Swali: Je, inafaa kwa mtu kuomba kuwa miongoni mwa hao watu 70.000[1]?

Jibu: Ni vyema. Kama ambavo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimwambia ´Ukkaashah:

”Ee Allaah! Mjaalie awe katika wao.”

Hilo ni kutokana na ukamilifu wa kumcha kwake Allaah na ukamilifu wa imani yake.

[1] Huswayn bin ´Abdir-Rahmaan amesema:

“Nilikuwa kwa Sa´iyd bin Jubayr pindi aliposema: “Ni nani kati yenu aliyeona kimondo [nyota] jana usiku?” Nikasema: “Mimi.” Halafu nikaeleza kwamba sikuwa nikiswali wakati ule kwa sababu nilikuwa nimedonolewa [na mdumu mwenye sumu]. Akasema: “Sasa ulifanya nini?” Nikasema: “Nilijitibu.” Akasema: “Kipi kilichokupelekea ufanye hivyo?” Nikasema: “Ni kutokana na Hadiyth aliyotuelezea ash-Sha´biy.” Nikasema: “Alikuelezeni nini?” Nikasema: “Ametueleza kutoka kwa Buraydah bin al-Huswayb ambaye amesema: “Ruqyah hairuhusiwi isipokuwa kwa ajili ya kijicho au homa.” Akasema: “Amefanya vyema kukomea kwenye alosikia. Lakini hata hivyo Ibn ´Abbaas ametusimulia ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema: “Ummah zote zilipitishwa mbele yangu, nikamuona Mtume akiwa na kundi dogo la watu, na Mtume akiwa na mtu mmoja au wawili, na Mtume akiwa hana mtu yeyote. Kisha nikaonyeshwa idadi kubwa ya watu niliodhania ni katika Ummah wangu, lakini nikaambiwa:  “Huyo ni Muusa na watu wake.” Kisha nikatazama nikaona kundi kubwa ambalo nikaambiwa: “Hawa ni watu wako, miongoni mwao kuna 70.000 watakaoingia Peponi bila ya kufanyiwa hesabu wala adhabu.” Kisha akainuka na kwenda nyumbani. Huku nyuma watu wakaanza kujadiliana ni nani hao watakaoweza kuwa? Baadhi yao wakasema: “Pengine ni Maswahabah wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).” Wengine wakasema: “Pengine ni wale waliozaliwa katika Uislamu na hawakumshirikisha Allaah na chochote.” Wakataja mengine kadhaa. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akatoka na kuja na wakamweleza waliyokuwa wakiyajadili. Akasema:  “Ni wale wasioomba kusomewa Ruqyah, hawajichomi chuma cha moto na wala hawaamini rajua nzuri na mbaya, bali wanamtegemea Mola Wao.” ‘Ukaashah bin Mihswan (Radhiya Allaahu ‘anh) aliposikia alisimama akasema: “Muombe Allaah anijaalie kuwa mmoja wao.” Akasema: “Wewe ni katika wao.” Kisha akasimama mtu mwengine na kusema: “Muombe Allaah anijaalie kuwa mmoja wao.” Akasema: “´Ukaashah amekutangulia.” (al-Bukhaariy (5705) na Muslim (220).)

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: https://binbaz.org.sa/fatwas/24371/هل-يجوز-الدعاء-بجعله-من-السبعين-الفا
  • Imechapishwa: 03/10/2024