Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Miaka kumi alilingania katika Tawhiyd. Baada ya miaka kumi alipandishwa mbinguni na akafaradhishiwa juu yake swalah tano kwa siku. Aliswali Makkah kwa miaka mitatu. Baada yake akaamrishwa kufanya Hijrah kwenda al-Madiynah.

MAELEZO

Miaka kumi alilingania katika Tawhiyd na akitahadharisha shirki. Akiwaamrisha watu kuacha kumuabudu asiyekuwa Allaah (Subhaanah) na kumtakasia ´ibaadah Allaah pekee katika du´aa, nadhiri, vichijnjwa na mambo yao mengine.

Baada ya hapo akapandishwa mbinguni akiwa pamoja na Jibriyl (Swalla Allaahu ´alayhimaa wa sallam). Akafunguliwa mbingu mpaka akaweza kupanda juu ya mbingu ya saba na akasikia kalamu zikiandika. Kisha akaitwa na Allaah (Jalla wa ´Alaa), akamuongelesha na akamfaradhishia swalah tano. Mwanzoni kulifaradhishwa swalah 50, kisha hakuacha kuomba kupunguziwa mpaka Allaah akazifanya kuwa tano. Allaah (Subhaanah) akamweleza kuwa ni swalah tano kiidadi lakini kunaandikwa 50 katika Ubao uliohifadhiwa. Atakayezihifadhi hizo swalah tano Allaah atamwandikiwa ujira wa swalah 50. Kila tendo jema moja linalipwa mara kumi mfano wake. Ndipo (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akateremka na amri hiyo. Swalah zilitakiwa kuswaliwa mara tano mchana na usiku; Dhuhr, ´Aswr, Maghrib, ´Ishaa na Fajr. Akaziswali miaka mitatu Makkah kabla hajahajiri.

Kwa vile Quraysh walikuwa wakimuudhi zaidi na zaidi yeye (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah wake, akahajiri kwenda al-Madiynah. Allaah akampa idhini ya kutoka Makkah kwenda al-Madiynah na kwa Answaar ili kuyaepuka maudhi na dhuluma ya Quraysh. Katika mnasaba wa hajj Answaar (Radhiya Allaahu ´anhum) walimpa kiapo juu ya kuhamia kwao na kumnusuru. Kilipotimia kiapo ndipo Allaah akamruhusu kuhamia kwao. Kabla ya hapo kuna baadhi ya Maswahabah wake walikuwa tayari wameshahajiri kwenda Uhabeshi na wakaishi kwa an-Najaashiy kwa muda fulani. Muda ulivyokuwa ukienda na wao pia wakahamia al-Madiynah ambapo wakatulizana huko na himdi zote anastahiki Allaah.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 49-50
  • Imechapishwa: 07/02/2017