39. ´Aqiydah ya Ashaa´irah juu ya Qur-aan haingii akilini

Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah) ana tafiti nzuri juu ya maudhui haya ambapo anasambaratisha tafsiri yao hii. Baada ya kuthibitisha kuwa maneno Yake Allaah (Ta´ala) ni ya kale, akasema:

”Maneno ni sifa kamilifu. Anayezungumza ni mkamilifu zaidi kuliko ambaye hazungumzi. Ni kama ambavo anayejua na kuweza ni mkamilifu zaidi kuliko ambaye hajui na hawezi. Anayezungumza kwa utashi na uwezo Wake ni mkalilifu zaidi kuliko ambaye hazungumzi kwa utashi na uwezo Wake, ikiwa jambo hilo ni lenye kuingia akilini. Kutokana na misingi ya Salaf mtu anaweza kuthibitisha kuwa ima akawa anaweza kuzungumza au si mwenye kuweza kuzungumza. Asiyeweza kuzungumza ni bubu, na ambaye anaweza kuzungumza lakini asizungumze amenyamaza.

Kwa mujibu wa Kullaabiyyah maneno si kitu chenye kuwezekana, na kwa ajili hiyo hawawezi kujengea hoja hiyo. Hapa kutasemwa kwamba haya yanajulisha ukale wa maneno, lakini yanajulisha ukale wa maneno maalum bila uwezo na matakwa yake au kwamba daima alikuwa ni Mwenye kuzungumza kwa utashi na uwezo Wake? Maoni ya kwanza ni ya Kullaabiyyah, maoni ya pili ni ya Salaf, maimamu na Ahl-ul-Hadiyth was-Sunnah. Kwa hivyo majulisho yake ni yale ya pili na si ya kwanza. Kwa sababu ni jambo lisiloingia akilini kuthibitisha maneno yasiyotokana na matakwa na uwezo – na hukumu ya kitu ni matokeo ya kule kukifiria. Kwa huyu anayetetea hoja hii na mwingine mwenye busara aambiwe kuwa ni jambo lisiloingia akilini mtu akazungumza pasi na matakwa na kutaka kwake. Itawezekanaje basi kutumia dalili ya kiakili juu ya kuthibitisha kitu kisichoingia akilini? Kusema kwamba ikiwa hazungumzi maana yake ni kwamba ni bubu na amenyamaza, ni hoja tu ambayo inaweza kutumiwa juu ya maneno yaliyo na herufi na sauti. Hakika aliye hai akipoteza uhai hawi mwenye kuzugumza. Ima akawa ni muweza wa kuzungumza lakini akaamua kunyamaza na kutozungumza, au akawa si muweza wa kuzungumza, jambo ambalo maana yake ni kwamba ni bubu.

Kuhusu yale wanayoyatetea ya maneno ya ndani ya nafsi, ni jambo lisiloingia akilini kwamba mwenye kuyakosa ima akawa amenyamaza au bubu. Na kama kweli kitu kama hicho kinapatikana, basi hakijulishi kuwa yule mwenye kukosa kitu hicho lazima awe mwenye kunyamaza au ni bubu. Jengine ni kwamba bado hamjathibitisha ni kitu gani yale maneno ya kale na ya ndani ya nafsi. Bali bado hamjayafikiria – na hukumu ya kitu ni matokeo ya kule kukifiria. Ni vipi basi mtu anaweza kuthibitisha kitu ambacho hajakifikiria? Ndio maana Abu Sa´iyd bin Kullaab – kiongozi juu ya suala hili – hakuwahi kutaja hoja inayoingia akilini katika kubainisha jambo hilo. Bali alichosema ni:

”Ni maana inayopingana na ukimya na ububu.”

Ukimya na ububu vinaweza kufikiria pale yanapothibitishwa kwanza maneno. Aliyenyamaza ni yule asiyezungumza, bubu ni yule asiyekuwa na uwezo wa kuzungumza au ambaye amepatwa na jambo linalomzuia yeye kuweza kutamka. Kwa ajili hiyo aliyenyamaza na bubu hawezi kutambulika mpaka kwanza yatambulike maneno, na wala maneno hayawezi kutambulika mpaka kwanza atambulike aliyenyamaza na bubu. Hivyo ikadhihirika kuwa hawakuyafikiria wala hata kuyathibitisha yale waliyoyasema. Bali uhakika wa mambo ni kwamba mtazamo wao inapokuja katika maneno umefanana na mtazamo wa manaswara katika neno na ´Aqiydah yao juu ya hypostases, utatu na umoja. Wao pia wanasema mambo wasiyoyafikiria wala wasiyoyabainisha. Mitume (´alayhimus-Salaam) wanaposema jambo tunaloshindwa kulifikiria, basi ni lazima kuwasadikisha. Lakini yale yanayothibitishwa kwa kutumia akili ni lazima kwanza aweze kuyafikiria yule mwenye kuyatetea. Vinginevyo atakuwa amezungumza kwa ujinga. Manaswara wanazungumza pasi na elimu na kwa ajili hiyo maneno yao yakawa yenye kujigonga na yasiyoingia akilini. Vilevile anayezungumza juu ya Allaah pasi na elimu maneno yake yanakuwa yenye kujigonga na yasiyoingia akilini. Kwa ajili hiyo miongoni mwa mambo waliyokuwa wakisimangwa kwayo ni kwamba wanajengea hoja katika msingi wa dini yao na utambuzi wa uhakika wa maneno – kwa maneno ya Allaah na maneno ya viumbe wote  – kwa kutumia hoja mashairi ya mkristo anayeitwa al-Akhtwal, ambaye amesema:

Maneno yanakuwa moyoni

lakini ulimi unajulisha yale yaliyomo moyoni

Wako waliosema kuwa si yeye ambaye alisema hivo. Kwa kukadiria kuwa ni mashairi yake, halisia za kiakili, au maneno yanayotamkwa na wanadamu wote, haurejei kwa washairi elfu moja, sembuse kurejeshwa kwa mshairi mmoja ambaye jina lake ni al-Akhtwal.”[1]

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (6/294-297).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Aqiydah at-Twahaawiyyah – Sharh wa Ta´liyq, uk. 57-61
  • Imechapishwa: 01/10/2024