29. Mambo yote yamebainishwa katika Uislamu

Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah amesema:

Ni vipi itayumkinika Kitabu hicho, Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) huyo na viumbe bora wa Allaah baada ya Mitume hawakuimairi maudhui hii kwa njia zote ziwezekanavyo?  Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliufunza Ummah wake kila kitu mpaka adabu za chooni.

MAELEZO

Hapa Shaykh (Rahimahu Allaah) anawakilisha matokeo ya utangulizi wake. Itayumkinika vipi Qur-aan, Sunnah zake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) hawakutubainishia ´Aqiydah sahihi? Iweje wasiwe na ujuzi wa majina na sifa za Allaah kimaneno na kivitendo? Hapa wanaraddiwa wale watu wanaowatuhumu Maswahabah eti walikuwa hawajui maana ya majina na sifa hizi tofauti na al-Jahm bin Swafwaan na wenzake ndio ambao walikuwa wanajua maana yake na wakazibainisha. Kwa maana nyingine wanamaanisha kuwa hapo kabla jambo lilikuwa limefungwa na watu hawalijui; walikuwa wakiyarudiarudia maneno pasi na kufahamu maana yake. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwafunza watu mpaka adabu za kukidhi haja. Myahudi mmoja alimwambia Salmaan (Radhiya Allaahu ´anh):

“Mtume wenu amewafundisha mpaka namna ya kukidhi haja.” Akasema: “Ndio. Ametukataza kuelekea Qiblah wakati tunapofanya haja kubwa au ndogo. Ametukataza vilevile kujisafisha chini ya mawe matatu, mkono wa kulia, kinyesi au mfupa.”[1]

Ni vipi basi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) asiibainishe ´Aqiydah ambayo ndio jambo muhimu zaidi? Hakuna jambo lolote la kidini lenye manufaa isipokuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amelibainisha. Walioyajua wameyajua, na ambao hawakuyajua hawakuyajua. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakufa isipokuwa baada ya kukamilisha Shari´ah na kukamilisha ubainifu. Ni jukumu la Allaah Shari´ah kukamilika na ni jukumu la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kukamilisha ubainifu. Kitendo cha baadhi ya watu kutokusoma, hawajui au hawataki kujua sio hoja. Ubainifu upo. Ni vipi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) atabainishia watu adabu za kukidhi haja na asiwafunze ´Aqiydah mpaka walipokuja watu hawa eti wao ndio wawabainishie watu?

[1] Muslim (262).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaaa al-Hamawiyyah, uk. 58-60
  • Imechapishwa: 31/07/2024