65. Shubuha nne kubwa za washirikina waliokuja nyuma

Ukihakikisha ya kwamba wale aliyowapiga vita Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) walikuwa na akili nzuri na shirki kidogo kuliko watu hawa[1], basi jua kuwa hawa wana shubuha wanazozitaja kwa tulioyataja, na ni katika shubuha zao kubwa, hivyo sikiliza vizuri majibu yake. Wanasema: “Wale ambao Qur-aan iliwateremkia walikuwa hawashuhudii ya kwamba hapana mungu isipokuwa Allaah, walikuwa wanamkadhibisha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), wanapinga kufufuliwa na wanakadhibisha Qur-aan na kuiona kuwa ni uchawi. Ama sisi tunashuhudia hapana mungu isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Mtume wa Allaah, na tunaisadikisha Qur-aan, na tunaamini kufufuliwa, tunaswali na tunafunga. Vipi basi mtatufanya sisi ni kama wao?”

Jibu ni: “Hakuna tofauti baina ya wanachuoni wote, ya kwamba mtu akimsadikisha Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika kitu na akamkadhibisha katika kitu kingine, ni kafiri ambaye hakuingia katika Uislamu. Hali kadhalika [ni kafiri] iwapo ataamini baadhi ya Qur-aan na akapinga baadhi yake nyingine, kama mwenye kukubali Tawhiyd na akapinga uwajibu wa swalah, au akakubali Tawhiyd na swalah na akakadhibisha uwajibu wa zakaah, au akakubali yote haya na akakadhibisha uwajibu wa swawm, au akakubali yote haya na akakadhibisha uwajibu wa hajj. Katika zama za Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wakati watu hawakujisalimisha juu ya hajj, Allah aliteremsha kuhusu wao:

وَلِلَّـهِ عَلَى النَّاسِ حِجُّ الْبَيْتِ مَنِ اسْتَطَاعَ إِلَيْهِ سَبِيلً ¤ وَمَن كَفَرَ فَإِنَّ اللَّـهَ غَنِيٌّ عَنِ الْعَالَمِينَ ا

”Na kwa ajili ya Allaah ni wajibu kwa watu watekeleze Hajj katika Nyumba hiyo kwa mwenye uwezo wa kuiendea. Na atakayekanusha, basi hakika Allaah ni Mkwasi kwa walimwengu.” (Aal ´Imraan 03 : 97)

Na mwenye kukubali yote haya na akakadhibisha kufufuliwa, anakufuru kwa maafikiano na ni halali damu yake na mali yake. Kama alivyosema (Ta´ala):

إِنَّ الَّذِينَ يَكْفُرُونَ بِاللَّـهِ وَرُسُلِهِ وَيُرِيدُونَ أَن يُفَرِّقُوا بَيْنَ اللَّـهِ وَرُسُلِهِ وَيَقُولُونَ نُؤْمِنُ بِبَعْضٍ وَنَكْفُرُ بِبَعْضٍ وَيُرِيدُونَ أَن يَتَّخِذُوا بَيْنَ ذَٰلِكَ سَبِيلًا أُولَـٰئِكَ هُمُ الْكَافِرُونَ حَقًّا

”Hakika wale wanaomkufuru Allaah na Mitume Yake na wanataka kufarikisha baina ya Allaah na Mitume Wake na wanasema: “Tunaamini baadhi na tunawakanusha baadhi” na wanataka kuchukua njia iliyo kati ya hayo – hao ndio makafiri wa kweli.” (an-Nisaa´ 04 : 150-151)

