Swali 95: Je, inafaa kujitoa muhanga?

Jibu: Hujui uhai ni kitu gani? Ni kwa nini ujitoe muhanga[1]? Allaah (Jalla wa ´Alaa) anasema:

وَلاَ تَقْتُلُواْ أَنفُسَكُمْ إِنَّ اللّهَ كَانَ بِكُمْ رَحِيمًا وَمَن يَفْعَلْ ذَلِكَ عُدْوَانًا وَظُلْمًا فَسَوْفَ نُصْلِيهِ نَارًا وَكَانَ ذَلِكَ عَلَى اللّهِ يَسِيرًا

”Wala msiziue nafsi zenu. Hakika Allaah ni Mwenye kuwahurumia. Na atakayefanya hivyo kwa uadui na dhuluma, basi tutamwingiza Motoni – na hilo kwa Allaah ni jepesi mno.”[2]

Haijuzu kwa mtu kujiua. Bali anatakiwa kuihifadhi nafsi yake. Hata hivyo hilo halizuii yeye kupigana na kupambana katika njia ya Allaah hata kama atauliwa hali ya kuwa ni shahidi. Lakini haijuzu kujiua kwa makusudi. Katika kipindi cha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) baadhi ya vita alikuweko bwana mmoja shujaa anayepambana bega kwa bega akiwa na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Akaumia na watu wakamsifu kwa kusema ”laiti tungelifikia yale aliyofikia bwana fulani”. Ndipo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:

”Yuko Motoni.”

Hilo likawa gumu kwa Maswahabah wakijiuliza; ni vipi bwana huyu ambaye anapambana na hamsalimishi kafiri yeyote atakuwa Motoni? Hivyo mtu mmoja akamfuata na kumfuatilia na hatimaye akamuona akasimika upanga wake ardhini na kuuegemea ili ncha ipenyeze mwili wake na kumuua. Swahabah yule akasema:

”Amesema kweli Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).”[3]

Alijua kuwa Mtume hazungumzi kwa matamanio. Ni kwa nini aliingia Motoni kwa kitendo hichi? Kwa sababu alijiua na hakusubiri. Kwa hiyo haijuzu kwa mtu kujiua wala kusababisha kujiua.

[1] Muhaddith al-Albaaniy (Rahimahu Allaah) amesema:

”Mambo ya kujitoa muhanga ya leo yote hayakubaliwi na Shari´ah na na pia yote ni haramu. Pengine ikawa miongoni mwa zile aina ambazo zinamdumisha mwenye nayo Motoni milele na pengine iakwa ni miongoni mwa zile aina ambazo hazimdumishi mwenye nayo Motoni milele. Ama mtu huyu kufanya kitendo hichi kwa kutumia jina la Allaah na kwa ajili ya kuwalinda watu wake na nyumba yake, mambo haya ya kujitoa muhanga yanazingatiwa hayana lolote kabisa kuhusiana na Uislamu.” (al-Fataawaa al-Muhimmah fiy Tabswir-il-Ummah, uk. 76)

´Allaamah na Shaykh Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn (Rahimahu Allaah) amesema:

”Kuhusu yale yanayofanywa na baadhi ya watu kujitoa muhanga kwa njia ya kwamba anabeba vilipuzi na kusogea mbele ya makafiri kisha pale anapokuwa mbele yake anavilipua, huku kunahesabika ni kujiua – na ulinzi unaombwa kutoka kwa Allaah. Kwa mujibu wa Hadiyth ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yule mwenye kujiua atadumishwa Motoni milele. Kujitoa muhanga kwa mtu huyo hakuleti manufaa yoyote juu ya Uislamu.” (al-Fataawaa al-Muhimmah fiy Tabswir-il-Ummah, uk. 76)

[2] 4:29-30

[3] al-Bukhaariy (2742) na (3966).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Ajwibah al-Mufiydah ´an As-ilat-il-Manaahij al-Jadiydah, uk. 227-228
  • Imechapishwa: 06/08/2024
  • taaliki: Shaykh Jamaal bin Furahyaan al-Haarithiy