Swali: Wakati ulipotuswalisha swalah ya kupatwa kwa jua tumesikia kutoka kwako yafuatayo; Takbiyr kabla ya swalah ambapo umesema “Allaahu Akbar”, “Allaahu Akbar laa ilaaha illa Allaah”. Pili umekariri kisomo cha baadhi ya Aayah katika swalah. Je, haya ni mambo yamewekwa katika Shari´ah?

Jibu: Haya ni miongoni mwa mambo yanayofahamisha kwamba ndugu zetu wanawachunga  wanachuoni na kutazama nini wanayoyasema, nini wanayoyafanya na nini ameacha. Namuomba Allaah niwe mmoja wao. Kwa hali yoyote mimi nafurahishwa na jambo hili. Mimi nafurahishwa juu ya mtu kuuliza jambo ambalo nimefanya na yeye anaona kuwa si la sawa ili mambo yawe wazi. Mimi nimeleta Takbiyr kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alileta Takbiyr. Sikuleta Takbiyr wakati nilipoanza swalah. Nikakumbuka hilo ambapo nikaleta Takbiyr kwa ajili ya kutekeleza amri ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hili ni mosi.

Kuhusu kukariri Aayah, basi itambulike kuwa katika Sunnah – hili linahusiana na swalah za Nawaafil peke yake – ni mtu akariri Aayah ambazo anaona kuwa katika kuzikariri kunaleta unyenyekevu katika moyo wake. Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliswali swalah ya usiku na akafika katika Aayah hii:

إِن تُعَذِّبْهُمْ فَإِنَّهُمْ عِبَادُكَ ۖ وَإِن تَغْفِرْ لَهُمْ فَإِنَّكَ أَنتَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ

“Ukiwaadhibu, basi hao ni waja Wako na kuwasaemehe basi hakika Wewe ni Mwenye nguvu kabisa asiyeshindika, Mwenye hekima.”[1]

akaikariri mpaka asubuhi ilihali yuko ndani ya swalah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Jengine huenda baadhi yao wamesikia ninapofika katika Aayah ya Tasbiyh, du´aa au Isti´aadhah, basi ninaleta Tasbiyh, naomba du´aa na kuomba kinga. Kwa sababu hili pia ni jambo limewekwa katika Shari´ah katika swalah ya usiku katika swalah ya Naafilah. Ama katika swalah ya faradhi, basi itambulike kuwa wanachuoni wana kanuni inayosema:

“Yaliyothibiti juu ya swalah ya Naafilah yanathibiti pia katika faradhi.”

Kujengea juu ya kanuni hii ambayo imefahamishwa vilevile na Sunnah, tunasema hata katika swalah ya faradhi ukipita katika Aayah ambayo kuikariri kwake kunaleta unyenyekevu basi ikariri. Lakini kinachonizuia kufanya hivo ni kwamba wale walioisifia namna ya swalah ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya faradhi hawakuyanukuu hayo kutoka kwake. Kwa ajili hiyo tunasema katika swalah ya faradhi inafaa kufanya hivo. Kuhusu katika swalah ya Naafilah imependekezwa.

[1] 05:118

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa’ ash-Shahriy (49) http://binothaimeen.net/content/1113
  • Imechapishwa: 06/06/2020