66- Mtawala au naibu wake ana haki zaidi ya uimamu juu ya swalah ya jeneza kuliko ndugu yake. Hilo ni kutokana na Hadiyth ya Abu Haazim ambaye ameeleza:

“Hakika nilishuhudia wakati alipofariki al-Hasan bin ´Aliy. Nilimwona al-Husayn bin ´Aliy akimwambia Sa´iyd bin al-´Aasw – akimgusa shingoni mwake na akimwambia – Tangulia mbele. Kama isingelikuwa Sunnah basi nisingelikutanguliza wewe. [Kipindi hicho Sa´iyd ndiye alikuwa mkuu wa mkoa wa al-Madiynah[1]] na kati yao kulikuwa na kitu.”

Ameipokea al-Haakim (03/171), al-Bazzaaz (714 – Kashf-us-Sattaar), at-Twabaraaniy katika “al-Mu´jam-ul-Kabiyr” (03/148/2912, 2913), al-Bayhaqiy (04/28) ambaye amezidisha mwishoni mwake:

“Abu Hurayrah akasema: “Mnashindana juu ya mtoto wa Mtume wenu kwa sababu tu ya udongo mtaomfunika juu yake. Hakika mimi nimemsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akisema:

“Yule atakayewapenda wawili hao, basi hakika amenipenda. Na yule atakayewachukia wawili hao, basi hakika amenichukia.”

Vilevile ameitoa Ahmad (02/431) pia kwa ziada hii. Lakini hata hivyo hakutaja kisa cha kutangulizwa kwa Sa´iyd kuswalisha. Bali yeye amekiashiria kwa kusema: “Akataja kisa.” Kisha al-Haakim akasema:

“Ni yenye mlolongo wa wapokezi Swahiyh.” adh-Dhahabiy ameafikiana naye.

al-Haythamiy amepokea kisa hicho katika “al-Mujma´” (03/31) kwa ukamilifu wake pamoja na ziada. Kisha akasema:

“Wapokezi wake ni wenye kuaminiwa.”

 al-Haafidhw katika “at-Talkhiysw” (05/275) amekiegemeza kwa wawili hao akiwemo al-Bayhaqiy pia na akasema:

“Ndani yake yumo Saalim bin Hafswah ambaye ni dhaifu. Lakini kaitoa an-Nasaa´iy na Ibn Maajah kwa mtazamo mwingine kutoka kwa Abu Haazim kwa mfano wa hiyo. Ibn-ul-Mundhiriy amesema katika “al-Awsatw”:

“Katika masuala haya hakuna ambayo iko juu kuliko hii. Kwa sababu jeneza la al-Hasan walihudhuria watu wengi katika Maswahabah na wengineo.”

Haya ndio maneno ya al-Haafidhw. Katika baadhi ya maneno hayo yanahitaji kujadiliwa. Hilo linakuwa kwa njia mbili:

Ya kwanza: Maneno yake kwamba Ibn Abiy Hafswah ni dhaifu yanapingana na yale aliyosema katika wasifu wake katika “at-Taqriyb”:

“Ni mkweli. Isipokuwa tu ni Shiy´iy mwenye kupindukia.”

Akiwa ni mkweli basi Hadiyth yake chinichini inakuwa na daraja ya uzuri. Kitendo chake cha yeye kuwa ni Shiy´iy hakidhuru kama ilivyothibiti katika elimu ya Hadiyth. Hadiyth hii inatiliwa nguvu na kitendo cha al-Bayhaqiy kuitoa katika upokezi wake yeye kupitia kwa njia ya Ismaa´iyl bin Rajaa´ az-Zubaydiy ambaye amesema:

“Amenipa khabari mimi yule aliyemuona al-Husayn bin ´Aliy wakati alipokufa… “

Akaitaja Hadiyth kwa ufupi. Pia katika maneno ya al-Husayn bin Sa´iyd alipomwambia:

“Tangulia mbele. Kama isingelikuwa Sunnah basi nisingelikutanguliza wewe.”

Ismaa´iyl huyu ni mwaminifu. Ibn Abiy Hafswah amemfuata. Hakika ni ufuatiliaji wenye nguvu hata kama hakumtaja ndani yake ambaye alishuhudilia kisa hicho. Kama ulivyoona Saalim amemtaja na wengineo pia, kama ambavo maneno ya al-Haafidhw yameashiria hivo:

“Lakini kaitoa an-Nasaa´iy, Ibn Maajah… “

Lakini kuna yale yatayokuja huko mbele:

Ya pili: Mimi sijaiona Hadiyth katika “al-Janaa-iz” kutoka katika Sunan ya an-Nasaa´iy na Ibn Maajah. Wala al-Mizziy hajaitaja katika “Tuhfat-ul-Ashraaf” wala an-Naabulusiy katika “adh-Dhakhaa-ir” katika Hadiyth zinazomuhusu al-Husayn wala katika Hadiyth zinazomuhusu al-Hasan. Allaah ndiye mjuzi zaidi.

