Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Mfano wa hilo, ni pale baadhi ya washirikina wanaposema:

أَلَا إِنَّ أَوْلِيَاءَ اللَّـهِ لَا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ

“Tanabahi! Hakika mawalii wa Allaah hawana khofu juu yao na wala hawatohuzunika.” (10:62)

Au anasema ya kwamba uombezi ni haki, au ya kwamba Mitume wana jaha mbele ya Allaah. Au akataja maneno fulani kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akijengea dalili kutoka kwa kitu katika batili yake, ilihali wewe hufahamu maana ya maneno aliyoyataja. Mjibu kwa kusema:

“Kwa hakika Allaah amesema katika Kitabu Chake ya kwamba wale ambao moyoni mwao mna upotofu, wanaacha [Aayah] zilizo wazi na wanafuata [Aayah] zenye kutatiza.”

MAELEZO

Halafu mtunzi (Rahimahu Allaah) akatoa mfano namna ambavyo mshirikina anaweza kukujia na kukwambia:

“Allaah si anasema:

أَلَا إِنَّ أَوْلِيَاءَ اللَّـهِ لَا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ

“Tanabahi! Hakika mawalii wa Allaah hawana khofu juu yao na wala hawatohuzunika.”?

Je, mawalii si wana jaha mbele ya Allaah (´Azza wa Jall)? Je, uombezi ni jambo limethibiti kwa Qur-aan na Sunnah?

Jibu kwa kusema:

“Ndio. Yote haya ni haki. Lakini hata hivyo hakuna dalili yoyote kwako ya kuwashirikisha mawalii hawa, Mitume au watu hawa ambao wana haki ya kushufaia mbele ya Allaah (´Azza wa Jall). Madai yako yote juu ya kwamba yanafahamisha juu ya unachokidai ni madai ya batili. Mtu wa batili pekee ndiye awezaye kujengea dalili kama hiyo. Wewe si mwengine isipokuwa ni mmoja katika wale ambao Allaah amesema juu yao:

فَأَمَّا الَّذِينَ فِي قُلُوبِهِمْ زَيْغٌ فَيَتَّبِعُونَ مَا تَشَابَهَ مِنْهُ

“Basi wale ambao katika nyoyo zao mna upotovu hufuata zile zenye kutatiza.” (03:07)

Lau ungelifasiri Aayah hizi Aayah zenye kutatiza kwa Aayah zilizo wazi, basi ungelijua kuwa hapa huna dalili yoyote.”

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 57
  • Imechapishwa: 11/11/2023