Ikiwa Allaah ameweka wazi katika Kitabu Chake ya kwamba mwenye kuamini baadhi na akakufuru baadhi, basi ni kafiri wa kweli na kwamba anastahiki alichokitaja, shubuha hii itakuwa imeondoka. Na hiki ni kitu walichosema watu kutoka al-Ahsaa´ katika kitabu chao walichotutumia. Mtu anaweza kusema pia: “Ikiwa unakubali ya kwamba mwenye kumsadikisha Mtume katika kila kitu na akakadhibisha uwajibu wa swalah, ni kafiri ambaye ni halali damu yake kwa maafikiano, hali kadhalika akikubali kila kitu isipokuwa kufufuliwa, hali kadhalika lau atakadhibisha uwajibu wa kufunga swawm ya Ramadhaan, hakanushi isipokuwa haya ilihali mengine yote anayasadikisha – madhehebu mbalimbali wamekubaliana kwa hili na Qur-aan imeliongelea kama tulivyosema – mtu atafahamu ya kwamba Tawhiyd ndio faradhi kubwa aliyokuja nayo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na ni kubwa kuliko swalah, zakaah, swawm na hajj. Vipi itakuwa mtu akikadhibisha kitu katika mambo haya anakufuru – hata kama atayafanyia kazi mambo yote aliyokuja nayo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) – na akikadhibisha Tawhiyd ambayo ndio dini ya Mitume wote asikufuru?” Ametakasika Allaah! Ni ajabu ilioje ya ujinga huu.

Mtu anaweza kusema pia: “Maswahabah wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) waliwapiga vita na Banuu Haniyfah, ilihali walikuwa Waislamu pamoja na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wao wanashuhudia ya kwamba hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Mtume wa Allaah, walikuwa wakiadhini na wakiswali.” Akisema: “Walisema: “Musaylamah ni Mtume”, mwambie: “Hili ndilo lililokuwa linatakikana. Ikiwa yule anayempandisha mtu katika daraja ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anakufuru na mali yake inakuwa halali na damu yake, na wala haimfai kitu Shahaadah zake mbili wala swalah, vipi kwa yule mwenye kumpandisha Shamsaan, Yuusuf, Swahabah au Mtume katika daraja ya al-Jabbaar wa mbingu na ardhi? Ametakasika Allaah! Ni Ukubwa ulioje alonao.

كَذَٰلِكَ يَطْبَعُ اللَّـهُ عَلَىٰ قُلُوبِ الَّذِينَ لَا يَعْلَمُونَ

”Hivyo ndivyo Allaah anavyopiga muhuri juu ya nyoyo za wale wasiojua.” (ar-Ruum 30 : 59)

Yaweza kusemwa pia: “Wale ambao ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) aliwaua kwa kuwaunguza moto, wote walikuwa wakidai Uislamu. Walikuwa ni katika wafuasi wa ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) na walisoma elimu kutoka kwa Maswahabah, lakini walimuamini ´Aliy kama ilivyokuwa inaaminiwa kwa Yuusuf, Shamsaan na mfano wao. Vipi walikubaliana Maswahabah kuwapiga vita na kuwaona kuwa ni makafiri? Je, unaafikiri ya kwamba Maswahabah wanawakufurisha Waislamu au mnadhani ya kwamba kuwa na imani kwa Taaj na mfano wake haidhuru na kuwa na imani kwa ´Aliy bin Abiy Twaalib ndio kunakufurisha?”

Yaweza kusemwa pia: “Banuu ´Ubayd al-Qaddaah, waliokuwa wanamiliki Magharibi na Misri katika zama za Banuu al-´Abbaas, wote walikuwa wakishuhudia hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Mtume wa Allaah, walikuwa wakidai Uislamu, wakiswali swalah ya ijumaa na ya mkusanyiko. Ilipodhihiri kukhalifu kwao Shari´ah katika mambo duni ya tuliyomo, walikubaliana wanachuoni kwamba ni makafiri na kwamba inatakiwa kuwapiga vita na kwamba miji yao ni miji ya vita. Hivyo Waislamu wakawashambulia mpaka wakaokoa waliokuwa nayo katika miji ya Waislamu.”

Yaweza kusemwa pia: “Ikiwa watu wa mwanzo hawakukufuru, isipokuwa kwa kujumuisha kwao baina ya shirki na kumkadhibisha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Qur-aan na kupinga kufufuliwa na kadhalika, ni nini maana ya mlango uliotajwa na wanachuoni wa kila madhehebu “Mlango: Hukumu ya mwenye kuritadi”, naye ni yule Muislamu ambaye anakufuru baada ya Uislamu wake? Halafu wakataja aina nyingi; kila aina inakufurisha na kuhalalisha damu ya mtu na mali yake. Mpaka walitaja mambo ambayo yalionekana ni madogo kwa yule mwenye kuyafanya, kama mfano maneno yaliosemwa na mdomo wake bila ya kuyamaanisha moyoni mwake au maneno aliyosema kwa njia ya mzaha na mchezo.