Ibn Hazm ametaja kisa hichi katika “al-Muhallaa” (05/144) kwa njia ya kukipitisha na wala hakukidhoofisha. Pamoja na kwamba yeye hakuchukua ile hukumu inayojulishwa nacho. Amesema:

“Tumesema: “Hatujadai kwenu nyinyi kuwepo kwa maafikiano mpaka mnatupinga kwa hili. Lakini wanapovutana maimamu basi ni lazima kurejea katika Qur-aan na Sunnah. Na katika Qur-aan na Sunnah yapo yale tuliyoyataja.”

Ni kama vile Ibn Hazm (Rahimahu Allaah) haoni pale Swahabah anaposema “Sunnah ni kufanya hivi” kwamba hukumu yake ni kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), jambo ambalo linakwenda kinyume na kile kilichothitihswa na wanachuoni wa misingi. Kwa sababu jambo hilo lina hukumu ya kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na ndio maoni ya sawa – Allaah (Ta´ala) akitaka. Ubainifu zaidi wa hayo utakuja katika masuala ya 73.

Kuhusu yale aliyoashiria Ibn Hazm kutoka katika “Qur-aan na Sunnah” anachomaanisha ni maneno Yake (Ta´ala):

“wa ulul arhami…fi kitaab”

Pia maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika Hadiyth inayokuja katika masuala yanayofuata:

“Wala mtu asimwongoze mwengine kabisa katika jamaa zake.”

Kama ilivyopokelewa katika upokezi. Ibn Hazm ameitumia kama hoja juu ya kwamba mtu ambaye ana haki zaidi juu ya maiti ni wale nduguze. Ni jambo lisilofichika kwamba ametumia dalili kwa maandiko yaliyokuja kwa njia ya ujumla. Sisi dalili yetu, ambayo ni ile Hadiyth ya al-Husayn (Radhiya Allaahu ´anhumaa), yenyewe ni maalum ambayo ndio yenye kutangulizwa kama ilivyopitishwa katika misingi. Ndio maana jopo la wanachuoni wengi wakaonelea yale tuliyoyataja. Miongoni mwao ni Abu Haniyfah, Maalik, Ahmad, Ishaaq, Ibn-ul-Mundhir na ash-Shaafi´iy katika maneno yake ya zamani kama ilivyo katika “al-Majmuu´” (05/217).

Kisha nikadiriki jambo na kusema: hakika ile Hadiyth ambayo Ibn Hazm ameitumia kama hoja haina ueneaji wowote katika yale ambayo sisi tunzunagumzia. Kwa sababu maana yake ni kwamba haifai kabisa kwa yeyote kuwaongoza watu kama imamu kumswalisha baba mwenye nyumba nyumbani kwake, jambo ambalo liko katika mkusanyiko wa mapokezi ya Hadiyth. Katika upokezi wa Muslim imekuja:

“Wala mtu asimwongoze mwengine kabisa katika utawala wake.”

Nyingine yake imekuja:

“Wala mtu asimwongoze mwengine kabisa katika jamaa zake na wala katika utawala wake.”

Hii ni hoja dhidi ya Ibn Hazm. Kwa sababu udhahiri ni kwamba mkusudiwa ni mtawala ambaye anayatawalia mambo ya watu. Udhahiri pia ni kwamba ndiye anayetangulizwa mbele ya mwengine yeyote ijapokuwa huyo mwengine ana Qur-aan nyingi kumliko. Tazama “ash-Shawkaaniy” (03/134).

[1] Alimuona Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alifishwa akiwa na miaka tisa. Alikuwa mpole na mwenye heshima. Alikuwa miongoni mwa Quraysh bora na mmoja katika wale walioandika msahafu wa ´Uthmaan. Alimpa utawala huko Kuufah. Aliwapiga watu vita Tabaristan na Mu´aawiyah akampa utawala al-al-Madiynah. Alifariki katika jumba lake la kifalme huko ´Araswah ambalo ni maili tatu kutokea hapo al-Madiynah mwaka wa 58 ambapo akazikwa al-Baqiy´.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Janaa-iz wa Bid´ahaa, uk. 128-131
  • Imechapishwa: 17/08/2020