2 – Upokezi wa ´Abdullaah bin Wahb[1]

al-Bayhaqiy amesema: Abu ´Abdillaah al-Haafidhw Ahmad bin Muhammad bin Ismaa’iyl Mihraan[2] ametukhabarisha: Baba yangu[3] ametuhadithia: Abur-Rabiy´[4], mwana wa kaka yake Rishdayn bin Sa’d: Nimemsikia ´Abdullaah bin Wahb akisema:

“Tulikuwa kwa Maalik bin Anas alipoingia wakati ambapo bwana mmoja aliingia na kusema: “Ee Abu ´Abdillaah!

الرَّحْمَـٰنُ عَلَى الْعَرْشِ اسْتَوَىٰ

”Mwingi wa rehema amelingana juu ya ´Arshi.”[5]

Amelingana juu vipi?” Maalik aliinamisha kichwa chake na kuanza kutokwa na jasho. Kisha akainua kichwa chake na kusema: “Mwingi wa rehema amelingana juu ya ´Arshi kama alivyojieleza Mwenyewe. Haipaswi kuulizwa juu ya namna, kwa sababu kuulizia namna Kwake ni jambo lisilokuwepo. Wewe ni mtu mbaya, mzushi. Mtoeni nje!” Wakamtoa nje.”[6]

adh-Dhahabiy amesema:

“al-Bayhaqiy ameisimulia kwa cheni ya wapokezi Swahiyh kupitia kwa Abur-Rabiy’ ar-Rushdayniy, kutoka kwa Ibn Wahb.”[7]

Haafidhw Ibn Hajar amesema:

“al-Bayhaqiy ameisimulia kwa cheni ya wapokezi nzuri kupitia kwa Ibn Wahb.”[8]

[1] Abu Muhammad ´Abdullaah bin Wahb bin Muslim al-Qurashiy al-Fihriy. Amepokea kutoka kwa watu wengi. Alikuwa ni mtu madhubuti kwa mujibu wa Ibn Ma’iyn na Abu Zur´ah. Ahmad bin Hanbal amesema juu yake:

“Ni usahihi na kuthibiti kulikoje kwa masimulizi yake.”

Alikuwa miongoni mwa wasimulizi thabiti zaidi kutoka kwa Maalik. Haaruun bin ´Abdillaah az-Zuhriy:

“Pindi watu walipokuwa wakitofautiana juu ya kitu kutoka kwa Maalik, wanasubiri kufika kwa Ibn Wahb ili wamuulize juu ya kitu hicho.”

Abu Musw’ab amesema:

“Maswali ya Ibn Wahb kwa Maalik ni sahihi.”

Ibn Hajar amesema juu yake:

“Alikuwa ni mtu madhubiti, mwenye kuhifadhi na mfanya ´ibaadah.” (Taqriyb-ut-Taqriyb (3718))

Alifariki mnamo 197. Tazama “Tahdhiyb-ul-Kamaal” (16/277-286).

[2] Abul-Hasan Ahmad bin Muhammad bin Ismaa´iyl bin Mihraan al-Ismaa´iyliy an-Naysaabuuriy. adh-Dhahabiy amesema juu yake:

“Abul-Hasan al-Ismaa´iyliy an-Naysaabuuriy – mwadilifu.” (Taariykh-ul-Islaam, uk. 187)

as-Sam´aaniy amesema:

“Ameyasikia mengi kutoka kwa baba yake.” (al-Ansaab (1/155))

[3] Muhammad bin Ismaa´iyl bin Mihraan al-Ismaa´iyliy. al-Haakim amesema juu yake:

”Ni mmoja katika nguzo za Hadiyth Naysaabuur. Alisafiri na kutambulika sana…  Alikuwa ni madhubuti na mwaminifu.”

Ibraahiym bin Abiy Twaalib amesema:

“Hakuna aliyetusimulia masimulizi ya Maalik kwa ubora kama al-Ismaa’iyliy.

Alikufa mwaka wa 295. Tazama “Siyar A´laam-in-Nubalaa’” (14/117-118).

[4] Abur-Rabiy’ Sulaymaan bin Daawuud bin Hammaad bin Sa’d al-Mahriy. Babu yake alikuwa Hammaad bin Sa’d, kaka yake Rishdayn bin Sa’d. Alifariki mwaka 253. al-Mizziy amemwandikia wasifu katika “Tahdhiyb-ul-Kamaal” (11/409-410) na akataja kwamba alikuwa mwaminifu kwa mujibu wa an-Nasaa’iy.

[5] 20:05

[6] al-Asmaa’ was-Swifaat (2/304). adh-Dhahabiy ameitaja katika “al-´Uluww”, uk 141 kwa ufupisho, na “al-Arba´iyn fiy Swifaat Rabb-il-Aalamiyn”, uk. 80. Tazama “Siyar A´laam-in-Nubalaa’” (8/100).

[7] Mukhtwasar-ul-´Uluww, uk. 141.

[8] Fath-ul-Baariy (13/406-407).

  • Muhusika: Shaykh ´Abdur-Razzaaq bin ´Allaamah ´Abdil-Muhsin al-´Abbaad al-Badr
  • Tarjama: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Athar al-Mash-huur ´an-il-Imaam Maalik fiy Swifat-il-Istiwaa’, uk. 32-34
  • Imechapishwa: 28/11/2025