Yaweza kusemwa pia: “Wale ambao Allaah amesema juu yao:

يَحْلِفُونَ بِاللَّـهِ مَا قَالُوا وَلَقَدْ قَالُوا كَلِمَةَ الْكُفْرِ وَكَفَرُوا بَعْدَ إِسْلَامِهِمْ

”Wanaapa kwa jina la Allaah kwamba hawakusema [maneno maovu]; ilihali wamesema neno la kufuru na wakakufuru baada ya Uislamu wao.” (at-Tawbah 09 : 74)

hamkusikia ya kwamba Allaah amewakufurisha kwa maneno yao, pamoja na kuwa walikuwa katika zama za Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), wakipigana Jihaad bega kwa bega pamoja naye, wakiswali pamoja naye, wakitoa zakaah pamoja naye, wakihiji na wakimpwekesha Allaah? Hali kadhalika wale ambao Allaah Kasema kuwahusu:

قُلْ أَبِاللَّـهِ وَآيَاتِهِ وَرَسُولِهِ كُنتُمْ تَسْتَهْزِئُونَ لَا تَعْتَذِرُوا قَدْ كَفَرْتُم بَعْدَ إِيمَانِكُمْ

“Sema: Je, mlikuwa mnamfanyia istihizai Allaah na Aayah Zake na Mtume Wake?” Msitoe udhuru! Mmekwishakufuru baada ya kuamini kwenu.”” (at-Tawbah 09 : 65-66)

Watu hawa ambao Allaah kaweka wazi ya kwamba wamekufuru baada ya kuamini kwao – pamoja na kuwa wako na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika vita vya Tabuuk – walisema maneno ambayo walisema kuwa waliyasema kwa mzaha tu. Fikiria shubuha hii, nayo ni kauli yao: “Je, mnawakufurisha Waislamu ambao wanashuhudia hapana mungu isipokuwa Allaah, wanaswali na wanafunga”. Kisha fikiria jibu lake. Kwa hakika ni katika yamanufaa yaliyomo kwenye waraka hii.

Na katika dalili ya hayo pia ni yale Allaah (Ta´ala) aliyosema kuhusu Banuu Israaiyl –pamoja na Uislamu wao, elimu yao na wema wao – walimwambia Muusa: “Tufanyie mungu kama wao walivyo na waungu”. Hali kadhalika walisema baadhi ya Maswahabah: “Tujaalie Dhaat Anwaatw”. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akaapa ya kwamba hii inakumbusha kauli ya Banuu Israaiyl: “Tufanyie mungu”.

MAELEZO

Shaykh (Rahimahu Allaah) bado anaendelea kuraddi shubuha za watatizi katika masuala ya shirki na Tawhiyd. Ameishia katika utata huu mkubwa ambao ndio katika utata wao mkubwa na ambao ni khatari zaidi. Si nyingine isipokuwa ni yale maneno yao kwamba mwenye kushuhudia ya kwamba hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Mtume wa Allaah, akaswali, akafunga, akahiji na akatekeleza matendo mengine hawezi kukufuru. Haijalishi kitu yale mambo mbalimbali atayofanya yanayomritadisha mtu.

Ama wale washirikina wa mwanzo ambao Qur-aan imeteremka kuwahusu hawa sio kama hao wengine. Hawakushuhudia ya kwamba hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Mtume wa Allaah. Kwa msemo mwingine hawakuingia katika Uislamu. Hawakuwa wakimuamini Allaah, Mtume, Uislamu wala Qur-aan. Kuhusu hawa wengine wanadhihirisha kuamini kufufuliwa, wanaswali, wanafunga, wanahiji, wanatoa zakaah, wanamdhukuru Allaah kwa wingi. Shaykh (Rahimahu Allaah) khaswa katika mnasaba wa utata huu amesema:

“Sikiliza majibu yake. Kwani ndio utata mkubwa walionao.”

[1] Washirikina wa leo.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 99
  • Imechapishwa: 06/02/2017