Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah amesema:

Hadiyth ya mbuzi inasema:

“Juu ya mbingu ya saba kuna bahari ambayo kufika mpaka chini ni sawa na umbali wa kutoka mbingu moja hadi nyingine. Juu yake kuna mbuzi wanane. Umbali kati visigino na magoti yavyo ni sawa na umbali wa kutoka mbingu moja hadi nyingine. Migongoni mwao ndiko kuna ´Arshi ambapo kutokea chini yake mpaka juu yake ni sawa na umbali wa kutoka mbingu moja hadi nyingine. Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) yuko juu yake.”[1]

Hadiyth hii licha ya kwamba imepokelewa Abu Daawuud, Ibn Maajah na at-Tirmidhiy, imepokelewa vilevile kupitia njia mbili zinazotambulika. Kuitia dosari njia moja wapo hakuitii dosari njia nyingine. Imamu wa maimamu Ibn Khuzaymah ameipokea katika kitabu chake “at-Tawhiyd” ambacho ameshurutisha kuwa hatonukuu ndani yake isipokuwa tu zile Hadiyth ambazo zimepokelewa kutoka kwa waadilifu hali ya kuungana cheni ya wapokezi kwenda mpaka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

MAELEZO

Shaykh na Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) ameitaja Hadiyth hii mwishoni mwa ”Kitaab-ut-Tawhiyd”. Ni Hadiyth iliyosimuliwa na al-´Abbaas bin ´Abdil-Muttwalib (Radhiya Allaahu ´anh). Humo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ameeleza uumbaji wa mbingu na ardhi na yale masafa marefu yaliyo kati yake, kwamba baadhi ya mbingu saba ziko juu ya zingine, mbingu iliyo juu kabisa juu yake kuna bahari, kwamba juu ya bahari kuna Kursiy iliyozizunguka mbingu na ardhi, kwamba juu ya Kursiy kuna ´Arshi – ambayo ndio kiumbe kikubwa zaidi – iliyowazunguka viumbe wote na kwamba Allaah yuko juu ya ´Arshi. Hili la mwisho ndio kinachokusudiwa katika Hadiyth. Inathibitisha kuwa Allaah yuko juu ya mbingu na juu ya viumbe wote. Hivyo kunathibitishwa ujuu wa Allaah (´Azza wa Jall).

[1] Ahmad (1/206), Abu Daawuud (4723), at-Tirmidhiy (3320) ambaye amesema ni nzuri na geni, Ibn Maajah (193), Ibn Khuzaymah katika ”at-Tawhiyd”, uk. 100-102, Ibn Abiy ´Aaswim (577) na ad-Daarimiy katika ”ar-Radd ´alaal-Jahmiyyah”, uk. 19. Nzuri na Swahiyh kwa mujibu wa Ibn-ul-Qayyim katika ”Ijtimaa´-ul-Juyuush al-Islaamiyyah”, uk, 87, na dhaifu kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Dhwilaal-ul-Jannah” (577).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaa al-Hamawiyyah, uk. 124-125
  • Imechapishwa: 25/08/2024