Upamoja huu unaokuwepo kwa mwenye kufanya Dhikr ni hali ambayo hakuna kitu kinachofanana nayo. Ni upamoja maalum zaidi kuliko ule anaokuwa nao mwenye kufanya wema na mchamungu. Ni upamoja ambao hauwezi kuelezeka wala kufikiwa na sifa. Bali hujulikana kwa ladha. Hii ni sehemu hatarishi kwa mtu endapo mja hawezi kupambanua baina ya cha kale na kilichozuka, baina ya Mola na mja, baina ya Muumba na kiumbe, baina ya mfanya ´ibaadah na mwabudiwa. Bila ya uwezo huu wa kupambanua atatutumbukia ndani ya imani ya kuona kuwa Allaah amekita ndani ya kila kiumbe inayofanana na ya manaswara, au atatumbukia ndani ya imani ya kuona kuwa mja na Mola ni kitu kimoja inayofanana na wale wenye imani hiyo. ´Aqiydah yao ni kwamba uwepo wa Muumba ni sawa na uwepo wa viumbe vyote hivi. Kwa mujibu wao wanaona kuwa hakuna Mola na mja, au wa Haki na kiumbe. Bali, wanaona kuwa Mola ndiye mja na mja ndiye Mola, na kwa mujibu wao wanaona kuwa kiumbe anayefananishwa pia ndiye wa Haki anayetakaswa kutokana na mapungufu yote. Makusudio hapa ni kuwa ikiwa mja hatokuwa na ´Aqiydah sahihi na pia akatawaliwa na Dhikr, kwa namna ya kwamba akapoteza utambuzi wa yule anayemtaja, Dhikr yake na nafsi yake, basi hapana shaka yoyote kwamba ataingia katika imani ya kuona kuwa Allaah amekita ndani ya kila kiumbe na kwamba Allaah na kiumbe ni kitu kimoja.

  • Muhusika: Imaam Shams-ud-Diyn Muhammad bin Abiy Bakr bin Qayyim-il-Jawziyyah (afk. 751)
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Waabil as-Swayyib wa Raafi´-ul-Kalim at-Twayyib, uk. 158
  • Imechapishwa: 03/09/2025