Abu Ja´far at-Twahaawiy (Rahimahu Allaah) amesema:

140 – Tunaamini kufufuliwa, kulipwa kwa matendo, uonyeshwaji, hesabu, kusoma ndani ya madaftari, thawabu, adhabu na Njia na Mizani siku ya Qiyaamah.

MAELEZO

Baada ya maisha ya ndani ya kaburi watu watafufuliwa kutoka ndani ya makaburi yao. Makaburi haya yanaweka na kuhifadhi miili. Itapofika wakati wa kufufuliwa basi Allaah ataianzisha upya miili hii kama alivyoiumba mara ya kwanza:

كَمَا بَدَأْنَا أَوَّلَ خَلْقٍ نُّعِيدُهُ ۚ وَعْدًا عَلَيْنَا ۚ إِنَّا كُنَّا فَاعِلِينَ

“Kama Tulivyoanza uumbaji umbo la mwanzo tutalirudisha. Hiyo ni ahadi juu Yetu – hakika sisi ni wafanyao.”[1]

Miili itarudishwa kama ilivyokuwa kwa njia ya kwamba watu watajuana kama ilivyokuwa mwanzo. Kisha baada ya hapo Allaah atamwamrisha Israafiyl apulize baragumu kwa mara ya pili ambapo roho zitaruka kuingia katika miili yake.

Mahala pa mkusanyiko ni maeneo ambapo nyumati zitakusanyika. Allaah atawakusanya wa mwanzo na wa mwisho baada ya kufufuliwa. Allaah juu ya kila jambo ni muweza. Kuamini kufufuliwa ni moja katika zile nguzo sita za imani, kama inavosema Hadiyth.

[1]21:104

  • Muhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat al-Mukhtaswarah ´alaal-´Aqiydah at-Twahaawiyyah, uk. 198
  • Imechapishwa: 19/01/2025