Swali: Ni ipi hukumu ya Shari´ah kwa mtazamo wenu kuhusu kusherehekea siku ya kuzaliwa? Je, ni Bid´ah nzuri au ni Bid´ah mbaya?

Jibu: Kusherehekea siku za kuzaliwa, ni mamoja ni ya Mitume, ya wanazuoni au ya watu binafsi, yote haya ni miongoni mwa Bid´ah ambazo Allaah (Ta´ala) hakuteremsha ushahidi wowote juu yake. Mbora na mtukufu zaidi aliyezaliwa ni Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Haikuthibiti kutoka kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), kutoka kwa makhaliyfah wake waongofu, kutoka kwa Maswahabah wake, wanafunzi wa Maswahabah wala kutoka vizazi bora, kwamba walifanya sherehe katika mnasaba wa kuzaliwa kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hapana vyengine isipokuwa hiyo ni miongoni mwa Bid´ah zilizozushwa baada ya karne bora kupitia mikono ya baadhi ya wajinga waliowafuata kichwa mchunga manaswara katika sherehe yao ya kuzaliwa kwa al-Masiyh (´alayhis-Salaam). Manaswara ndio wazushi wa Bid´ah hii. al-Masiyh (´alayhis-Salaam) hakuwawekea Shari´ah ya kusherehekea kuzaliwa kwake. Bali wao wenyewe ndio waliizua. Kisha baadhi ya waislamu baada ya karne bora wakawaiga kipofu. Matokeo yake wakasherehekea mazazi yake Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kama wanavyosherehekea manaswara kuzaliwa kwa al-Masiyh (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Makundi yote mawili ni wazushi na wapotofu katika jambo hili. Hakika Manabii hawakuwawekea Shari´ah ummah zao sherehe za kuzaliwa kwao. Bali waliwasunishia kuwafuata, kuwatii na kuwafuata maisha yao kwa yale ambayo Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) ameyaamrisha. Hii ndiyo Shari´ah. Ama hizi sherehe za mazazi zote ni katika kupoteza muda, kupoteza mali, kufufua Bid´ah na kuwapeleka watu mbali na Sunnah.

  • Muhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (02/693)
  • Imechapishwa: 09/09/2025