18. Ni ipi hukumu ya mwenye kufunga ilihali ni mwenye kuacha swalah?

Swali 18: Ni ipi hukumu ya mwenye kufunga ilihali ni mwenye kuacha swalah? Je, funga yake ni sahihi?

Jibu: Maoni yenye nguvu ni kwamba kuacha swalah kwa makusudi mtu anafuru ukafiri mkubwa kwa kitendo hicho. Hivyo swawm yake wala ´ibaadah zake zengine hazisihi mpala pale atapotubia kwa Allaah (Subhaanah). Allaah (´Azza wa Jall) amesema:

وَلَوْ أَشْرَكُوا لَحَبِطَ عَنْهُم مَّا كَانُوا يَعْمَلُونَ

“Lau wangemshirikisha bila shaka yangeporomoka yale waliyokuwa wakitenda.”[1]

Kuna Aayah na Hadiyth nyingi zilizo na maana yake.

Wapo wanachuoni wengine wenye kuona kwamba mtu hakufuru kwa kitendo hicho na wala swawm na ´ibaadah zake zengine haziharibiki midhali ni mwenye kukubali uwajibu wake lakini hata hivyo ameacha swalah kwa sababu ya kuzembea na uvivu. Lakini maoni yenye nguvu ni yale ya kwanza yanayosema kwamba anakufuru kwa kuiacha kwake kwa makusudi japokuwa atakiri uwajibu wake. Zipo dalili nyingi  ikiwa ni pamoja na maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Baina ya mtu na ukafiri na shirki ni kuacha swalah.”

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Jaabir bin ´Abdillaah (Radhiya Allaahu ´anhumaa).

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Ahadi iliopo baina yetu sisi na wao ni swalah. Hivyo basi, yule mwenye kuiacha amekufuru.”

Ameipokea Imaam Ahmad na waandishi wane wa “as-Sunan” kwa cheni ya wapokezi Swahiyh kupitia kwa Buraydah bin al-Huswayb al-Aslamiy (Radhiya Allaahu ´anh). ´Allaamah Ibn-ul-Qayyim (Radhiya Allaahu ´anh) amelizugumza hilo vya kutosha katika kijitabu chake cha kipekee katika “Ahkaam-us-Swalaah wa Tarkiyhaa”. Ni kijitabu chenye faida na kizuri ambacho ni vizuri kukirejelea na kufaidika nacho.

[1] 06:88

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdllaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: As-ilah Muhimmah tata´alaqah bisw-Swiyaam, uk. 24-25
  • Imechapishwa: 30/04/2019