Kula kichinjwa cha Udhhiyah ambacho hakikutajiwa jina la Allaah

Swali: Tukichinja Udhhiyah na tukasahau kuleta Tasmiyah nimekusikia ukisema kwamba kichinjwa hiki haijuzu kukila ilihali Allaah (Ta´ala) amesema:

رَبَّنَا لَا تُؤَاخِذْنَا إِن نَّسِينَا أَوْ أَخْطَأْنَا

“Ee Mola wetu! Usituchukulie pale tutaposahau au tukikosea.”[1]

وَلَيْسَ عَلَيْكُمْ جُنَاحٌ فِيمَا أَخْطَأْتُم بِهِ وَلَـٰكِن مَّا تَعَمَّدَتْ قُلُوبُكُمْ

”Hapana dhambi juu yenu katika yale mliyoyakosea, lakini isipokuwa katika yale yaliyoyakusudia nyoyo zenu.”[2]

Jibu: Mtu amechinja Udhhiyah na amesahau kutaja jina la Allaah – je, kichinjwa hicho kitakuwa ni halali au si halali? Jibu ni kwamba si halali. Kwa sababu Allaah (Ta´ala) amesema:

وَلَا تَأْكُلُوا مِمَّا لَمْ يُذْكَرِ اسْمُ اللَّـهِ عَلَيْهِ

“Wala msile katika ambavyo havikutajiwa jina la Allaah.”[3]

Amesema kwa kuachia. Hapa kuna mambo mawili:

1- Kitendo cha mchinjaji.

2- Kitendo cha kula.

Akichinja na akasahau kutaja jina la Allaah hapati dhambi. Kwa sababu Allaah (Ta´ala) amesema:

رَبَّنَا لَا تُؤَاخِذْنَا إِن نَّسِينَا أَوْ أَخْطَأْنَا

“Ee Mola wetu! Usituchukulie pale tutaposahau au tukikosea.”

Lakini kinachobaki ni kitendo cha kula. Mwenye kula haifai kwake kukila ilihali anajua kuwa hakikutajiwa jina la Allaah kwa sababu Allaah amemkataza kufanya hivo. Lakini tukikadiria kuwa yule mwenye kula amekula kwa kusahau au kwa kutokujua hapati dhambi. Haya tuliyothibitisha ndio muqtadha wa dalili za Qur-aan na Sunnah na ndio chaguo la Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah).

Huenda mtu akasema kwamba kutakuwa kumepotea pesa nyingi ikiwa kwa mfano kilichochinjwa ni ngamia? Tunasema kwamba zikipotea basi zimepotea kwa amri ya Allaah:

وَلَا تَأْكُلُوا مِمَّا لَمْ يُذْكَرِ اسْمُ اللَّـهِ عَلَيْهِ

“Wala msile katika ambavyo havikutajiwa jina la Allaah.”[4]

Zikipotea basi baada ya siku hiyo hatosahau tena maishani kutaja jina la Allaah. Kwa sababu atakuwa akikumbuka kuwa kilimpotea kichinjwa hichi.

Unaonaje ikiwa mtu ataswali akiwa na hadathi na mwenye kusahau. Hana dhambi kwa swalah hiyo. Lakini hata hivyo ni lazima kwake kurudi kuiswali kwa kukosekana kwa sharti. Tumetaja maneno ya kutosha kuhusiana na masuala haya katika kitabu chetu “al-Udhhwiyah wadh-Dhakaah”. Lau ukirejea huko itakuwa ni vyema.

[1] 02:286

[2] 33:05

[3] 06:121

[4] 06:121

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa´ ash-Shahriy (73) http://binothaimeen.net/content/1713
  • Imechapishwa: 02/08/2020