Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah amesema:

يَا عِيسَى إِنِّي مُتَوَفِّيكَ وَرَافِعُكَ إِلَيَّ

“Ee ‘Iysaa! Hakika Mimi ni Mwenye kukuchukua na Mwenye kukupandisha Kwangu.”[1]

MAELEZO

Wakati walimfanyia njama za kumuua al-Masiyh (´alayhis-Salaam), Allaah alimwambia:

يَا عِيسَى إِنِّي مُتَوَفِّيكَ وَرَافِعُكَ إِلَيَّ

“Ee ‘Iysaa! Hakika Mimi ni Mwenye kukuchukua na Mwenye kukupandisha Kwangu.”

Allaah alimpandisha kutoka kati yao na hawakuhisi hilo. Kama ambavo Allaah alimtoa nje Muhammad kutoka kati ya washirikina wakati alipotaka kuhajiri. Akatoka kati yao walipokuwa wanamsubiri atoke nje ili wamuue. Hawakumuhisi (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hivyo yeye na Abu Bakr wakaenda katika pango la Thawr ambapo alijificha. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَإِذْ يَمْكُرُ بِكَ الَّذِينَ كَفَرُوا لِيُثْبِتُوكَ أَوْ يَقْتُلُوكَ أَوْ يُخْرِجُوكَ ۚ وَيَمْكُرُونَ وَيَمْكُرُ اللَّـهُ ۖ وَاللَّـهُ خَيْرُ الْمَاكِرِينَ

“Pindi walipokupangia vitimbi wale waliokufuru ili wakufunge, au wakuue, au wakutoe [nje ya Makkah]. Na wanapanga vitimbi na Allaah anapanga vitimbi; na Allaah ni mbora wa wenye kupanga vitimbi.”[2]

Vivyo hivyo Allaah akamuokoa al-Masiyh kati ya mayahudi pasi na wao kuhisi, na akamnyanyua Kwake. Allaah (Ta´ala) amesema:

إِنِّي مُتَوَفِّيكَ

“Mimi ni Mwenye kukuchukua… “

Kipo kinachokusudiwa hapa ni aina fulani ya usingizi. Ni kama maneno Yake (Ta´ala):

وَهُوَ الَّذِي يَتَوَفَّاكُم بِاللَّيْلِ وَيَعْلَمُ مَا جَرَحْتُم بِالنَّهَارِ ثُمَّ يَبْعَثُكُمْ فِيهِ لِيُقْضَىٰ أَجَلٌ مُّسَمًّى ۖ ثُمَّ إِلَيْهِ مَرْجِعُكُمْ ثُمَّ يُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ

“Naye ndiye anayekufisheni usiku na anajua yale myafanyayo mchana halafu anakufufueni humo ili utimizwe muda maalum uliokadiriwa. Kisha Kwake pekee ni marejeo yenu, kisha atakujulisheni kuhusu yale mliyokuwa mkiyatenda.”[3]

Usingizi ni kifo. al-Masiyh (´alayhis-Salaam) alipatwa na hali ya usingizi. Hakufa. Alipandishwa juu mbinguni akiwa hai, na katika zama za mwisho atashuka chini, kama ilivyopokelewa kwa mapokezi mengi katika Hadiyth na kama ilivyo katika Qur-aan:

وَإِن مِّنْ أَهْلِ الْكِتَابِ إِلَّا لَيُؤْمِنَنَّ بِهِ قَبْلَ مَوْتِهِ ۖ وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ يَكُونُ عَلَيْهِمْ شَهِيدًا

“Hakuna yeyote katika Ahl-ul-Kitaab isipokuwa atamwamini kabla ya kufa kwake na siku ya Qiyaamah atakuwa shahidi juu yao.”[4]

Kinacholengwa ni pale Allaah aliposema:

وَرَافِعُكَ إِلَيَّ

“… na Mwenye kukupandisha Kwangu.”

Kupandishwa inakuwa maeneo ya juu. Kwa hivyo hilo likafahamisha kuwa Allaah (Ta´ala) yuko juu ya viumbe.

[1] 3:55

[2] 8:30

[3] 6:60

[4] 4:159

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaaa al-Hamawiyyah, uk. 109-110
  • Imechapishwa: 19/08/2024