Miongoni mwa vipaumbele vyake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni kwamba alichagua utumwa badala ya ufalme. Siku ya Ufunguzi kuna bwana mmoja aliyeanza kutetemeka kwa khofu mbele yake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), ambapo (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:

“Tulia. Mimi si mwana wa mfalme; mimi ni mtoto wa mwanamke wa Quraysh ambaye alikuwa akila nyama iliyokaushwa.”[1]

Imesihi pia kwamba amesema (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam):

”Msinisifu kwa kupindukia kama manaswara walivomsifu ´Iysaa bwana wa Maryam kwa kupindukia. Hakika si vyengine mimi ni mja wa Allaah. Hivyo basi semeni: ”Mja na Mtume wa Allaah”.”[2]

Imaam Ahmad (Rahimahu Allaah) amesema: Muhammad bin Fudhwayl ametuhadithia, kutoka kwa Amaarah, kutoka kwa Abu Zur´ah, kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh), ambaye amesema:

“Jibriyl alipokuwa amekaa kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), akatazama juu mbinguni na akamuona Malaika akishuka. Jibriyl akasema: “Malaika huyu hajashuka tangu alipoumbwa isipokuwa sasa.” Aliposhuka, akasema: “Ee Muhammad! Mola wako amenituma kwako na anakuuliza kama unataka kuwa mfalme na Mtume au mja na Mtume.” Jibriyl akasema: ”Mnyenyekee Mola wako, ee Muhammad.” Akasema: “Mja na Mtume.”[3]

Miongoni mwa Hadiyth za Yahyaa bin Kathiyr, ambazo kuna Swahabah anayekosekana katika cheni ya wapokezi, ni kwamba Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amesema:

“Nakula kama anavyokula mja na ninakaa kama anavyokaa mja – hakika si vyenginevyo mimi ni mja.”[4]

Ameipokea Ibn Sa’d katika “at-Twabaqaat al-Kubraa”. Kupitia kwa Abu Ma´shar amesimulia pia al-Maqburiy, kutoka kwa ´Aaishah (Radhiya Allaahu anhaa), ambaye amesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amesema:

Akanijia Malaika na kusema: “Mola wako anakusalimu kwa amani na anakuuliza unataka kuwa Nabii na mfalme au mtumwa na mjumbe. Jibriyl alinionyesha kunyenyekea, hapo nikasema: “Mja na Mtume.” Akasema: “Baada ya hapo, Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa hapendi kula hali ya kuegemea. Akasema: “Nakula kama mtumwa na nakaa kama mtumwa.”[5]

Miongoni mwa Hadiyth za az-Zuhriy (Rahimahu Allaah), ambazo kuna Swahabah anayekosekana katika cheni ya wapokezi, ni kwamba alisema:

“Tumefikiwa na khabari kwamba Malaika alikuja kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kwa mara ya kwanza. Pamoja naye alikuwa na Jibriyl. Wakati Jibriyl ( ́alayhis-Salaam) akiwa kimya, Malaika akasema: “Mola wako amekupa chaguo kati ya kuwa mfalme na Mtume au mja. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamtazama Jibriyl (‘alayhis-Salaam) katika hali ya kumwomba ushauri, ndipo akamwashiria anyenyekee. Ndipo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akasema: “Mtume na mja.” az-Zuhriy amesema: “Wamesema eti kuwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) hakuwahi kula chakula kwa kuegemea baada ya hapo mpaka alipoaga dunia.”[6]

[1] Ibn Maajah (3212) na al-Haakim (3/50), ambaye ameisahihisha kwa mujibu wa sharti za al-Bukhaariy na Muslim. Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika “as-Swahiyhah” (1876).

[2] al-Bukhaariy (3445), at-Tirmidhiy katika ”ash-Shamaa-il al-Muhammadiyyah” (2/161), ad-Daarimiy (2/230), at-Twayaalisiy (25) na Ahmad (154, 164, 331 na 391).

[3] Ahmad (2/231) na Ibn Hibbaan (2137). Wote wawili wameipokea kupitia kwa Muhammad bin Fudhwayl, kutoka kwa ´Amaarah bin al-Qa´qaa´, kutoka k wa Abu Zur´ah, kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”as-Swahiyhah” (¾).

[4] Ibn Sa´d (1/371). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika “Swahiyh-ul-Jaamiy´” (8).

[5] Ibn Sa´d (1/281).

[6] Abdur-Razzaaq (5247).

  • Muhusika: Imaam Zayn-ud-Diyn ´Abdur-Rahmaan bin Rajab al-Hanbaliy (afk. 795)
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Khushuu´ fiys-Swalaah, uk. 98-102
  • Imechapishwa: 24/11/2025