Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) amesema:

وَدَاعِيًا إِلَى اللَّـهِ بِإِذْنِهِ

”… na mlinganiaji kwa Allaah kwa Idhini Yake… ”[1]

Moja miongoni mwa majukumu ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni kwamba anawalingania watu katika imani na kumpwekesha Allaah:

قُلْ هَـٰذِهِ سَبِيلِي أَدْعُو إِلَى اللَّـهِ ۚ عَلَىٰ بَصِيرَةٍ أَنَا وَمَنِ اتَّبَعَنِي

“Sema: “Hii ndio njia yangu: nalingania kwa Allaah, juu ya ujuzi na umaizi – mimi na anayenifuata.”[2]

ادْعُ إِلَىٰ سَبِيلِ رَبِّكَ بِالْحِكْمَةِ وَالْمَوْعِظَةِ الْحَسَنَةِ ۖ وَجَادِلْهُم بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ

“Lingania katika njia ya Mola wako kwa hekima na mawaidha mazuri na jadiliana nao kwa ambayo ni mazuri zaidi.”[3]

Mtume alikuwa ndio kichwa cha wanaolingania kwa Allaah (´Azza wa Jall). Kulingania kwa idhini ya Allaah maana yake ni kulingania kwa Shari´ah Yake. Haijuzu kwa yeyote kulingania pasi na dalili, elimu na Shari´ah kutoka kwa Allaah. Ni lazima kwa mlinganizi awe na elimu. Vinginevyo ni vipi atawalingania watu hali ya kuwa ni mjinga? Mlinganizi huyu mjinga atawapotosha watu. Lakini akiwalingania kwa elimu na utambuzi atawaongoza katika njia ilionyooka. Kwa sababu elimu hii ni nuru tupu.

وَسِرَاجًا مُّنِيرًا

“… na taa lenye kuangaza.”

Anaangazia watu ulimwengu kwa elimu na ulinganizi wake ili watu watoke katika viza vya shirki na kufuru. Ni kama ambavyo jua linaangaza ulimwengu ili watu waweze kupita njia ya umaizi na ilioangazwa:

تَبَارَكَ الَّذِي جَعَلَ فِي السَّمَاءِ بُرُوجًا وَجَعَلَ فِيهَا سِرَاجًا وَقَمَرًا مُّنِيرًا

”Amebarikika ambaye amefanya buruji katika mbingu na amefanya humo taa yenye mwanga mkali na mwezi wenye nuru.”[4]

Siraji ni jua. Allaah amelifanya jua ni siraji inayoangaza ulimwengu huu ili viza viondoke. Ni kama ambavyo watu walikuwa ndani ya viza vya ujinga, vya kufuru na vya shirki ambapo Allaah akawaokoa kupitia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambaye aliwalingania katika Tawhiyd na elimu. Elimu zote za manufaa zilizopo ulimwenguni zinarejea katika ujumbe ambao Allaah alimtumiliza kwao Mtume huyu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

[1] 33:46

[2] 12:108

[3] 16:125

[4] 25:61

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat at-Tawdhwiyhiyyah ´alaa Muqaddimat-il-Fatwaaa al-Hamawiyyah, uk. 42-43
  • Imechapishwa: 28/07/2024