Swali: Ni ipi hukumu ya wudhuu´ kwa yule ambaye kwenye kucha zake amepaka rangi ya kucha?

Jibu: Rangi ya kucha ni kitu anachopaka mwanamke juu ya kucha na ni kitu kilicho na ukoko. Haijuzu kwa mwanamke kuitumia kipindi ambapo anaswali kwa kuwa inazuia maji kufika kwenye ngozi wakati wa kutawadha. Kila kitu kinachozuia maji kufika kwenye ngozi haijuzu kwa mwenye kutawadha kukitumia. Kwa kuwa Allaah amesema:

فَاغْسِلُوا وُجُوهَكُمْ وَأَيْدِيَكُمْ

“Hivyo basi osheni nyuso zenu na mikono yenu mpaka kwenye visugudi.” (05:06)

Mwanamke huyu ambaye amepaka juu ya kucha zake rangi ya kucha yanazuia maji kufika kwenye ngozi. Kwa hivyo hawezi kusadikishwa ya kwamba ameosha mikono. Katika hali hiyo anakuwa ameacha kiungo cha faradhi wakati wa kutawadha au wakati wa kuoga.

Kuhusu wale wasioswali, kama mfano wa mwanamke mwenye hedhi, hakuna neno kuitumia. Isipokuwa ikiwa kama rangi hii ni katika mambo maalum ya makafiri. Katika hali hiyo itakuwa haijuzu kwa kuwa itakuwa ni kujifananisha.

Nimewasikia baadhi ya watu waliotoa fatwa ya kwamba rangi hii inaingia katika aina ya kuvaa soksi na kwamba inajuzu kwa mwanamke kuitumia kwa muda wa mchana mmoja na usiku wake kwa yule ambaye ni mkazi na kwa muda wa michana mitatu na nyusiku zake kwa yule amabaye ni msafiri. Fatwa hii ni ya kimakosa. Sio kila kitu kinachofunika miili ya watu kinaingizwa katika soksi. Shari´ah imekuja kufahamisha kuwa mtu anatakiwa kufuta juu ya khofu pindi mtu anapohitajia kufanya hivo. Mguu unahitajia kufunikwa na kusitiriwa kwa kuwa unagusa chini katika ardhi kwenye changarawe, baridi na mengineyo. Ndipo Shari´ah ikaja kusunisha kufuta juu yake. Mtu anaweza kutumia kipimo juu ya kilemba vilevile. Si sahihi kwamba kilemba mahala pake ni kichwani. Kimsingi ni kwamba ufutaji wa kwenye kichwa ni mwepesi. Ufaradhi wa kwenye kichwa ni kufuta tofauti na mkono ambao unatakiwa kuoshwa. Kwa ajili hii Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakumpa ruhusa mwanamke kufuta vifuniko vyake vya mikono (gloves) pamoja na kuwa vinafunika mikono. Hii ni dalili inayofahamisha kuwa haijuzu kwa mtu kutumia kipimo kwa kila kizuizi kinachozuia maji kufika na kikalinganishwa na kilemba na soksi.

Ni wajibu kwa muislamu kutumia juhudi zake katika kuitambua haki na wala asitoe fatwa yoyote isipokuwa atambue kuwa Allaah atamuuliza juu yake. Kwa kuwa mtu anaelezea kuhusu Shari´ah ya Allaah (´Azza wa Jall).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (11/147-148)
  • Imechapishwa: 01/07/2017