Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah amesema:

Hadiyth ya matabano inasema:

“Yule ambaye atahisi maumivu mmoja wenu, au akahisi maumivu ndugu yake, aseme: “Mola wetu ni Allaah ambaye yuko mbinguni. Limetakasika jina Lako. Amri Yako iko mbinguni na ardhini kama ambavyo huruma Yako iko mbinguni. Tusamehe madhambi na makosa yetu. Wewe ni Mola wa wazuri. Teremsha rehema Yako na dawa Yako kwa huyu anayehisi maumivu.” ili aweze kupona.”[1]

MAELEZO

Matabano ni kumsomea Qur-aan au du´aa zilizowekwa katika Shari´ah mgonjwa, na ni sababu inayopelekea kupona kwa idhini ya Allaah. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alifanya matabano na yeye mwenyewe alifanyiwa matabano na Malaika. Miongoni mwa mambo ambayo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alifanya nayo matabano ni Hadiyth hii:

“Mola wetu ni Allaah ambaye yuko mbinguni… “

Kipande hichi ndicho kinacholengwa katika Hadiyth kwa sababu amemweleza Mola wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba yuko juu ya mbingu. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Amri Yako iko mbinguni na ardhini… “

Amri ya Allaah (Jalla wa ´Alaa) iko mbinguni na ardhini. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Teremsha rehema Yako na dawa Yako kwa huyu anayehisi maumivu.”

Hii ni dalili nyingine inayofahamisha kuwa juu kwa Allaah, kwa sababu kushuka inakuwa kutokea kwa juu. Hadiyth mosi inathibitisha kuwa Allaah yuko juu ya mbingu, na pili Yeye ndiye ambaye anashusha dawa. Kama alivosema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

”Allaah hakuteremsha maradhi isipokuwa pia ameteremsha dawa yake; mwenye kuijua ameijua, na ambaye hakuijua hakuijua.”[2]

[1] Abu Daawuud (3892), an-Nasaa’iy (10877) na al-Haakim (1/344). Dhaifu kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Dhwa´iyf Sunan Abiy Daawuud” (3892).

[2] al-Bukhaariy (5678), Ahmad (1/377), Ibn Hibbaan (6062) na al-Haakim (4/218).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaa al-Hamawiyyah, uk. 122-123
  • Imechapishwa: 25/08/2024