123 – Muhammad bin ´Abdillaah bin al-Mubaarak ametuhadithia: Yaziyd bin Haaruun ametuhadithia: ´Aaswim bin Muhammad ametukhabarisha, kutoka kwa baba yake, kutoka kwa Ibn ´Umar, kutoka kwa ´Umar:

“Anayenyenyekea kwa ajili Yangu namna hii, Humuinua namna hii.”

Kwa mujibu wa Yaziyd ni lazima kwamba ´Umar aliisimulia kutoka kwa Mtume  (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) namna hiyo.

Hadiyth hii ni ngeni.

124 – Fadhwl bin Sahl ametuhadithia: Abu Nadhwr ametuhadithia: Muhammad bin Twalhah ametuhadithia, kutoka kwa Muhammad bin Juhaadah, kutoka kwa al-Hasan, aliyesimulia ya kwamba Mtume wa Allaah  (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mja hajiinui nafsi yake isipokuwa Allaah humshusha, na hajinyenyekezi isipokuwa Allaah (´Azza wa Jall) humuinua.”

125 – Salm bin Junaadah ametuhadithia: Muhammad bin Fudhwayl ametuhadithia, kutoka kwa ´Imaarah bin al-Qa´qaa´, kutoka kwa Abu Zur´ah, kutoka kwa ´Amaarah, kutoka kwa Abu Hurayrah, ambaye ameeleza:

”Jibriyl aliketi karibu na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Alipotazama mbinguni akamuona Malaika anateremka. Jibriyl akamwambia: “Huyu ni Malaika hajawahi kushuka tangu alipoumbwa hadi siku ya Qiyaamah.” Aliposhuka, akasema: “Ee Muhammad! Mola wako amenituma kwako na anakuuliza: ”Akufanye uwe Mtume na mfalme au mja na Mtume?” “Jibriyl akasema: ”Jinyenyekeze kwa Mola wako.” Mtume akasema: “Bali niwe mja na Mtume.”

126 – Ishaaq bin Ismaa´iyl ametuhadithia: Abu Mu´aawiyah ametuhadithia, kutoka kwa al-Ash´ath, kutoka kwa al-Musayyab bin Raafiy´, kutoka kwa ´Aamir bin ´Abdillaah, aliyesema:

“Anayejinyenyekeza kwa unyenyekevu basi Allaah humuinua, na anayejivuna kwa kujikweza basi Allaah humshusha.”

127 – ´Abdur-Rahmaan bin Swaalih ametuhadithia: Abul-Qaasim amenihadithia:

”Nilikuwa kwa Ibn Shubrumah wakati alipokuja bwana mmoja akamwambia: “Je, nisikuhadithie Hadiyth iliyonifikia kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)?” Ibn Shubrumah akasema: “Ilete, huenda ukaleta Hadiyth nzuri.” Akasema: “Kuna mambo manne Allaah hampi mtu isipokuwa yule ampendaye.” Ibn Shubrumah akauliza: “Ni yapi hayo?” Akasema: “Kunyamaza, nayo ndiyo mwanzo wa ´ibaadah, kumtegemea Allaah, unyenyekevu na kuipa kisogo dunia.”

  • Muhusika: Imaam Abu Bakr ´Abdullaah bin Muhammad bin Abiyd-Dunyaa (afk. 281)
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Kitaab-ul-Khumuul wat-Tawaadhwu´, uk. 159-166
  • Imechapishwa: 04/02/2026