maneno yao. Wameifahamu Qur-aan na Sunnah kutokana na waliyobainisha. Walikuwa ni wanachuoni wa kweli.

Ama kuhusu hawa wa leo kama at-Turaabiy, al-Ghazaaliy, al-Qaradhwaawiy na at-Tilmisaaniy, ni wakubwa wa vigogo ya watu wanaowakimbiza watu kutoshikamana na Sunnah. Hali inatofautiana kati ya mtu mwenye kukosea katika suala fulani, tawi au katika suala limoja la ´Aqiydah au mawili na mwenye kwenda kinyume na asli yenyewe. Watu hawa wa mwisho waliotajwa hawajali Tawhiyd. Wala hawaitilii umuhimu wowote. Bali uhakika wa mambo ni kwamba Ahl-ut-Tawhiyd wameudhika na wao kwa kiasi kikubwa, kama inavyoshuhudiwa.

at-Turaabiy hali yake inajulikana. Anaonelea kuwa ni lazima kuifanya upya misingi ya Uislamu na Fiqh. Anasema kuwa misingi ya Fiqh ni istilahi tu za wanachuoni za jinsi ya kufahamu Qur-aan na Sunnah na ambayo hatuhitajii kuifuata. Anasema kuwa leo tunahitajia misingi mipya ya Fiqh ili kwayo tuweze kufahamu Qur-aan na Sunnah kwa njia inayoendana na zama za leo.

al-Ghazaaliy anairudisha Sunnah pale ambapo haiendani na akili zake na ufahamu wake. al-Qaradhwaawiy ana mfumo huo huo. Anapita njia hiyo hiyo ingawa yeye haoneshi hilo wazi wazi kama al-Ghazaaliy.

at-Tilmisaaniy haitambui ni nini Tawhiyd-ul-´Ibaadah. Hajui ni nini Sunnah. Anachanganya mambo yote haya kwa njia mbaya sana.

Watu hawa wane na mfano wao wanatoka katika shule moja: shule ya al-Ikhwaan al-Muslimuun. Shule misingi na mfumo wake unajulikana. Kwa hivyo sio maajabu ikazalisha watu kama hawa na wakawa ni wenye kuishi mpaka hivi leo kwa kuzingatia ya kwamba wamelelewa kutokana na misingi ya shule hiyo.

Kwa ajili hiyo ni wajibu kuwaraddi na kanuni zao. Kwa sababu wanawapoteza vijana kwa kutumia jina la Da´wah. Vijana wanawaadhimisha kwa kuonelea kuwa ni walinganizi wa Uislamu.

Ama kuhusiana na al-Haafidhw Ibn Hajar na an-Nawawiy, hatujawahi kusikia hata siku moja ya kwamba kuna yeyote ambaye ametetea makosa yao ya ´Aqiydah waliyotumbukia ndani yake. Makosa yao yalifanywa katika wakati wao na wakati watu bado wanaendelea kustafidi na elimu yao iliyobobea na ufahamu wao wenye kutoa mwanga. Ama kuhusu wale wengine, wasilinganishwe. Haijuzu kuwalinganisha na wao na kuwazingatia kuwa wako sawa. Udongo haulinganishwi na nyota.

  • Mhusika: Shaykh Swaalih bin ´Abdil-´Aziyz Aal ash-Shaykh
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: https://www.youtube.com/watch?v=7kfcyHHfYO0&feature=youtu.be&app=desktop
  • Imechapishwa: 23/07/2020