12. Ni ipi hukumu ya kufanya Tayammum licha uwepo wa maji?

Swali 12: Ni ipi hukumu ya kufanya Tayammum licha uwepo wa maji[1]?

Jibu: Nimeelezwa na baadhi ya watu waaminifu kuwa baadhi ya watu wa mashambani hutumia Tayammum kwa ajili ya swalah licha ya kuwa maji yanapatikana kwao, jambo ambalo ni maovu makubwa ambayo ni lazima kuyazindua. Hivo ni kwa sababu kutawadha kwa ajili ya kuswali ni sharti miongoni mwa sharti za kusihi kwa swalah wakati wa kupatikana kwa maji. Amesema (Ta´ala):

وَإِن كُنتُمْ جُنُبًا فَاطَّهَّرُوا ۚ وَإِن كُنتُم مَّرْضَىٰ أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ أَوْ جَاءَ أَحَدٌ مِّنكُم مِّنَ الْغَائِطِ أَوْ لَامَسْتُمُ النِّسَاءَ فَلَمْ تَجِدُوا مَاءً فَتَيَمَّمُوا صَعِيدًا طَيِّبًا فَامْسَحُوا بِوُجُوهِكُمْ وَأَيْدِيكُم مِّنْهُ

“Mkiwa na janaba, basi jitwaharisheni na mkiwa wagonjwa au mko safarini au mmoja wenu akija kutoka msalani au mmewagusa wanawake kisha hamkupata maji, basi fanyeni Tayammum kwa ardhi kwa juu panguseni kwayo nyuso zenu na mikono yenu.”[2]

al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kuwa amesema:

“Allaah hakubali swalah ya mmoja wenu pindi anapopata hadathi mpaka atawadhe.”[3]

Allaah ameruhusu kufanya Tayammum na akafanya ichukue nafasi ya wudhuu´ katika hali kukosekana kwa maji au kushindikana kutumiwa kwa ajili ya maradhi au mfano wake kutokana na Aayah iliyotangulia. Vilevile amesema (Ta´ala):

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَقْرَبُوا الصَّلَاةَ وَأَنتُمْ سُكَارَىٰ حَتَّىٰ تَعْلَمُوا مَا تَقُولُونَ وَلَا جُنُبًا إِلَّا عَابِرِي سَبِيلٍ حَتَّىٰ تَغْتَسِلُوا ۚ وَإِن كُنتُم مَّرْضَىٰ أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ أَوْ جَاءَ أَحَدٌ مِّنكُم مِّنَ الْغَائِطِ أَوْ لَامَسْتُمُ النِّسَاءَ فَلَمْ تَجِدُوا مَاءً فَتَيَمَّمُوا صَعِيدًا طَيِّبًا فَامْسَحُوا بِوُجُوهِكُمْ وَأَيْدِيكُمْ ۗ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَفُوًّا غَفُورًا

“Enyi walioamini! Msikaribie swalah na hali mmelewa mpaka mjuekile mnachokisema na wala mkiwa mna janaba isipokuwa mmo safarini mpaka muoge josho na mkiwa wagonjwa au safarini au mmoja wenu ametoka msalani au mmewagusa [kuwajamii] wanawake kisha hamkupata maji, basi fanye Tayammum kwa ardhi safi ya mchanga – pakeni nyuso zenu na mikono yenu. Hakika Allaah ni Mwingi wa kusamehe, Mwingi wa kusamehe.”[4]

´Imraan bin Huswayn (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwa kusema: “Tulikuwa pamoja na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika safari moja ambapo akawaswalisha watu. Tahamaki akajitokeza Mu´taziliy mmoja. Akasema: “Ni kipi kilichokuzuia kuswali?” Akasema: “Nimepatwa na janaba na sina maji.” Akamwambia (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Lazimiana na mchanga. Kwani hakika unakutosha.”[5]

Kutokana na haya inapata kufahamika kwamba haijuzu kufanya Tayammum kwa ajili ya kuswali panapokuwepo maji na uwezo wa kuyatumia. Bali ni lazima kwa muislamu kuyatumia maji wakati wa kutawadha na kuoga kwake kutokamana na janaba popote anapokuwepo muda wa kuwa anaweza kuyatumia. Si mwenye kupewa udhuru kwa kuyaacha na akatosheka na kufanya Tayammum. Katika hali hiyo swalah yake itakuwa si sahihi kwa kukosekana sharti miongoni mwa sharti zake ambayo; kujisafisha kwa maji wakati wa kuweza kuyatumia.

Watu wengi wa mashambani – Allaah awaongoze – na wengineo ambao wanaenda kwenye pikniki hufanya Tayammum ilihali wanayo maji mengi na ni wepesi kule kuyafikia. Hapana shaka kwamba kufanya hivo ni kuchukulia wepesi kubaya na kitendo kiovu ambacho haitakiwi kukifanya, kwa sababu kinaenda kinyume na dalili zilizowekwa katika Shari´ah.

Muislamu anapewa udhuru wa kufanya Tayammum pindi maji yanapokuwa mbali naye, amebaki na maji madogo ambayo atayatumia kwa ajili ya kuokoa maisha, familia na wanyama wake.

Kwa hivyo ni lazima kwa kila muislamu popote anapokuwa kumcha Allaah (Subhaanah) katika mambo yote na atahadhari na yale Allaah aliyomuharamishia juu yake ambapo moja wapo ni kufanya Tayammum licha ya kuwepo maji na uwezo wa kuyatumia.

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (10/190-192).

[2] 05:06

[3] al-Bukhaariy (135) na Muslim (536).

[4] 04:43

[5] al-Bukhaariy (344).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Musaafir, uk. 24-27
  • Imechapishwa: 23/02/2022