Swali: Ni ipi hukumu ya Bid´ah? Je, katika Uislamu kuna Bid´ah nzuri?

Jibu: Bid´ah ni haramu. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Nakutahadharisheni kutokana na Bid´ah, kwani hakika kila kilichozuliwa ni Bid´ah na kila Bid´ah ni upotofu.”[1]

Imekuja kwa an-Nasaa´iy:

“… na kila upotofu ni Motoni.”

Anas bin Maalik (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Allaah amezuia tawbah kwa kila mtu wa Bid´ah mpaka aiache Bid´ah yake.”[2]

Katika Uislamu hakuna Bid´ah nzuri. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Yeyote atakayezua katika jambo letu hili kile kisichokuwemo, atarudishiwa mwenyewe.”[3]

Imekuja katika tamko jengine:

“Yeyote anayefanya kitendo kisichoafikiana na amri yetu, atarudishiwa mwenyewe.”[4]

Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) amesema:

الْيَوْمَ أَكْمَلْتُ لَكُمْ دِينَكُمْ

”Leo Nimekukamilishieni dini yenu.”[5]

Wale wanaosema ipo Bid´ah nzuri wanajengea hoja kwa Hadiyth:

“Tulikuwa kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) mwanzoni mwa mchana wakati walipokuja watu waliokuwa uchi. Nguo zao zilikuwa za kuchanika na panga zao zilikuwa zimenolewa. Wengi wao walikuwa ni kutoka Mudhwar. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipoona ufakiri walionao sura yake ikabadilika. Akaingia kisha akatoka. Halafu akamwamrisha Bilaal aite kwa ajili ya swalah. Wakaswali na kuhubiri na kusoma:

يَا أَيُّهَا النَّاسُ اتَّقُوا رَبَّكُمُ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن نَّفْسٍ وَاحِدَةٍ وَخَلَقَ مِنْهَا زَوْجَهَا وَبَثَّ مِنْهُمَا رِجَالًا كَثِيرًا وَنِسَاءً ۚ وَاتَّقُوا اللَّـهَ الَّذِي تَسَاءَلُونَ بِهِ وَالْأَرْحَامَ ۚ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلَيْكُمْ رَقِيبًا

“Enyi watu! Mcheni Mola wenu ambaye Amekuumbeni kutokana na nafsi moja na akaumba kutoka humo mke wake na akaeneza kutoka hao wawili wanaume wengi na wanawake na mcheni Allaah Ambaye Kwake mnaombana na jamaa. Hakika Allaah amekuwa juu yenu Mwenye kuchunga.”[6]

na:

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّـهَ وَلْتَنظُرْ نَفْسٌ مَّا قَدَّمَتْ لِغَدٍۖ وَاتَّقُوا اللَّـهَ ۚ إِنَّ اللَّـهَ خَبِيرٌ بِمَا تَعْمَلُونَ

“Enyi mlioamini! Mcheni Allaah na nafsi itazame imetanguliza nini kwa ajili ya kesho na mcheni Allaah. Hakika Allaah ni Mjuzi kwa myatendayo.”[7]

Mtu anaweza kutoa swadaqah ya dinari, dirhamu, nguo, ngano hata kipande cha tende.” Mtu mmoja kutoka Answaar akaja na mfuko ambao ulikaribia kumshinda kuubeba. Watu wakaanza kuleta baada yake mpaka nikaona matuta mawili ya chakula na nguo. Uso wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ukanawiri. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:

“Atakayeweka katika Uislamu msingi mzuri basi atalipwa ujira wake na ujira wa yule atakayeufanya baada yake pasi na kupunguziwa chochote katika ujira wao. Na atakayeweka katika Uislamu msingi mbaya ataadhibiwa kwao na adhabu ya yule atakayeufanya pasi na kupunguziwa chochote katika adhabu zao.”[8]

Bwana aliyetajwa katika Hadiyth aliwahimiza watu kutoa swadaqah. Swadaqah ni jambo limewekwa katika Shari´ah na sio Bid´ah.

Wamejengea hoja kwa kukusanywa kwa Qur-aan, lakini huo ni usadikisho wa maneno Yake (Ta´ala):

إِنَّا نَحْنُ نَزَّلْنَا الذِّكْرَ وَإِنَّا لَهُ لَحَافِظُونَ

“Hakika Sisi Tumeteremsha Ukumbusho na hakika Sisi bila shaka ndio Tutakaoihifadhi!”[9]

Pengine wakatumia hoja kwa mambo mengine yaliyozuliwa, lakini hata hivyo sio hoja; dalili ni Qur-aan na Sunnah. Isitoshe napendekeza kusoma ”al-I´tiswaam” ya ash-Shaatwibiy, ”al-Bid´a wan-Nahiy ´anhaa” cha Muhammad bin Wadhdhwaah al-Andalusiy na chuo cha ”al-I´tiswaam” katika ”as-Swahiyh” ya al-Bukhaariy.

[1] Abu Daawuud (4607), at-Tirmidhiy (2676) na Ibn Maajah (34). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”al-Irwaa’” (2455).

[2] Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika “Swahiyh-ut-Targhiyb wat-Tarhiyb (54).

[3] Muslim (1718).

[4] al-Bukhaariy (2697).

[5] 5:3

[6] 4:1

[7] 59:18

[8] Muslim, an-Nasaa’iy, Ibn Maajah na at-Tirmidhiy kwa mukhtaswari. Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika “Swahiyh-ut-Targhiyb wat-Tarhiyb (61).

[9] 15:6

  • Muhusika: ´Allaamah Muqbil bin Haadiy al-Waadi´iy
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Qam´-ul-Mu´aanid, uk. 313-314
  • Imechapishwa: 20/05/2025